Zinazobamba

Mafunzo ya Takaful yazidi kusambazwa

 

Taasisi mbalimbali zimeendelea kuandaa mafunzo ya bima ya Kiislamu, Takaful, nchini ili kuongeza uelewa  kwa wadau mbalimbali

Mafunzo haya yanaandaliwa kufuatia mafanikio ya juhudi za Kituo cha Usimamizi na Ushauri wa Masuala ya Huduma za Kifedha za Kiislamu Tanzania (CIFCA) katika kuunganisha nguvu za wadau katika kupigania serikali iruhusu bima hiyo.


Mafunzo ya hivi karibuni yaliandaliwa na Kampuni ya Bima ya Zanzibar (ZCI), ambayo mwakilishi wake alisema anaamini soko la bima ya Kiislamu ni kubwa kwa vile huduma hiyo imekuwa ikiulizwa na wateja.

Kutokana na hitajio hilo, Meneja wa ZCI kanda ya Dar es Salaam na Pwani, Majda Issa, alisema wameandaa mafunzo hayo ya siku moja kwa wadau wakiwemo madalali, mawakala na makampuni ya bima. Lengo la mafunzo hayo limetajwa kuwa ni kuwajengea uelewa wadau hao.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi, mwezeshaji wa semina hiyo ambaye pia ni Mratibu wa CIFCA, Sheikh Muhammad Issa alisema katika semina hiyo, mada mbalimbali ziliwasilishwa ikiwamo kuhusu tofauti ya takaful na bima za kawaida; na namna kampuni na wadau wengine wanavyoweza kupata faida.

“Katika semina hii tulifundisha mfumo mzima wa takaful unavyofanya kazi, na pia namna bima hii itatanua wigo wa matumizi ya huduma za bima kwa ujumla wake kwani kwa sasa bado hali hairidhishi,” alisema Sheikh Muhammad.

“Takwimu zinaonyesha kwamba mchango wa sekta ya bima katika pato la taifa ni asilimia 0.5, lakini malengo ya Mamlaka ya Bima (TIRA) ni kukuza sekta hiyo angalau iweze kuchangia asilimia 1.5,” alisema Sheikh Muhammad.

“CIFCA inafurahishwa kuendesha semina hizi kwa sababu wanakuwa sehemu ya kukuza sekta ya bima hapa nchini na hivyo kuchangia ukuaji wa pato la taifa,” alisema aliongeza Sheikh Muhammad na kuongeza kuwa tayari kuna mabadiliko ya kuongezeka mwamko, licha ya changamoto zilizopo.

“Mwamko ni mkubwa. Kama unavyoona, watu wanajitokeza kwenye semina wakitaka kusikia takaful ni kitu gani hasa, tumeshafanya semina takribani nne na nyingine zinakuja. Kikubwa sasa ni kuongeza jhudi ya kutoa elimu kwa umma naoi li wafahamu takaful,” alisema.

 

Ataja changamoto

Akitaja baadhi ya changamoto zinazokabili bima hii mpya, Sheikh Muhammad alisema idadi ya Masheikh watakaoshiriki moja kwa moja kama wakuu wa bodi ni wachache kwa sababu wengi wao hawajasomea mambo ya takaful.

Katika kukabiliana na changamoto hiyo, Sheikh Muhammad alisema tayari wameanza kuwajengea uwezo masheikh kuhusu uendeshwaji wa biashara ya bima na ana imani kuwa baada ya muda kila kitu kitakuwa sawa.

“Baadhi ya taasisi za wanazuoni wa Kiislamu zimeanza kutoa mafunzo ili kuziba pengo hilo la wataalamu, ambapo moja ya taasisi hizo ni Hay-atul Ulamaa.’ Kama hatua ya mpito ya kutatua tatizo la kukosekana wataalamu Sheikh Muhammad alishauri wataalamu waliopo wahudumie zaidi ya kampuni moja kwani sio dhambi kufanya hivyo.

“Kwa wakati huu ambapo tunafanya jitihada za kuongeza wataalamu wa kuziba pengo la masheikh watakaosimamia takaful, haina maana soko lisimame. Tunaweza kuwatumia waliopo. Imefanyika kwenye benki za Kiislamu na mambo yamekwenda vizuri. Leo hii tunazo huduma za benki za Kiislamu,” alifafanua.

Mshiriki mmoja katika mafunzo hayo Marley Shabaan kutoka taasisi ya Af-Marzom Insurance alisema bima ya takaful ina manufaa makubwa kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla.

“Licha ya kwamba bima hii ina jina la Kiislamu, haina maana kuwa wanunuzi wake ni Waislamu pekee. Hii ni bidhaa kama bidhaa nyingine na anaweza kununua Mtanzania yeyote. Watu wasiogope,” alisema.

Kwa upande wake, Abdallah Rashid Khamis, Mkurugenzi wa FAM Insurance Broker alisema bidhaa ya takaful ni mpya hapa nchini lakini anaamini wateja wapo wengi na biashara itakuwa kubwa zaidi.

Alisema bima ya takaful imekuja kuondoa pengo lililopo la bima, kwani kulikuwa na watu wengi hawatumii bima za kawaida kwa sababu inaenda kinyume na mafundisho ya dini yao, hususan Waislamu.

Itakumbukwa hivi karibuni mamlaka ya TIRA ilizindua miongozo ya bima ya Kiislamu na kinachoendelea sasa ni watu kujipanga kwa ajili ya kusajili kampuni za kutoa huduma hizo.

TIRA ilitangaza kuanzia Mei 1, 2022 kama tarehe ya kuanza kupokea maombi ya kampuni zinazotaka kufanya shughuli hizo. Mchakato wa kuanzisha takaful ulianza toka mwaka 2014 huku CIFCA wakiwa na mchango mkubwa katika kushauri serikali ikubali huduma hizi.










 


 

No comments