Zinazobamba

KAMANDA KOVA AJIPANGA KUPAMBANA NA WAHARIFU SIKU YA MKESHA WA MWAKA MPYA,SOMA HAPO KUJUA







JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA
WIZARA YA MAMBO YA NDANI
JESHI LA POLISI TANZANIA


28/12/2015
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

JESHI LA POLISI KANDA MAALUM LIMEJIPANGA UPYA KUHAKIKISHA USALAMA KATIKA MKESHA WA MWAKA MPYA BAADA YA SHEREHE ZA MAULID NA KRISMAS KUMALIZIKA SALAMA

Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limeweka mikakati ya hali ya juu kuhakikisha kwamba wakati wa mkesha wa Mwaka Mpya hali ya usalama inakuwa shwari. Katika mkakati huo vikosi vyote vya Polisi ikiwa ni pamoja na askari unifomu (GD), FFU, wanamaji, kikosi cha Mbwa na Farasi, askari kanzu, na wengine. Aidha, kikosi cha Polisi Anga kitafanya doria kwa kutumia helkopta ya Polisi. askari wa doria ya pikipiki watakuwepo barabarani wakifanya doria.
Pia tumekusudia kushirikisha wadau wengine wa ulinzi na usalama ikiwa ni pamoja na Jeshi la Zimamoto, kampuni binafsi za ulinzi, wadau wanaohusika na uokoaji wakati wa majanga,  vikundi vya ulinzi shirikishi pamoja na kamati za  ulinzi na usalama ngazi zote jijini Dar es Salaam. Aidha, wakaguzi wa Tarafa na askari  Kata watashiriki kikamilifu kuhakikisha maeneo yote yanalindwa masaa 24.
Sambamba na hatua hizo, vikosi vyote vya Polisi vitakuwa barabarani masaa sita kabla ya mwaka Mpya vikifanya doria.
Fukwe zote za bahari na maeneo yote yenye mikusanyiko yatalindwa kwa kuweka vituo vya polisi vya muda vinavyohamishika (Mobile Police Station). Pia askari wa kutosha watakuwepo kuhakikisha wananchi wanasherehekea kwa amani. 
Wakati wa mkesha huo nyumba zote za ibada zitalindwa hivyo wananchi wasiwe na hofu yoyote juu ya usalama wao kwa kuwa Jeshi la Polisi lipo imara. Hata hivyo wananchi wanatakiwa kuchukua tahadhari za kiusalama kwa kutoa taarifa kwa hali yoyote inayotia shaka.
Wananchi wanashauriwa kusherehekea siku ya Mwaka Mpya katika ngazi ya familia au kukusanyika katika mitaa kwa amani wakisherehekea.
Aidha, wafanyabiashara mbalimbali hasa wa maduka ya kubadilishia fedha (Bureau De Change), na wale wenye maduka makubwa wanatakiwa kuchukua tahadhari kwa kutosafirisha pesa nyingi kwa njia za kawaida. Wanashauriwa kusafirisha pesa hizo kwa njia za kietroniki na nyingine kama hizo. Pia wanashauriwa kuomba ulinzi wa Polisi kama kuna ulazima wa kufanya hivyo ili kuepuka kuvamiwa na watu wenye nia mbaya.
Madereva wanatakiwa kuzingatia sheria za usalama barabarani ikiwa ni pamoja na kutoendesha vyombo vya moto kwa mwendo kasi, na kutokuwa walevi.
Wananchi wanapoona dalili zozote au maandalizi ya uvunjifu wa amani watoe taarifa haraka na mapema iwezekanavyo katika vituo vya Polisi vya karibu ili hatua zichukuliwe kwa haraka.
Watu wajiepushe ma ulevi wa kupindukia au kupiga risasi za moto kama sehemu ya sherehe hiyo.
Upigaji wa fataki na flash flash haziruhusiwi katika usiku wa mkesha wa Mwaka Mpya.
Atakayekaidi atakachukuliwa hatua pao kwa papo kutokana na mtandao madhubuti wa vyombo vya usalama ikiwa ni pamoja na askari makachero watakaokuwa doria kila mahali.


TATHMINI YA UHALIFU WAKATI WA SIKUKUU YA MAULID NA KRISMAS

Kwa ujumla hali ya ulinzi na usalama katika jiji la Dar es Salaam wakati wa sikukuu za Maulid na Krismas ilikuwa shwari. Hapakuwa na matukio makubwa ya uhalifu katika siku hizo mbili licha ya makosa madogo yaliyoripotiwa kati ya tarehe 25/12/2015 hadi 27/12/2015.

Aidha, Jeshi la Polisi limefanikiwa kukamata Bastola moja aina ya RIVOLVER yenye namba 801340 rangi nyeusi iliyotengenezwa nchini Brazil ikiwa na risasi mbili. Tukio hili limetokea tarehe 24/12/2015 maeneo ya Ubungo Kibo wakati askari wa upelelezi wakiwa wanafuatilia matukio ya uhalifu waliwatilia shaka watu watatu na kuwafuatilia kisha kuwakamata.

Baada ya mahojiano walikiri kumiliki bastola hiyo ambayo ilikuwa imefichwa dukani kwa PETER S/O MASSAWE, Miaka 25, mkazi wa Rombo Kibo jijini Dar es Salaam. Wengine waliokamatwa ni kama ifuatavyo:
·          MATOLA S/O RASHIDI @ Carlos, Miaka 30, Mkazi wa Kimara Baruti
·        ISMAIL S/O OMAR, Miaka 29, Mkazi wa Kimara Baruti

Jumla ya watuhumiwa 71 wamekamatwa kwa tuhuma za makosa mbalimbali yakiwemo ya kubugudhi abiria, kupika na kuuza pombe haramu ya moshi (gongo), kuuza na kuvuta bhangi, kupiga debe, na makosa mengine. Aidha umekamatwa mtambo mmoja wa kutengeneza gongo, kete 236 na misokoto 174 za bhangi pamoja na lita 50 za gongo.

Tunawaomba wananchi waendelee kulisaidia Jeshi la Polisi katika kukabiliana na uhalifu katika jiji la hasa tunapouaga mwaka 2015 na kuukaribisha mwaka 2016




SULEIMAN H. KOVA – CP
KAMISHNA WA POLISI KANDA MAALUM
DAR ES SALAAM.

Hakuna maoni