HABARI KUBWA LEO,WABUNGE WA UKAWA WAIPOPOA BAJETI YA SERIKALI,WAGEUKA MBOGO,SOMA HAPO KUJUA HAPO
![]() |
| Mbunge wa Iringa Mjini, Peter Msigwa |
WABUNGE wamewasha moto kwa kuikosoa bajeti
inayopendekezwa na Serikali kwa mwaka wa fedha 2015/2016, wakisema imejikita
kuwakandamiza wananchi maskani huku ikikosa vyanzo vya uhakika vya mapato. Anaandika Pendo Omary … (endelea).
Moto huo wameuwasha wakati wakichangia
hotuba iliyowasilishwa bungeni Ijumaa iliyopita na Saada Mkuya, Waziri wa Fedha
na Uchumi ya Sh. 22.4 trioni.
Peter Msigwa wa
Iringa Mjini (Chadema), amesema kupandisha kodi ya mafuta ya taa, petroli na
dizeli ni kuwanyanyasa wananchi masikini.
Ameitaka serikali kuboresha sekta ya mtambuka ya utalii ambayo
inachangia pato la taifa kwa asilimia 17. Kwamba ni hifadhi mbili za Serengeti
na Kilimanjaro ndizo zinaweza kujiendesha kati ya hifadi 16.
“Tunapaswa kuwa
makini katika uhifadhi. Tusipime uhifadhi kwa kuangalia fedha. Mdhibiti na
Mkaguzi wa Hesabu za Serikali amesema asilimia 20 ya fedha zinazotegwa huwa
zinaliwa. Hivyo, hizo trioni 22.5 tunazotenga nazo zitaliwa,” amesema Msigwa.
Salehe Pamba wa
Pangani (CCM), amesema elimu kuhusu ukusanyaji Kodi ya Ongezeko la Thamani
(VAT), inapaswa kutolewa kwa wafanyabiashara na wananchi. Pia lazima
halmashauri zijengewe uwezo wa kukusanya angalau asilimia 10 ya kodi na
serikali kuwa na kiwango cha ukomo cha kukopa katika taasisi za ndani ya nchi.
“Lazima tukope
kiwango ambacho hakizuii wananchi na taasisi binafsi kukopa. Pia lazima kuwa na
mipango mahususi kwa ajili ya kuondoa utegemezi kutoka asilimia 15 ya sasa hadi
asilimia 5 au kufuta kabisa utegemezi. Nchi ikijitegemea itapata heshima,”
ameeleza Pamba.
Mbunge wa Lindi
Mjini, Salum Halfan Barwani (CUF), amesema “bajeti ya nchi ni tendo la
kisheria. Siku za nyuma wananchi walihamasika kufuatilia bajeti. Lakini siku
hizi wanaona ni tendo la kawaida.”
Amesema kwa sasa hata nusu ya bajeti haifiki kwa walegwa. Hakuna
vyanzo vipya vya mapato. Bajeti si rafiki kwa maisha ya kawaida ya Watanzania
wala mazingira ya nchi.
“Hakuna uwiano
wa mgawanyo wa rasilimali. Bado vigezo sahihi vya upimaji wa mgawanyo wa bajeti
havijawekwa. Tunataka serikali ya CCM ihakikishe mgawanyo sawa wa rasilimali
hata kama ni kidogo.” Ameeleza Barwani.
Naye Mohamed
Sanya wa Mji Mkongwe (CUF), amesema hana tatizo na kuongezeka kwa bei ya
mafuta. Ila ni busara kwa serikali kuangalia vyanzo vipya vya mapato.
“Serikali inapaswa
kukusanya kodi ya majengo. Inaweza kupata asilimia tatu katika majengo ambayo
hayalipiwi kodi kuliko kuhangaika na mafuta. Pia serikali ilipe deni ambalo
shirika lake la ndege linadaiwa ili kuendelea kufanya biashara ya usafiri
katika kanda na kimataifa kwa ajili ya kuongeza pato,” amesema Sanya.
Kwa upamde wake Moses Machali wa Kasulu Mjini (NCCR-Mageuzi),
amesema serikali inapaswa kujiuliza ni sababu zipi zimepelekea kukua kwa uchumi
wa Marekani ambapo kumepelekea kupanda kwa thamani ya Dola ya Marekani na
kushuka kwa Shilingi ya Tanzania.
“Kuna mahali tunafanya uzembe kama taifa. Hata kama utakusanya
fedha nyingi kiasi gani kama usimamizi wake ni mdogo, huwezi kuleta maendeleo.
Serikali imeshidwa kuangalia sekta za utalii, uchukuzi na usafiri wa anga
katika kuongeza mapato yake,” ameeleza Machali.
Suzan Kiwanga wa Viti Maalum (Chadema), amesema hakuna ongezeko
lolote la bajeti ya mwaka wa fedha 2015/16 kutoka bajeti ya mwaka 2014/15 kama
ambavyo Waziri Mkuya ametoa taarifa yake
wakati akisoma hotuba ya bajeti.
Amesema kushuka
kwa shilingi na kupanda kwa thamani ya dola kunasababisha kutokuwepo kwa
uharisia wa ongezeko la bajeti ya mwaka huu kwa sababu mwaka wa fedha uliopita
dola moja ya Marekani ilinunuliwa kwa Sh. 1500 na kwa mwaka huu inanunuliwa kwa
Sh. 2200.
“Mnapandisha bei ya
mafuta ili kupeleka umeme vijijini. Umeme ambao hata wananchi wa kawaida
vijijini hawautumii kutokana na gharama ambazo mnataka walipie. Gharama ya
nguzo peke yake ni Sh. 500,000,” amefafanua Kiwanga.
Kwa hisani ya Mwanahalisi oline

No comments
Post a Comment