Tumekwama wapi Ithibati ya bidhaa halali?
Binafsi napenda sana nyama, kama wanavyopenda Watanzania na
Waafrika au hata labda wanadamu wote, ukiacha wale waliojiharamishia.
Hata hivyo, ulaji wangu wa nyama umepungua sana, hasa nje ya
nyumbani. Hii ni kwa sababu ya kujiwekea masharti mengi kwa sababu ya mashaka
ya uhalali na usalama wa nyama zinazouzwa. Kwa mfano, sili kuku kwenye sehemu
za wauza chipsi na baadhi ya migahawa. Mashaka yangu si ya bure.
Upo ushahidi kuwa watu wengi siyo waaminifu katika mnyororo
mzima wa biashara ya nyama kuanzia wanakotolewa hadi kwa wauzaji wanaopeleka
bidhaa hiyo kwa mlaji (sehemu wanazouza vyakula). Kwenye nguzo zote nne za
uchinjaji halali yaani mnyama, vifaa, mchinjaji na taratibu za uchinjaji, kuna
ukakasi na wasiwasi mkubwa.
Kinachonipa mashaka zaidi ni ushahidi mbalimbali niliopata
kuuona na kuusikia kuhusu nyama tunazokula.
Mara kadhaa kwenye mitandao ya kijamii tumeona video za wanawake
wakiwanyonga kuku kwa mikono badala ya kuwachinja. Wengine wanachinjwa kwa ukatili
wa hali ya juu kwa visu butu, kisha wanaachwa wanapaparika.
Juzijuzi tu nilisikia tena huko Bagamoyo, maeneo ya Mapinga, Kerege na Kiaraka, ambako kuna ufugaji mkubwa wa kuku kuwa kuna utaratibu wa kukusanya vibudu na kuwauzia wanawake.
Wanawake hao, kila asubuhi kati ya saa 1 na 3 au jioni kuanzia
saa 12 hadi mbili usiku wamekuwa wakionekana wakienda na kurejea na ndoo
zilizojaa nyamafu (vitoweo mfu).
Rafiki yangu mmoja aishiye Kibaha aliwahi kunihadithia kuhusu
ng’ombe wanaofia njiani (kutoka huko wanakotolewa) na kushushwa Kibaha kisha
huchinjwa na kuingizwa sokoni. Siku moja alipoenda buchani, rafiki yake muuza
nyama akamwambia leo usinunue hii ni kibudu. Mara ngapi tunasikia watu
wamekamatwa kwa kuuza mishkaki ya nyama za wanyama wasioliwa kama mbwa na
kadhalika?
Katika mazingira haya, siyo tu tupo hatarini kula haramu, lakini
pia afya zetu pia ziko matatani kwa kula vitu vibaya, kinyume na maagizo ya
Mwenyezi Mungu aliyesema: “Enyi watu! Kuleni vilivyomo katika ardhi, halali na
vizuri, wala msifuate nyayo za Shetani. Hakika yeye ni adui yenu aliye
dhaahiri.” [Qur’an, 2:168]. Vilivyo halali bila shaka ndiyo vizuri pia.
Haihitaji sayansi ya roketi kujua kuwa viwango vya halali vya
Uislamu siyo tu suala la kiimani bali vinamhakikishia mwanadamu usalama wake
anapotumia bidhaa husika.
Imethibitika kisayansi mnyama asiyefaa kuliwa, au yule anayefaa
lakini mgonjwa au amechinjwa isivyotakiwa, anaweza kumsababishia mwanadamu
madhara na maradhi mbalimbali.
Ziko
wapi bidhaa halali?
Katika mazingira haya, tunajiuliza ziko wapi bidhaa za halali
ili tuweze kula vizuri kama Uislamu unavyotutaka? Jitihada kadhaa zimefanyika
katika kuanzisha kampuni za kutoa ithibati ya halali kuthibitisha ubora wa
huduma na bidhaa, ikiwemo nyama. Sasa hivi kuna kampuni ya MICO International
Halal Bureau (MIHB) ikibeba jukumu hilo na kutoa cheti.
Hata hivyo, licha ya uwepo wa kampuni hiyo, kuna changamoto
nyingi bado ikiwemo mwamko mdogo wa jamii unaopelekea uwepo wa watoa huduma
wachache waliothibitishwa. Na hata hao waliothibitishwa, hawajulikani kwa
walaji wengi wa kawaida.
Tathmini yangu ni kutoka katika mtazamo wa mlaji. Naishi
Mburahati lakini silijui duka lolote ambalo lina ithibati ya halali siyo tu
Mburahati bali pia maeneo ya jirani kama Manzese, Kigogo, Mabibo na hata
Magomeni. Sisemi hayapo bali siyajui kwa sababu taarifa hazifiki kwangu na
nikizitafuta sizipati. Huu ni udhaifu mkubwa katika maendeleo ya kuweka
ithibati ya halali ya bidhaa siyo tu nyama bali zote na huduma pia.
Ofisa mmoja wa MICO aliniambia kuna shida pia kwa watoa huduma
kutokuwa tayari kugharamia zoezi la kufanyiwa ithibati. Hii ni sahihi lakini
labda kampuni yenyewe ingejitahidi kuwepesisha gharama kwa kutafuta wafadhili.
Ithibati ya halali ni jambo la kiibada na isingefaa lifanyike
kwa madhumuni ya kibiashara zaidi. Tukishindwa kuweka na kuvisimamia hivi
viwango, tumeshindwa wote kama umma na madhara yanarudi kwa jamii nzima.
Natoa rai kwa kampuni kubwa za Waislamu ziingie kwenye biashara
ya bidhaa halali, hususan bidhaa za nyama ili Waislamu na jamii kwa ujumla
tununue na kula nyama kwa kujiamini.
Watu wangu wa nyumbani wanapenda sana soseji lakini kama hatujui
zinatoka wapi na zinatengenezwaje, na kama je, viwango vya halali vimefikiwa au
la, ni ngumu kununua tu na kula ovyo.
Masheikh nao tunawapa rai wajitahidi kuzungumzia umuhimu wa
kutumia bidhaa na huduma halali ili kuongeza uelewa na mwamko wa Waislamu.
Uimara wa ithibati ya halali utapatikana tu kama kuna watumiaji wa kutosha.
Tujifunze
kwa wengine
Waislamu wa Tanzania tunaishi kwa mazoea sana. Wenzetu katika
mataifa mengine wanachukulia masuala haya kwa umakini mkubwa na ndiyo maana
kumekuwa na vikwazo katika upelekaji bidhaa, hususan za nyama, katika nchi za
Kiislamu.
Ajabu ni kuwa sisi wenyewe, licha ya ushahidi mwingi wa
kukosekana uadilifu katika mnyororo mzima wa thamani katika uandaaji bidhaa za
nyama, bado tunadhani bidhaa tunayoikuta buchani, hotelini, migahawani ni safi
na imekidhi vigezo huku tukijificha kwenye kigezo kuwa kwa kuwa hatujui, haina
tatizo.
Binafsi, hatari ninayoiona katika bidhaa za nyama Tanzania
naifananisha na hali ya China, ambako niliishi kwa mwaka mmoja. Kule mara mbili
nilikula nguruwe, bila kujua.
Siku nilipofika katika mgahawa wa chuo, nikaagiza wali na samaki
lakini kumbe waliweka nyama ya kusaga ya nguruwe. Siku nyingine nikatoka na
rafiki aliyekuwa akinifundisha kichina nikaagiza tambi na yai. Nilipoanza kula,
nilipozamisha vile vijiti vyao (chopstick) kwenye bakuli nikaibua pande la
nyama.
Mazingira tofauti lakini hatari ni ileile. Jiulize mwenzangu
unayejisosomola makuku kwenye vibanda vya chipsi, mara ngapi umekula wale kuku
vibudu au nyama kibudu aliyefia njiani na kushushwa pale Kibaha au wale
waliochinjwa baada ya kuuawa kwa kwa maji ya moto, wanaofugwa kwenye vitongoji
mbalimbali vya hapa Dar es Salaam?
Tuchukue tahadhari kama umma kwa kuunga mkono ithibati ya bidhaa
za halali.
Hakuna maoni
Chapisha Maoni