Na Mussa Augustine.
Mfuko wa Bima wa Taifa
wa NHIF imefanya maboresho ya kitita Cha Mafao kwa Wanachama wake ambayo utekelezaji
wake utaanza rasmi Machi 1, 2024 ikwa lengo ni upatikanaji wa huduma Bora wa
Wanachama pamoja na kuongeza huduma ambazo hazikuepo hapo awali.
Hayo yamesemwa leo
Februari 28,2024 jijini Dar es salaam na Mkurugenzi Mkuu wa NHIF Dkt, Benard Konga wakati
akizungumza na waandishi wa habari,ambapo amesema kuwa maboresho ya mwisho ya
kitita Cha Mafao ya Mfuko huo kinachotumika kwasasa yalifanyika Mwezi June, 2016
na hivyo upo umuhimu wa kufanya marejeo yake kutokana na sababu mbalimbali.
Aidha Dkt Konga,
ameendelea kubainisha kuwa Maboresho
hayo ya Orodha ya huduma za Matibabu ambazo zinatolewa kwa wanufaika wa NHIF na
bei zake ambazo hutumika wakati wa malipo kwa madai ya watoa huduma za Matibabu
yamezingatia Maendeleo ya teknolojia na hali halisi ya bei katika soko ,pia
kuwianisha kitita cha Mafao na Miongozo ya tiba iliyoboreshwa ili kuongeza
ubora wa huduma zinazotolewa kwa wanufaika wa Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya.
Mkurugenzi Mkuu huyo
wa NHIF kupitia taarifa yake kwa Vyombo vya habari amefafanua kuwa maeneo
yaliofanyiwa Mapitio na Maboresho ya kitita cha Mafao ni pamoja na ada ya
usajili na kupata ushauri wa daktari,Huduma za dawa, vipimo,upasuaji na gharama
za kliniki za kawaida na kibingwa .
“Jumla ya dawa 736
zimefanyiwa mapitio kwa kuzingatia bei ya soko na gharama za uendeshaji na
wastani wa faida ,hii itaondoa changamoto ya wananchi kukosa baadhi ya huduma
za dawa kutokana na changamoto ya bei,pia tumeongeza dawa mpya zipatazo 247
ambazo zinatokana na dawa mpya zilizopo kwenye muongozo wa orodha ya dawa muhimu
za Taifa (NEMLIT)”amesisitiza Dkt Konga.
Nakuongeza kuwa “Gharama za vipimo 311 na upasuaji zimefanyiwa
mapitio kwa kuzingatia bei za soko katika ununuzi wa vifaa na vitendanishi
,gharama za uendeshaji na wastani wa faida hii itaondoa changamoto ya
kukosekana kwa huduma za vipimo na
upasuaji kutokana na changamoto ya bei”.
Hata hivyo, Mkurugenzi
Mkuu huyo amewaomba wananchi kuendelea kujiunga na NHIF ili kuwawezesha kupata
huduma za matibabu kupitia Mfuko huo kwani lengo la Serikali ni kuanza kutoa huduma
za Afya kuanzia ngazi ya zahanati, hadi hospital ngazi ya Taifa,nakwamba Mpango
wa huduma ya afya kwa wote unatarajiwa kuanza hivi karibuni.
Kwa mujibu wa Dkt.Konga
NHIF itaendelea kupokea maoni kutoka kwa
wadau na itaendelea kuwajulisha pindi maboresho yoyote yatakapotokea ili kuwa
na ufanisi katika utoaji wa huduma kwa wananchi.
Hakuna maoni
Chapisha Maoni