MKURUGENZI TGNP AWAPA SOMO WAHARIRI, WAMILIKI WA VYOMBO VYA HABARI,
| Mkurugenzi Mtendaji wa Tgnp Mtandao Bi. Lilian Liundi akizungumza na waandishi wa habari |
SELEMANI MAGALI-DARESALAAM
Mkurugenzi Mtendaji wa Tgnp Mtandao Bi. Lilian Liundi amewashauri wamiliki
na wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari kuanza kuwekeza katika habari za Mabaraza
ya Halmashauri, akisisitiza kuwa kufanya hivyo kutasaidia kuwatua ndoo kichwani
wanawake walio wengi ambao kwa kiasi kikubwa wanaathirika na maamuzi
yanayofanyika katika ngazi hiyo ya maamuzi.
Kitendo cha kuanza kuandika habari za mabaraza ya halmashauri kwa wingi
kutasaidia kumurika changamoto mbalimbali zinazowakabili, jambo litakalosaidia
kupata majawabu kutoka serikalini.
Akizungumza katika semina maalum ya
waandishi wa habari, Bi. Liundi amesema kwa muda mrefu habari za mabaraza ya
Halmashauri zimekuwa sio kipaumbele kwa vyombo vingi vya habari, badala yakae
wamekuwa wakitumia nguvu nyingi kuwekeza katika bunge la Dodoma ili kupata
habari.
Amesema kwa uzoefu ambao wameupata,
wamegundua kuwa vikao vya madiwani ni sehemu muhimu kwa mustakabali wa maisha
ya Mtanzania.
Nataka niseme hapa “ tasnia ya habari
kwa ujumla wake tuwaombe waanze kuwekeza kwa kurusha habari za mabaraza ya
Halmashauri, ifahamike kuwa lile ni bunge kama lilivyo la Dodoma, wakikosea
pale basi kila kitu kinaharibika” Alisema.
Amesema masuala kama ya Maji, Afya,
Zahanati, Shule na mengineyo mengi yanayopaswa kufikishwa katika kata, mitaa au
vijiji bajeti yake yote inafanyika
Halmashauri, kukosa kiviripoti kunachangia kuendelea kudumaza hali za wananchi
hususani Wanawake.
Aidha katika hatua nyingine, Liundi
ametoa wito kwa jamii kuitumia dhana ya utafiti wa uragabishi ili kuweza kuistua jamii
kujitambua na kukua kimaendeleo
Bi. Liundi amesema utafiti wa
Uraghabishi umesaidia kuleta mwamko katika Wilaya Saba ambazo wamezifanyia
utafiti, kwani watu wengi wameweza kuchokozeka na kuanza kuhoji haki zao za
msingi na hivyo kuongeza maendeleo katika kata zao.
Amesema katika utafiti wao
walioufanya, katika wilaya za Kisarawe,
Kinondoni, Ilala, Morogoro, Tarime na Mbeya wameweza kufikia vikundi 222 ,
wanaume 1000 na wanawake 3000 na kugundua kuwa baada ya kufanya uragabishi
kumekuwa na mabadiliko makubwa ya Kimaendeleo.
Aidha Kwa upande wake
afisa mipango, uchambuzi na
machapisho wa TGNP Bw. Deogratius Temba
ameelezea dhana ya bajeti yenye mrengo wa kijinsia kuwa ni bajeti yenye macho
yanayogusa makundi yote ya Kibinadamu.
Alisema kama kuna dhana kuwa bajeti yenye mrengo wa kijinsia
ni kutaka kuwapendelea wanawaake inapaswa kuondoka kwani si tafsiri sahihi ya
bajeti hiyo
Akizungumzia Tafsiri sahihi ya bajeti hiyo, Temba alisema ni
bajeti yenye uhalisia
ambayo itazingatia mahitaji ya kimakundi na hatimaye kitaifa.