WAZIRI NCHEMBA KUWA MGENI RASMI SIKU YA VIJANA.DK MARWA AWATAKA VIJANA KUJITOKEZA,SOMA HAPO KUJUA
![]() |
| Pichani ni Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba(picha na Maktaba) |
NA KAROLI VINSENT
WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mwigulu Nchemba
anatarajiwa kuwa Mgeni rasmi katika siku ya vijana inayofanyika leo katika
viwanja vya Zakhiem Mbagala jijini Dar es Salaam.
Hayo yamesemwa leo Dar es Salaam na Ofisa Miradi wa
Shirika la umoja wa mataifa la idadi ya watu Duniani, Daktari Majaliwa Marwa
alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari kuhusu siku hiyo iliyopangwa
kuwakutanisha vijana zaidi ya 1000 kutoka maeneo mbali mbali.
Amesema Vijana wanapaswa kujitokeza kwa wingi katika
siku hiyo kwa kuwa Shirika hilo kwa kushirikiana na Serikali pamoja na wadau
mbali mbali wamepanga kutoa elimu kwa vijana ya kuweza kujitambua na kuacha
masuala ya kuwa tegemezi.
"Katika siku ya Kesho tumepanga kufanya mambo
mbali mbali ikiwemo yale ya ujasiriamali pamoja na kujenga uelewa wa masuala ya
afya kwa vijana ili tuweze kujenga taifa ambalo litakuwa na watu wenye afya bora
pamoja na wenye kipato," amesema Dkt.Marwa.
Dkt. Marwa ameongeza kuwa Vijana wanapaswa kufuata
kauli mbiu ya Mwaka huu isemayo 'Kijana, Sepesha Umaskini Ongeza uzalishaji kwa
maendeleo endelevu' ili kuweza kufanya maliasili zilizopo katika nchi hii
ziweze kusaidia vizazi vya mbeleni.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Afya ya Uzazi wa
Shirika la PSI Tanzania,Pludence Masaku amesema kuwa kwa hivi sasa nchini
kumekuwa na ongezeko kubwa la vijana kupata ujauzito kabla ya kujiandaa hivyo
vijana wanapaswa kujitokeza kwa wingi ili kuweza kupata elimu itakayowawezesha
kuweka mpangilio wa Familia zao.
Alisema kuwa Shirika hilo litatoa huduma za afya
katika maadhimisho hayo pamoja na kutoa semina kwa vijana itakayoweza
kuwasaidia katika kuendesha maisha yao pamoja na kusaidia kukuza ustawi wa
jamii.
"Ili taifa liweze kupata maendeleo ni lazima
watu wajiandae kila idara ikiwemo ile ya afya, hivyo siku ya kesho sisi
tutaitumia kwaajili ya kutoa semina na elimu mbali mbali kwa vijana ili waweze
kupanga wakati ambao wanataka kupata watoto na sio kuzaa holela holela na
kupeleka kushindwa kuwalea watoto wao," alisema Masaku.
...Mwisho...
