Msimamizi Mkuu wa Chaneli ya Sinema Zetu Sophia Mgaza akizungumza katika utambulisho wa tamthilia mbili mpya za Mawio na Koneksheni jijini Dar es Salaam.

Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Azam Media LTD kupitia Chaneli 103 ya Sinema Zetu imetambulisha tamthilia mbili mpya Mawio na Koneksheni ambazo zitaanza kuonekana hivi karibuni.

Akizungumza leo Mei 2, 2024 jijini Dra es Salaam kwenye hafla ya kutambulisha tamthilia hizo, Msimamizi Mkuu wa Chaneli ya Sinema Zetu Sophia Mgaza, amesema kuwa tamthilia ya Mawio itakuwa na wasanii maarufu kutoka Zanzibar ambao hawajawahi kuonekana katika kazi za filamu nchini.

"Hapa mila, tamaduni na mifumo ya maisha ya kisasa ya Wazanzibar yanatazamwa kwa kina na kwa namna ya kukuacha ukifurahi nyakati zote," amesema Mgaza na kuongeza,

"Pamoja na zawadi hii kutoka Zanzibar, ingizo jingine jipya ni la burudani katika msimu huu wa Promosheni  ya Sibanduki Ng'o ni tamthilia ya Koneksheni. Hakuna shaka harakati za mjini zinahitaji koneksheni wakati mwingine ili utoboe,".

Kwamba sura nyingi mpya katika ulingo wa tamthilia nchini umekaa pamoja na kushusha kitu cha kipekee 'koneksheni'.

Mgaza amebainisha kuwa kupitia Channeli 103 ya Sinema Zetu, tamthilia ya Mawio itaanza kuonyeshwa Juni 7, 2024 (Ijumaa hadi Jumapili), huku Koneksheni ikianza kuonyeshwa Mei 6, 2024 (Jumatatu hadi Alhamisi).