Zinazobamba

WAZIRI MKUU AMLILIA SAMWEL SITTA KITOFAUTI,SOMA HAPO KUJUA

SERIKALI imekiri kwamba pengo la Spika mstaafu, Samuel Sitta ni kubwa na kamwe halitazibika ndani ya serikali, chama na jamii.
Kauli hiyo ilitolewa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati akitoa salamu za Rais John Magufuli na Makamu wake, Samia Suluhu Hassan kwenye maziko ya Spika huyo yaliyofanyika kitongoji cha Mwenge, Urambo mkoani Tabora jana.

Waziri Mkuu Majaliwa alisema kama serikali wamepata pigo kwa kumpoteza mtu muhimu serikalini. Majaliwa alisema, kuondokewa na mzee Sitta ni pengo kubwa na kamwe halitazibika ndani ya serikali, chama na jamii kwa ujumla kutokana na mchango wake wakati wa uhai wake.
Pamoja na kutoa pole kwa familia, aliisihi wao pamoja na wana Urambo kwa ujumla kuupokea msiba huo kwa mikono miwili, licha ya ukweli kuwa kifo siku zote huwa hakizoeleki.
Akifafanua zaidi jinsi taifa lilivyonufaika Waziri mkuu huyo alisema, Sitta akiwa mtumishi wa serikali atakumbukwa kwa mazuri yake kwani alikuwa mtumishi aliyetukuka, mpenda amani, msikivu na aliyependa kushirikiana na jamii.
Alisema uongozi wake ulikuwa mfano wa kuigwa na viongozi na jamii kwa ujumla na kwamba kila kazi ambayo alipewa hakusita kuipokea na wala hakuwahi kuishindwa.
Majaliwa alisema binafsi asiwe mchoyo wa fadhila, kwani alimfundisha kazi kipindi ambacho yeye alikuwa mkuu wa wilaya ya Urambo na Sitta akiwa mbunge wa jimbo la Urambo na Spika wa Bunge la Tisa.
“Mara kadhaa alikuwa akikaa nami pale juu ghorofani nyakati za usiku saa mbili na kunifundisha kazi…..lakini alinionya kuwa nisipende kujihusisha na migogoro ya watu na alinitaka kupenda kazi kamwe nisiwe mvivu,” alisema.