Zinazobamba

TEA: Mradi wa kuendeleza ujuzi umekamilika kwa mafanikio, vijana 49,000 wamenufaika

 

Kaimu Mkurugenzi Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi Masozi Nyirenda akitoa elimu kwa wadau waliotembelea banda la TEA wakati wa maonesho ya miaka 50 ya Baraza la Mitihani la Tanzania yaliyofanyika Jijini Dar es Salaam viwanja vya Mnazi Mmoja.



Na Mwandishi wetu-Dar es salaam

Kaimu Mkurugenzi wa Utafutaji Rasilimali na Usimamizi wa Miradi Masozi Nyirenda amesema serikali kupitia Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) imefanikiwa kukamilisha mradi wa kuendeleza ujuzi kwa mafanikio makubwa ambapo jumla ya vijana 49,000 wamenufaika kwa kupata ujuzi.

Mh. Nyirenda amesema hayo Novemba 3, 2023 wakati akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea Banda la TEA wakati wa maonyesho ya miaka 50 ya Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), yaliyofanyika katika uwanja wa Mnazi mmoja Jijini Dar es salaam



“Mwaka 2017 TEA ilikabidhiwa jukumu la ziada na Wizara ya Elimu sayansi na teknolojia kusimamia mfuko wa kuendeleza ujuzi, huu ni mfuko ambao kazi yake ni kufadhili taasisi zinazotoa mafunzo ya ujuzi pamoja na vijana ambao wanataka kupata mafunzo hayo, mwishoni mwa mwezi Juni tulikamisha mradi ambapo vijana elfu 49 walinufaika,” alisema

Vilevile, amesema katika ufuatiliaji walioufanya kwa lengo la kubaini vijana hao wameishia wapi baada ya kupata ujuzi, wamebaini asilimia 80 wapo kazini, aidha kwa kuajiliwa au kujiajili.

Akieleza kwa nini wameshiriki katika maonesho ya baraza la mitihani Tanzania, Masozi amesema wao ni wadau wakubwa wa elimu na hivyo ni muhimu wakakutana na wananchi na kutoa elimu juu ya kazi wanazozifanya

“Wenzetu NECTA wanatathimini ubora wa elimu, sisi tunafadhili vifaa na kuhakikisha mazingira ya ufundishaji yanakuwa bora, kwa hiyo tupo hapa kueleza fursa zinazopatikana,” alisema

Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa mstari wa mbele katika kutekeleza, na kusimamia Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) ikiwemo kusimamia upatikanaji wa elimu bora na kwa usawa kote nchini pamoja na uboreshaji wa miundombinu ya kujifunzia na kufundishia.

Katika kufanikisha utekelezaji wa malengo haya, Serikali imeendelea kufanya maboresho makubwa katika sekta ya Elimu kuanzia elimu ya awali, msingi, sekondari hadi vyuo vikuu. Maboresho na mageuzi haya yanahitaji rasilimali na nguvu kazi kutoka kwa wadau mbalimbali ili kuunga mkono jitihada za Serikali za kuboresha sekta ya sekta ya Elimu.

 

Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA) inalo jukumu la kuhamasisha uchangiaji maendeleo ya Elimu kote nchini ambapo, kwa mujibu wa Sheria ya Mfuko wa Elimu, Namba 8 ya mwaka 2001 sehemu ya 12 (1) (a) na (b) mchangiaji ni mtu yeyote anayetoa mchango wa pesa, bidhaa, au huduma kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa au kutekeleza mradi kwa uratibu wa Mfuko huo wa Elimu

 

Hakuna maoni