Ni msimu wa ukame, wananchi fanyieni kazi maelekezo ya TMA
Hivi karibuni Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya
hali ya hewa Tanzania TMA, Dkt Agnes Kijazi aliwasihi wadau mbalimbali wa mamlaka hiyo kujipanga vizuri kukabiliana ukame
ambao unatarajiwa katika msimu wa vuli unaoanza Oktoba hadi Disemba 2022.
Katika nasaha zile, Dkt Kijazi alinukuliwa akisema mifumo ya hali ya hewa
imeonyesha uwepo wa kipindi kirefiu cha ukavu katika maeneo mengi ya nchi, huku
sekta mbalimbali zikitarajiwa kupata athari kwa ukosefu wa mvua.
Alinukuliwa
akisema “Kwa ujumla mvua za vuli zitakuwa chini ya wastani hadi wastani, pia msimu
unatarajiwa kuanza kwa kuchelewa na kuambatana na mtawanyiko wa mvua
usioridhisha,”
Akieleza
mvua zitakavyokuwa, alisema kwa Kanda ya Ziwa Viktoria hasa mikoa ya Kagera,
Geita, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Mara pamoja na kaskazini mwa mkoa wa Kigoma (wilaya
za Kibondo na Kakonko) kutakuwa na mvua za chini ya wastani hadi wastani na
kwamba mvua hizo zinatarajiwa kuanza wiki ya nne ya mwezi Septemba, 2022.
Pia,
katika mikoa ya Geita, Shinyanga na Simiyu mvua zinatarajiwa kuanza katika wiki
ya nne ya mwezi Oktoba, 2022. Mvua zinatarajiwa kuisha mwezi Januari, 2023.
Kwenye ukanda wa Pwani ya Kaskazini hasa mikoa ya Morogoro, Pwani, visiwa vya
Mafia, Dar es Salaam, Tanga pamoja na visiwa vya Unguja na Pemba nako
zinatarajiwa kuwa za chini ya wastani hadi wastani na mvua zake zitaanza
kunyesha kati ya wiki ya nne ya mwezi
Oktoba na wiki ya kwanza ya mwezi Novemba, 2022 na kuisha kwake Januari 2023.
Pia nyanda za Juu Kaskazini Mashariki, Mikoa
ya Arusha, Manyara na Kilimanjaro kutakuwa na mvua za chini ya wastani hadi
wastani na zinatarajiwa kuanza kati ya wiki ya nne ya mwezi Oktoba na wiki ya
kwanza ya mwezi Novemba, 2022.
Kutokana na utabiri huo, Dkt Kijaz ametoa
maelekezo kwa wadau kutumia chakula kwa uangalifu, toka ngazi ya kaya hadi
taifa bila kusahau kutumia mvua chache zitakazojitokeza kwa faida.
Kwa upande wa wafugaji na wavuvi amewashauri
kuhifadhi malisho kwani kuna uwezekano kutokea kwa uhaba wa upatikanaji wa maji.
Ushauri mwingine kwa wafugaji ni kuendelea
kuwataka kufuatilia maelekezo yanayotolewa na maafisa ugani na kujenga tabia ya
kufuatilia utabiri wa mamlaka kujua hali inavyokwenda
Pia kwenye Sekta ya utalii na wanyama pori,
Dkt Kijazi alisema wanyama pori wanaweza kutoka porini kutafuta malisho sehehmu
zingine kwa sababu ya kukosa malisho hifadhini na kuzishauri mamlaka kutoa
elimu ili kuwakinga watu wanaozunguka maeneno yao na hatari ya kuvamiwa na
wanyama
Kwenye upande wa Usafiri na usafirishaji,
alisema ni muda mzuri wa kuendeleza mipango ya uboreshaji wa miundo mbinu,
ujenzi unaoendelea basi ufanyike kwa kufuata utabiri wa hali ya hewa.
Nao waandishi wa habari wametakiwa kuendelea
kuhabarisha umma habari sahihi kutoka mamlaka kwani kufanya hivyo kunaongeza
elimu kwa umma.
“Vyombo vya habari vinashauriwa kufuatilia,
kupata na kusambaza taarifa sahihi za mwenendo wa msimu wa Vuli pamoja na
taarifa zilizohuishwa za hali ya hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania
(TMA),” alisema
Ni matumaini yetu kuwa maelekezo yaliyotolewa
na mamlaka yatafanyiwa kazi na wadau wote kuanzia wakulima, wafugaji, maafisa
mipango miji, wizara husika kwa lengo la kuleta ufanisi kwenye jamii yetu.
Ends
Hakuna maoni
Chapisha Maoni