Zinazobamba

UTEUZI WA MAWAZIRI UZINGATIE JINSIA- TGNP



Wawakilishi wa TGNP Mtandao, Action Aid Tanzania, FemAct  pamoja na wanaharakati ngazi ya jamii wakiongea na waandishi wa habari kuhusu ushiriki wa wanawake katika uchaguzi mkuu mwaka huu na uundwaji wa baraza la mawaziri

TGNP Mtandao, Action Aid Tanzania, FemAct  pamoja na wanaharakati ngazi ya jamii tumekuwa tukifuatilia kwa ukaribu mchakato mzima wa uchaguzi kuanzia hatua za awali, upigaji kura na baada ya matokeo kutangazwa. Nia yetu ni kufuatilia na kudai ushiriki kamilifu wa wanawake kwenye mchakato  mzima kama wagombea na wapiga kura.



Tunawapongeza Wanawake wote walioshiriki kwa kujitokeza kujindikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura, waliojitokeza kupiga kura na zaidi kabisa Wanawake wote waliogombea nafasi mbalimbali za uongozi bila kuvisahau vyama vya siasa na jamii zotezilizowawaunga mkono  na kufanikisha ushindi.



Tunawapongeza wanawake wote waliothubutu kujitokeza katika kinyanganyiro za uchaguzi kuanzia ngazi ya uteuzi ndani ya vyama na hatimaye baadhi yao kuingia kama wagombea. Kipekee tunampongeza Makamu wa Rais Mama Samia Suluhu kwa kudhubutu  na kufanikiwa kuwa makamu wa kwanza wa Rais Mwanamke tangu taifa letu kupata uhuru. Pamoja na hayo tunampongeza aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya chama cha ACT wazalendo Anna Mghwira kwa kuwa mgombea pekee mwanamke wa nafasi ya Urais kwa udhubutu na ujasiri aliouonesha. Tunatambua na kuthamini jitihada zake sio kugombea kwake tu, bali hata jinsi alivyobeba ajenda za msingi za wanawake na wananchi wa kawaida wakati wa kampeni.



Ndugu waandishi wa habari, takwimu zinaonesha kuwa, idadi ya wanawake mawaziri iliongezeka kutoka 14.8% (2003/05) kufikia 31.25% (2013/15) wakati idadi ya manaibu waziri wanawake ikipungua kutoka 30% (2003/05) hadi 24% (2013/15). Aidha, idadi ya makatibu wakuu wa wizara wanawake ilipungua kutoka 28% (2003/05) hadi 18.2% (2013/15) wakati idadi ya manaibu katibu wakuu wa wizara wanawake ikiongezeka kutoka 12.5%(2003/05)  hadi 40.7% (2013/15).

 Tanzania ni moja kati ya Mataifa yaliyosaini mikataba mbalimbali ya Kimataifa na kikanda inayoweka misingi ya usawa kwa binadamu ikiwemo haki na usawa  katika ushiriki kwenye uongozi wa ngazi zote. Moja kati ya Mikataba hiyo ni Tamko la Umoja wa Matifa la Haki za Binadamu(UDHR:1948), Mkataba wa Kimataifa wa Kutokomeza aina zote za Ubaguzi dhidi ya Wanawake (CEDAW: 1979, Articles 7: a, b na c), Mpango Kazi wa Beijing (1995), Mkataba wa Ziada wa Maputo, na Mkataba wa Nyongeza wa jinsia na Maendeleo kusini mwa Africa (SADC Gender Protocol,) ambayo inaelekeza serikali husika kuhakikisha wanawake wanapewa nafasi sawa na wanaume katika ngazi mbalimbali za uongozi.

Hivyo basi tunategemea kulingana na ahadi za viongozi wetu wakati wanaomba kura kuwa watasimamia utekelezaji wa mikataba mbalimbali ya kikanda na kimataifa, ni matarajio yetu kuwa serikali mpya chini ya  Mhe. Rais John Magufuli itatekeleza kwa vitendo ahadi hizo hususan katika kuwateua Wanawake zaidi katika nafasi za juu za uongozi katika mihimili mikuu mikuu mitatu ya serikali (Mahakama, baraza la mawaziri na bunge).



Pia ikumbukwe kuwa, Mhe. Rais Mstaafu Jakaya Kikwete akiwa katika Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa viongozi wa nchi wanachama uliofanyika mwaka huu 2015 nchini Marekani aliahidi kuwa Tanzania itasimamia utekelezaji wa kanuni ya 50/50 na kuweka mifumo mizuri ya ufuatiliaji na uwajibikaji wa utekelezaji wa masuala yote ya usawa wa kijinsia na matamko ya kimataifa na kikanda katika ngazi ya taifa na jamii.

Kwa kuzingatia hayo, tunasisitiza kuwa Baraza la Mawaziri lijalo pamoja na nafasi zote za uteuzi serikalini zibebe sura ya usawa wa Kijinsia. Nafasi nyinginezo ni pamoja na uteuzi wa wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, makatibu wakuu na naibu makatibu wakuu wa wizara mbalimbali, wakurugenzi na wakuu wa taasisi na mashirika ya umma kadhalika uteuzi wa bodi mbalimbali katika mashirika na taasisi hizo bila kusahau uteuzi katika mihimili ya mahakama na bunge. Ni matarajio yetu kuwa, mamlaka za kiuteuzi ikiwa ni pamoja na Rais, Waziri Mkuu na Mawaziri wa wizara mbalimbali watazingatia kikamilifu usawa wa kijinsia katika uteuzi wowote watakaofanya. TGNP Mtandao na Action Aid tutahakikisha kuwa tunafuatilia kwa karibu teuzi zitakazofanyika.

Mwisho tunawataka Wanawake wote waliochaguliwa kwenye nafasi za uongozi Ubunge na udiwani kuwajibika kikamilifu kwa kuitumikia Jamii iliyowapa ridhaa, waoneshe mfano wa kuigwa kwa kujenga hoja za msingi zenye maslahi mapana kwa Jamii hasa Wanawake  wanapokuwa kwenye Bunge au vikao vya Halmashauri ili kuleta tija na mabadiliko chanya kwa Jamii. Tunarajia kama ilivyokuwa katika awamu zilizopita sisi asasi za kiraia tutaendelea kushirikiana na serikali iliyoingia madarakani katika kuleta maendeleo ya Taifa.


No comments