Zinazobamba

SAMWEL SITTA ATANGAZA VITA NA MAASKOFU NCHINI,WENYEWE WASEMA ATAKUWA ANAMPUUZA MUNGU,SOMA HAPA KUJUA ZAIDI

Samuel Sitta
Pichani ni Mwenyekiti wa Bunge la Katiba Samwel Sitta picha na Maktbaba
MWENYEKITI  wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta, amejiweka katika wakati mgumu kwa kuzua mgogoro mpya dhidi ya viongozi wa dini ya Kikristo, baada ya kuita waraka wao kuwa ni wa kipuuzi na wa hovyo hovyo.
          Huku yeye akisema kuwa waraka wao una lugha ya UKAWA, wao wamesisitiza kwamba ni waraka wa kinabii, kwa ajili ya maslahi mapana ya nchi.
            Wakati yeye akikemea waraka wao, maaskofu wamesema ile ilikuwa sauti kutoka mbinguni, na kwamba anapambana na Mungu.
            Wakati yeye akisema waraka wao haukuwa na utukufu wowote, wao wamemfananisha yeye na Goliati wa kwenye Biblia aliyeshindwa na Daudi kwa sababu ya jeuri na matusi kwa Mungu. Wamesisitiza kwamba kwa sababu ya jeuri yake, wataanzia pale atakapoishia baada ya Bunge Maalumu la Katiba.

         Juzi na jana asubuhi, Sitta alitoa maneno ya kejeli dhidi ya viongozi wa Kikristo, hasa Jukwaa la Wakristo,  ambao walitoa waraka kuonyesha kutoridhishwa kwao na mwenendo wa Bunge Maalumu la Katiba.
        Sitta alitoa kauli hiyo bungeni alipokuwa akielezea mwenendo wa upigaji kura za kupitisha ibara na sura za rasimu ya katiba inayopendekezwa, akisema amekuwa akituhumiwa kwenye mitandao kwamba anadharau maaskofu.
Kauli ya Sitta
“Nimalizie na viongozi wangu wa kiroho…mababa zangu maaskofu, natuhumiwa sana kwenye mablog kwamba nadharau maaskofu. Wakiwa na matendo kama hayo hao baadhi ya maaskofu itabidi tuendelee kuwadharau.
      “Ninao waraka huu ambao umelazimishwa kutumwa katika makanisa. Sioni utukufu wa Ukristo katika waraka huo. Huu waraka unamwamuru Rais airudishe Tume ya Mabadiliko ya Katiba. Kuna Ukristo hapa? Waraka huu unamlazimisha Rais asitishe mchakato wa Bunge Maalum…tangu lini watu wa kiroho wanatoa maagizo ya kisiasa? Hii sio haki hata kidogo…kuna Ukristo hapa? Waraka una lugha za wale UKAWA tuliowazoea.
       “Hivi kweli maaskofu wa Kikristo wanaweza kusema kwamba Wizara ya Katiba na Sheria irudishe tovuti ya Tume ya Jaji Warioba na kuirejeshea nyaraka zake zote ili wananchi wasome na kujifunza?
        “Kwamba maoni ya wananchi hayawezi kufutwa na kudharauriwa na chama tawala, hivyo basi Bunge la Katiba lijadili na kuboresha tu rasimu ya katiba na si kubadilisha?
       “Waraka huu kwa shinikizo la maaskofu umesambazwa kwenye makanisa na kusomwa. Mimi nasema kama Mkristo, tukianza kuruhusu nchi yetu kutoa nyaraka hizi za kisiasa zisomwe makanisani kwa kudai huo ni msimamo wa maaskofu, basi nchi hii tutaipeleka kubaya.
         “Na mini kama mtu mzima lazima nionye kuhusu tabia hii, ukizingatia nchi hii haina dini, hawa baadhi ya maaskofu ambao walikusanywa Dar es Salaam na makundi yale yale yanayohusishwa na UKAWA, kama wao ni wanachama wa siri wa vyama vya siasa vinavyochukia CCM wajitokeze wazi
wazi,” alisema.
          “Na kuna askofu mmoja ameapa kabisa kwamba atawaelimisha waumini wake ili siku za usoni wawashughulikie viongozi kama mimi. Nasema aendelee
lakini Mungu anaona yote yaliyo moyoni mwetu.”
Maaskofu nao wanena
    Chanzo hicho ilizungumza na maaskofu kadhaa kutoka CCT, wakasema wamekerwa na kebehi na dharau za Sitta.
          Askofu wa Kanisa la Kiinjili na Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Karagwe, Dk. Benson Bagonza, alisema waraka wa maaskofu ni nguvu kutoka mbinguni, si kukurupuka.
      “Nimemsikia Sitta akitushambulia. Sasa natumia hekima kumjibu kwamba maandiko matakatifu katika Biblia; 1Samweli 17:31-37, hasa mstari wa 36, yanasema Goliati alipogombana na kijana mdogo Daudi. Ushindi wake ulitokana na Goliata kumtukana Mungu wa Daudi.
        “Na ukiona Goliati anaanza kumtukana Mungu, ujue ushindi wa Daudi umekaribia. Hivyo ndivyo Sitta sasa anavyokebei na kutukana viongozi wa dini. Hapo tunakumbushwa na maneno ya Mungu yanayosema, ‘awakatae nyinyi niliowatuma, amenikataa mimi.’  Tazama Luka 10: 16, ” alisema Askofu Bagonza na kuongeza:
           “Na katika kauli zake hizo amekuwa akisema kuwa waraka wetu unafanana na msimamo wa UKAWA … sasa kama katupeleka huko nasi tutaeleeke huko huko, tusije kulaumiana tu, mbele ya safari.
       “Nilikuwa mmoja wa wanakamati walioandika waraka huo. Wakati wenzangu wanautoa mbele ya umma, nilikuwa kwenye msiba mzito wa Askofu Mkuu Mstaafu Mukuta, lakini nataka nimwambie hivi mtetezi wetu yu hai, na wala hatuwezi kujitetea mbele yake (Sitta).”
        Askofu wa Jimbo la Katoliki la Bunda, Mhashamu Renatus Nkwande, alisema matamshi ya Sitta yanaonyesha anavyohangaika kualalisha kilicho haramu.
             Alisema kitendo cha Sitta kuendesha BMK kwa kukejeli wajumbe wenzake walioondoka bungeni (UKAWA) na wajumbe walioandaa rasimu ya pili kwenye Tume ya Katiba Mpya chini ya Jaji Joseph Warioba, ni jambo la aibu ambalo halivumiliki, na ndiyo maana walitoa waraka wa kutokubaliana nacho.
         “Kwa kweli Sitta ametutukana, ametafuta ubaya kwa viongozi wa dini, kwa kuwa tumesema ukweli ? Sisi tulikuwa tunatimiza wajibu wetu kwa Wakristo …tulizungumza kutokana na hitaji la wakati, na ulikuwa waraka wa unabii,” alisema.
        Askofu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini, Dk. Steven Munga, alisema hawatajibizana na Sitta, bali wataanzia pale alipoishia.
           “Ukibishana na mjinga utakuwa mjinga pia. Tunasubiri wamalizie kazi iliyowapeleka huko kula fedha ya wananchi. Sisi viongozi wa dini tuna watu wengi zaidi,” alisisitiza.
       Baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa na kijamii waliliambia gazeti hili kuwa jeuri ya Sitta imemfanya atangaze vita tatu kwa mpigo.
           “Kwanza, ametangaza vita na viongozi wa dini ya Kikristo. Pili ametangaza vita ya CCM na viongozi hao, iwapo CCM haitamkemea hadharani. Tatu, ametangaza vita na imani yake mwenyewe,” alisema mchambuzi mmoja.

           Mzozo huu mpya wa Sitta na viongozi wa dini unaweza kumweka njia panda, hasa kwa kuwa amekuwa anatumia makanisa hayo hayo kujipigia debe na kushambulia wanasiasa wenzaka anaopambana nao kusaka urais
Chanzo ni Gazeti makini la Tanzania Daima

Hakuna maoni