Zinazobamba

LHRC yataja Chanzo cha mauaji yatokanayo na wivu wa mapenzi



 Mwandishi wetu

KITUO cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimesema chanzo cha mauaji yatokanayo na wivu wa mapenzi kinatokana na migogoro isiyokoma ndani ya ndoa.

 

Hayo yamebaibishwa leo Mei 31, 2022 jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC Wakili Anna Henga akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mwenendo wa mambo kadhaa ya Haki za Binadamu yaliyojitokeza mwezi Aprili na Mei mwaka 2022.

 

“Chanzo cha mauaji yatokanayo na wivu wa mapenzi kinatokana na migogoro isiyokoma ndani ya ndoa licha ya kifungu cha 102 cha Sheria ya Ndoa No. 29 ya Mwaka 1971 kama ilivyofanyiwa marekebisho mwaka 2019 kuwa na chombo cha usuluhishi wa migogoro ya ndoa kabla ya Mahakama kutoa talaka,” amesema Wakili Henga.

 

Amesema mauaji haya huchangiwa na ukosefu wa usawa wa kijinsia na kuwepo kwa vitendo vya ukatili baina ya wenza.

Kwamba kwa mujibu wa taarifa ya haki za Binadamu ya Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu takwimu zinaonesha kwamba kimekuwa na ongezeko kubwa la vitendo vya ukatili.

 

Wakili Henga ameeleza, kwa mwaka 2019 yalikuwa matukio 39,365 mwaka 2020 matukio 42,414 na kwa mwaka 2021 matukio 29,373.

 

“Katika matukio hayo Wanawake waliathirika zaidi ambapo katika matukio yote 111,152 Wanawake walikuwa 66139 sawa na asilimia 60,” amesema Wakili Henga.

 

Aidha ameeleza kuwa mauaji ya wenza pia yamekuwa yakiripotiwa zaidi ambapo kwa mwaka 2021 taarifa hiyo iliripoti matukio 35 ya mauaji ya wenza ambapo Wanawake walikuwa 31 sawa na asilimia 89 huku wanaume wakiwa wanne.

 

Hivyo amesema vitendo vya ukatili vimekuwa vikiendelea kuathiri Wanawake zaidi kwamba ndani ya kipindi cha Mei pekee LHRC imepokea visa saba vya mauaji ya wenza yatokanayo na wivu wa mapenzi ikiwemo tukio lililotokea Jijini Mwanza hivi karibuni.

 

Akizungumzia kuhusu mauaji yatokanayo na wananchi kujichukulia sheria Mkononi, amesema hivi karibuni kumeibuka wimbi la matukio hayo ambayo yalisababisha vifo 473 kwa mwaka 2021 pekee huku mikoa ya Mwanza, Pwani, Rukwa, Lindi, Songwe na Katavi ikiwa kinara.

 

Kuhusu ukatili wa kingono dhidi ya Watoto Henga amesema hivi karibuni kumekuwepo na taarifa za matukio ya Watoto wadogo kufanyiwa vitendo hivyo vya unyanyasaji wa kingono ikiwemo kibakwa na kulawitiwa.

 

Kwamba kwa mujibu wa taarifa ya haki za Binadamu ya LHRC ya mwaka 2021 matukio 11,499 ya ukatili dhidi ya Watoto yameripotiwa huku matukio ya kingono yakishamiri zaidi ambapo asilimia 89 ya matukio hayo yalikuwa yakingono na mikoa ya Dar es Salaam, Arusha, Tanga, Shinyanga, na Mwanza ikiibuka kinara wa matukio hayo.

 

No comments