Zinazobamba

TGNP WATAJA SABABU ZA WANAWAKE KUSHINDWA KUCHOMOZA KATIKA MEDANI ZA KISIASA



 Imeelezwa kuwa chanzo kikubwa cha Taifa la Tanzania kushindwa kuwa na wanawake wengi katika nyanja mbalimbali za uongozi ni kukithiri kwa vitendo vya rushwa, hususani rushwa ya ngono pamoja na umasikini unaowazunguka.
Hayo yamebainika katika kongamano maalum lilolenga kuwajengea uwezo Wanawake ili waweze kupambana na changamoto zinakwamisha jitihada za wanawake kuchomoza katika nafasi mbalimbali za Uongozi hapa nchini.
Katika Kongamano hilo lililohudhuriwa na aliyekuwa Spika mstaafu ya Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mama ANNA MAKINDA, Wanawake walibainisha vikwazo mbalimbali wanavyokumbana navyo wakati wa kusaka nafasi za uongozi, lakini kubwa wakisisitiza juu ya suala la umasikini na Rushwa ya Ngono.
Kwa muda mrefu wanaharakati wa haki za wanawake na wadau mbalimbali wameendelea kupambana kuhakikisha kuwa wanawake wanapata nafasi sawa katika Nyanja mbalimbali ikiwemo ya uongozi lakini jitihada hizo zinaonekana kukwamishwa na Umasikini.

Kongamano hilo Liliandaliwa na Mtandao wa Jinsia Tanzania TGNP kwa kushirikiana na ACTIONAID mahususi kwa ajili ya kuwajengea uwezo wanawake hao kupambana katika nafasi mbali mbali za uongozi nchini.


Mgeni Rasmi katika shughuli hiyo Spika mstaafu Mama Anna Makinda akiwa katika Picha ya pamoja na viongozi mbalimbali wa kisiasa  wanawake 
Wakisoma tamko mbele ya Mgeni Rasmi ANNA MAKINDA wanawake hao wameeleza kuwa uwezo mdogo wa kiuchumi miongoni mwa wanawake walio wengi umekuwa kikwazo kikubwa sana katika harakati zao kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika chaguzi za nchi na kujikuta wakishindwa kushiriki kwa ukamilifu zoezi la uchaguzi jambo ambalo linazidi kuwapa nafasi wanaume kutawala katika nafasi mbalimbali za uongozi nchini.

Aidha wameeleza kuwa kwa uzoefu walioupitia katika uchaguzi wa mwaka jana imeeonyesha kuwa  Rushwa ya ngono ilikuwepo kwa kiasi cha kuwakwamisha baadhi ya wanawake na wengine kuogopa kujitokeza katika nafasi hizo huku pia familia zikishindwa kuwaunga mkono wanawake wanaotaka kugombea kwa kile walichoita ni kuogopa aibu ya rushwa ya ngono kwa familia.

Wanawake mbalimbali wakichangia mijadala katika shughuli hiyo
Wanawake hao ambao walikutana kwa mara ya kwanza Mjini Dodoma mwaka 2015 kabla ya uchaguzi mkuu na baaadae kukutana Wiki hii kupeana mrejesho wa kile kilichotokea katika uchaguzi mkuu wa mwaka jana wamesema kuwa wanaitaka serikali Asasi za kiraia,TAKUKURU na wadau wengine kuongeza jitihada za kukemea Rushwa ya ngono na kuongeza uhamasishaji ili iweze kuzunguziwa kwa uwazi ili kutoa ushirikiano kwa vyombo vya sheria katika kulishughulikia Tatizo hilo.


Aidha wanawake hao wameitaka serikali kurekebisha sheria ya usajili wa vyama vya siasa ya mwaka 1992 itamke rasmi uwiano na usawa wa kijinsia katika nafasi kuu za maamuzi ndani ya vyama na pia sheria ivitake vyama vya siasa kuteua wanawake asilimia 50 kwenye kugombea nafasi za uongozi kuanzia ngazi za vijiji hadi Taifa.