Zinazobamba

KC Mabwepande yawaunganisha wananchi na viongozi wao kujadili changamoto za kata hiyo kwa pamoja

Picha ya Viongozi wa Serikali za Mitaa mbalimbali na Kata Mabwepande wakiwa katika picha ya Pamoja baada ya Mdahalo.

Na Vicent Macha DSM.

Kituo cha Taarifa na Maarifa Kata ya Mabwepande Kimewakutanisha wananchi, Pamoja na viongozi mbalimbali wa Mitaa na Kata ya Mabwepande, lengo likiwa ni kutoa mrejesho wa changamoto walizoziibua na namna ya kuzitafutia ufumbuzi baada ya kupewa elimu hiyo na TGNP mwezi Machi mwaka jana.

Akiwasilisha changamoto hizo kwa viongozi hao Mwenyekiti wa Kituo hicho Bi. Fatuma Ramadhani Nurru amesema kuwa Kata hiyo imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya Maji Safi na salama kwa baadhi ya maeneo, Barabara, Elimu, Masoko ya kufanyia Biashara Pamoja na Ukatili wa kijinsia.

Akiongelea changamoto ya Ukatili wa Kijinsia amesema kuwa wao kama Kituo wamekuwa wakipokea kesi mbalimbali za wanawake kupigwa na wanaume zao, lakini pia Watoto kufanyiana vitendo vya ubakaji na kulawitiana wenyewe kwa wenyewe.

Ameongeza kuwa kumekuwa na baadhi ya changamoto kwenye kufikia Elimu kwani kwa upande wa Bunju “B” hakuna Shule ya Msingi hivyo inawalazimu Watoto kuvuka Barabara kuu ya Bagamoyo na kwenda upande wa pili kufuata shule hali inayochangia Watoto kugongwa na magari mara kwa mara.

Na mwisho amewataka viongozi na wananchi kuweza kushirikiana ili kuleta maendeleo katika kata hiyo kwani maendeleo hayawezi kuletwa na viongozi peke yake bali ni kwa ushirikano wa makundi yote mawili wananchi na viongozi wao.

Mdahalo Ukiondelea.

Kwa upande wake Diwani wa Kata hiyo Mh. Muhajirina Kasimu Obama amesema kuwa kwa upande wa Mabwepande wako vizuri kwani mahitaji mengi ya msingi wanayo, akizungumzia upatikanaji wa Maji amesema kuwa huduma hiyo imeweza kufika katika Mitaa yote minne na kwasasa zoezi hilo lipo katika Mtaa wa Mbopo na linakwenda vizuri kabisa.

Ameongeza kuwa kwa upande wa Elimu pia wako vizuri kwani kata zote Nne zimebahatika kupata Shule za msingi na sekondari, na kutoa ufafanuzi kuwa kwa changamoto ya Watoto wa Bunju “B” Serikali inalitambua hilo hivyo muda si mrefu wataweza kupata Shule na kuondokana na hadha ya kuvuka barabara kubwa ya Bagamoyo kufuata masomo.

Diwani huyo ameendelea kusisitiza kuwa Kata ya Mabwepande ni kata kubwa sana hivyo wanafunzi ulazimika kutembea kilometa 2 mpaka 5 kufuata masomo hivyo wao wakabuni mbinu nzuri ya kuhakikisha Watoto watakaomaliza elimu ya msingi katika shule moja wanahakikisha wanampanga katika shule ya karibu na Mtaa wake ili kupunguza umbali mrefu wa kufuata shule ilipo.

Aidha Diwani huyo amemaliza kwa kusema kuwa changamoto ya barabara ameshaiwasilisha Halmashauri na inaendelea kufanyiwa kazi  kwani barabara nyingi za kata hiyo ni za Changarawe na hazijafanyiwa marekebisho kwa muda mrefu hali inyofanya kutopitika kwa urahisi hali inayosababisha kukosekana kwa Daladala zenye ruti ya Mabwepande, na kuongeza kuwa changamoto hiyo inawafanya wakazi na wanafunzi kuzunguka sana wakati kuna njia nyepesi ambayo ingeunganishwa na daladala.

Baadhi ya washiriki wakiwa katika kazi za vikundi.

Nae Mwenyekiti wa Mtaa wa Mji mpya Mohamed Bafta amesema kuwa kilio cha Wananchi kilikuwa ni soko hivyo serikali ikaamua kuwajengea soko changamoto iliyokuja kutokea wafanyabiashara wengi wamejenga vibanda na badala yake hawavitumii hali iliyofanya kudhoofika kwa soko hilo, na matokeo yake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kinondoni ametoa maagizo ya kuwa wote wasiyovitumia vibanda hivyo waviondoe mara moja.

Kwa upande wake Mtafiti wa Elimu Wilaya ya Kinondoni ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Elimu Kata ya Mabwepande Dkt. Bill Abraham amsemea kuwa sababu kubwa inayosababisha elimu kushuka katika kata hiyo ni kwamba walimu wengi wanaokuja katika kata hiyo wanakuwa wamekuja kutumikia adhabu na siyo kutekeleza wajibu wao.

Akitoa ufafanuzi huo amesema kuwa walimu wamekuwa wakiambiwa na wakubwa wao wa kazi kwa kuwa umefanya kosa hili adhabu yako nakupeleka Mabwepande hivyo na wao wanaona ni kama sehemu ya kutekeleza adhabu kutoka kwa wakubwa wa kazi na siyo kutoa elimu bora.

Ameongeza kuwa wakazi wa kata hiyo pia hawakuipa elimu kipaumbele kwani linapokuja suala muhimu la shule wazazi ulipuuzia kwa mfano kuhusu suala la masomo ya ziada kwa wanafunzi au suala la chakula hivyo husababisha Watoto kusinzia Darasani na kutofanya vizuri katika masomo yao.

Hakuna maoni