Zinazobamba

Ni msimu wa ukame, wananchi wapewa angalizo TMA

 


Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya hali ya hewa Tanzania TMA, Dkt Agnes Kijazi amewashauri wadau wa mamlaka hiyo kujipanga vizuri kukabiliana na msimu wa mvua hafifu unaotarajiwa kuwepo katika kipindi cha msimu wa vuli unaoanza Oktoba hadi Disemba 2022.

Akizungumza na waandishi wa habari Makao Makuu ya Mamlaka hiyo iliyopo Jijini Dar es Salaam, Dkt Kijazi  alisema mifumo ya hali ya hewa inaonyesha kuwa katika msimu wa vuli wa mwaka huu kutakuwa na kipindi kirefiu cha ukavu.

Alisema kutakuwa na mvua za chini ya wastani hadi wastani na kusababisha ukame kwa baadhi ya maeneo na kuwashauri wakulima na wafugaji kujipanga kwa kupanda mazao yanayostamili ukame lakini pia kuweka malisho ya ziada ili kuepuka migogoro.

“Kwa ujumla mvua za chini ya wastani hadi wastani zinatarajiwa katika maeneo mengi ya nchi yanayopata misimu miwili ya mvua kwa mwaka. Msimu unatarajiwa kuanza kwa kuchelewa na kuambatana na mtawanyiko wa mvua usioridhisha.

 Vipindi virefu zaidi vya ukavu vinatarajiwa katika miezi ya Oktoba na Novemba 2022, hata hivyo vipindi vya ongezeko kidogo la mvua vinatarajiwa kujitokeza katika maeneo machache hususan wiki ya tatu na ya nne ya mwezi Disemba, 2022.

 Kwa kawaida msimu wa mvua za Vuli huisha mwezi Disemba, hata hivyo, kunatarajiwa kuwepo na mwendelezo wa mvua kwa mwezi Januari, 2023,” alifafanua Dkt Kijazi.

Aidha alisema kwa Kanda ya Ziwa Viktoria hasa mikoa ya Kagera, Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Mara pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma (wilaya za Kibondo na Kakonko) kutakuwa na mvua za chini ya wastani hadi wastani na kwamba mvua hizo zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Septemba, 2022. Aidha, katika mikoa ya Geita, Shinyanga na Simiyu mvua zinatarajiwa kuanza katika wiki ya nne ya mwezi Oktoba, 2022. Mvua zinatarajiwa kuisha mwezi Januari, 2023.

Kwenye ukanda wa Pwani ya Kaskazini  hasa mikoa ya Morogoro, Pwani, visiwa vya Mafia, Dar es Salaam, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba nako zinatarajiwa kuwa za chini ya wastani hadi wastani na mvua zake zitaanza kunyesha  kati ya wiki ya nne ya mwezi Oktoba na wiki ya kwanza ya mwezi Novemba, 2022 na kuisha kwake Januari 2023.

Pia nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, Mikoa ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro kutakuwa na mvua za chini ya wastani hadi wastani na zinatarajiwa kuanza kati ya wiki ya nne ya mwezi Oktoba na wiki ya kwanza ya mwezi Novemba, 2022.

Katika hatua Mtaalam huyo wa masuala ya hali ya hewa ameishauri jamii kutumia chakula kwa uangalifu, toka ngazi ya kaya hadi taifa kwani msimu ujao ni wa ukame.

Aidha wadau wa Sekta ya mifugo, wavuvi, alisema sekta hiyo itakabiliwa na uhaba wa upatikanaji wa maji hivyo migogoro na watumiaji wengine wa ardhi inaweza kujitokeza, kwa hiyo amewataka wafugaji kujitahidi kuhifadhi malisho pamoja na kufuatilia maelekezo yanayotolewa na maafisa ugani na kujenga tabia ya kufuatilia utabiri wa mamlaka kujua hali inavyokwenda

Pia kwenye Sekta ya utalii na wanyama pori, Dkt Kijazi alisema wanyama pori wanaweza kutoka porini kutafuta malisho sehehmu zingine kwa sababu ya kukosa malisho hifadhini na kuzishauri mamlaka kutoa elimu ili kuwakinga watu wanaozunguka maeneno yao na hatari ya kuvamiwa na wanyama

Kwenye upande wa Usafiri na usafirishaji, alisema ni muda mzuri wa kuendeleza mipango ya uboreshaji wa miundo mbinu, ujenzi unaoendelea basi ufanyike kwa kufuata utabiri wa hali ya hewa.

Nao waandishi wa habari wametakiwa kuendelea kuhabarisha umma habari sahihi kutoka mamlaka kwani kufanya hivyo kunaongeza elimu kwa umma.

“Vyombo vya habari vinashauriwa kufuatilia, kupata na kusambaza taarifa sahihi za mwenendo wa msimu wa Vuli pamoja na taarifa zilizohuishwa za hali ya hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA),” alisema

Pia amewashauri wanahabari kutafuta na kutumia ushauri wa kisekta kutoka kwa wataalam wa sekta mbalimbali ili kuandaa na kusambaza makala za taarifa za kisekta kwa lugha nyepesi inayoeleweka na isiyoleta taharuki, kwa lengo la kuijulisha na kuielimisha jamii juu ya matumizi sahihi ya taarifa za hali ya hewa katika kujikinga na madhara yanayoweza kujitokeza.

 

Hakuna maoni