Zinazobamba

BAADA YA GAZETI LA MAWIO,WINGU LATANDA GAZETI LA MWANANCHI,POLISI YAINGILIA KATI,SOMA HAPO KUJUA




Jeshi la Polisi jana liliwahoji Mhariri Mtendaji wa Mwananchi, Frank Sanga na mwandishi wa habari, Elias Msuya kuhusu makala iliyochapishwa juzi kuhusu utendaji wa jeshi hilo. 

Baada ya mahojiano yaliyofanyika kwa muda tofauti, waliachiwa kwa dhamana na kutakiwa kuripoti kituoni hapo leo asubuhi. 

Msuya ndiye aliyeanza kuhojiwa baada ya juzi jioni kupigiwa simu na maofisa wa polisi akitakiwa kufika Kituo Kikuu cha Polisi jijini Dar es Salaam kuhojiwa kutokana na makala yake ya uchambuzi yenye kichwa cha habari “Polisi na hofu ya watawala kuondoka madarakani.” 


Makala hayo yalichapishwa katika gazeti hilo toleo la Julai 13 na mwandishi huyo alieleza mambo mbalimbali yanayohusu utendaji wa jumla wa jeshi hilo kwa wananchi. 

Baada ya kutoa maelezo kwa saa mbili, maofisa hao walimpigia simu Sanga na kumtaka afike kituoni hapo kwa ajili ya kuhojiwa kuhusu makala hiyo. 

“Wamenihoji maswali mbalimbali kuhusiana na makala niliyoandika. Nimewajibu kulingana na jinsi walivyokuwa wakiniuliza,” alisema Msuya. 

Msuya alifika katika kituo hicho saa moja asubuhi na kukaa kwa saa mbili kabla ya kuanza kuhojiwa na kisha Sanga ambaye alifika kituoni hapo mchana na kuhojiwa kwa dakika 90. 

Akizungumzia suala hilo, Mhariri Mtendaji Mkuu wa Mwananchi Communications Ltd (MCL), Bakari Machumu alisema baada ya wito huo wa polisi, kampuni imetoa ushirikiano wa kutosha kwa kuwaruhusu Sanga na Msuya kwenda kutoa maelezo polisi. 

Alisema ni vyema masuala yanayohusu habari ambazo zinatakiwa kutolewa ufafanuzi yakaihusisha Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo na Baraza la Habari Tanzania (MCT). 

“Nadhani jambo kama hili kuchukuliwa moja kwa moja na polisi ni kama kuingilia uhuru wa habari. Vipo vyombo vinavyoweza kutoa ufafanuzi wa habari iliyoripotiwa na vyombo vya habari,” alisema Machumu. 

Baada ya mahojiano hayo, Sanga na Msuya waliachiwa kwa kila mmoja kudhaminiwa na mtu mmoja.