MHA. MRAMBA NA BENKI YA DUNIA WAJADILI UIMARISHAJI WA GRIDI YA TAIFA
Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati anayeshughulikia Umeme na Nishati Jadidifu, Mha. Felchesmi Mramba, amekutana na wawakilishi wa Benki ya Dunia (WB) kujadili matokeo ya utafiti uliofanyika chini ya ufadhili wa benki hiyo ukilenga kuimarisha mfumo wa Gridi ya Taifa nchini.
Utafiti huo umebainisha maeneo muhimu ya utekelezaji yatakayosaidia kuimarisha Gridi ya Taifa ili kuhakikisha mfumo wa umeme nchini unakidhi mahitaji ya sasa na ya baadaye.
Akizungumza katika kikao hicho, Mha. Mramba ameishukuru Benki ya Dunia kwa kuendelea kuunga mkono maendeleo ya sekta ya nishati nchini kupitia ufadhili na usimamizi wa tafiti mbalimbali zenye lengo la kuboresha miundombinu ya umeme na kuongeza ufanisi wa huduma kwa wananchi.
Amesisitiza kuwa Serikali itaendelea kuweka mkazo katika utekelezaji wa mapendekezo yaliyotolewa kwenye ripoti hiyo ili kusaidia mipango ya uwekezaji, kuboresha uendeshaji wa mfumo wa umeme, kuendeleza usasa wa Gridi ya Taifa na kuongeza uimara wa huduma za umeme nchini.
Katika kikao hicho ilielezwa kuwa miongoni mwa mafanikio yatakayotokana na utafiti huo ni kuimarishwa kwa uwezo wa wataalam wa Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) kupitia mafunzo ya vitendo, warsha za kitaalam na ushiriki wa moja kwa moja katika tafiti za kisasa zinazohusu mifumo ya umeme.
Mkutano huo umehudhuriwa na viongozi na wataalam kutoka Wizara ya Nishati, TANESCO pamoja na kampuni ya ushauri ya GOPA Tech.

No comments
Post a Comment