Zinazobamba

WAZIRI NYALANDU AZIDI KUIMALIZA WIZARA YA MALIASILI NA UTALII,SASA ANASHIRIKIANA NA MAKADA WA CCM KUIMALIZA WIZARA HIYO SOMA HAPA UONE JINSI NYALANDU ANAVYOIMALIZA NCHI


                           Pichani ni Waziri wa Maliasili na Utalii Lazaro Nyalandu


WINGU la ufisadi, rushwa na upendeleo limetanda tena katika Wizara ya Maliasili na Utalii baada ya watendaji wake kudaiwa kugawa vibali vya kupasua mbao katika msitu wa serikali Sao Hill uliopo wilayani Mufindi Mkoani Iringa kwa watu wasio na sifa.
          Taarifa zilizokusanywa na Raia Mwema kwa wiki mbili sasa kutoka vyanzo mbalimbali zinabainisha kuwa vibali vya kupasua mbao kwa mwaka huu 2014-15 vimetolewa kwa upendeleo huku rushwa ikitawala mchakato mzima wa zoezi hilo.
           Wanaotuhumiwa kwa ufisadi huo ni pamoja na kamati ya ugawaji yamsitu ambayo inawahusisha menejimenti ya Sao Hill, Maafisa wa Idara ya Misitu katika Wizara ya Maliasili na Utalii na Naibu Waziri wa Wizara hiyo Mahmoud Mgimwa.

            Kwa kawaida vibali hutolewa kwa wafanyabiashara wenye sifa muhimu, kama kuwa na leseni ya biashara ya mbao na pia mashine za kupasua mbao za viwango vya juu (kiwanda) za kati na wajasiriamali wadogo.
            Hata hivyo, kinyume cha utaratibu huo katika utoaji vibali kwa mwaka huu inadaiwa kuwa idadi kubwa ya majina ya watu na taasisi zilizopewa vibali ni ya watu wasiofanya biashara hiyo kabisa wakiwemo wanafunzi.
Orodha ya waliopewa vibali
           Katika uchunguzi wake Raia Mwema imebaini kuwa katika orodha iliyotolewa na Kamati ya Ugawaji kuna majina mengi ya vigogo  na  makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Iringa na wafanyabiashara ambao ni ndugu na marafiki wa karibu wa viongozi hao.
              Orodha hiyo pia ina majina ya mashirika yasiyo ya kiserikali, taasisi za dini na chama cha Wandishi wa Habari Mkoa wa Iringa ambavyo kimsingi hazifanyi biashara ya mbao.
       Katika orodha hiyo (nakala tunayo) pia wamo watu wanaodaiwa kuwa majirani, na ndugu wa karibu wa Naibu Waziri Mgimwa ambaye pia ni Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kaskazini (CCM).
               Kutajwa kwa Naibu  Waziri huyo kumechochea zaidi madai ya kuwapo kwa ufisadi katika zoezi hilo hasa ikizingatiwa kuwa  yeye ni Mbunge wa eneo hilo na pia ni Waziri anayehusika moja kwa moja na Wizara inayosimamia  msitu huo.
           Viongozi wa CCM wanaotajwa kupewa hekta za uvunaji miti ni pamoja na Spika wa Bunge la Tanzania Anne Makinda kupitia kampuni yake ya Makinda One to One Co.Ltd ambayo imepewa mita za ujazo 450 kuvuna miti aina ya misindano.
            Orodha hiyo pia inamhusisha Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Njombe Deo Sanga (Jah People)  ambaye pia ni Mbunge wa Makambako  ambaye kampuni yake ya Jah People Transport Ltd imemegewa mita za ujazo 200 huku yeye binafsi pia akipewe mita nyingine za ujazo 200.
              Aidha, orodha hiyo ya vigogo wa CCM pia inamhusisha Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Pindi Chana, kupitia kampuni ya Pindi Chana Garage iliyogawiwa mita 200 za ujazo huku Katibu Mwenezi wa CCM Wilaya ya Mufindi Yasin Daud Mlowe, kuptia kampuni tatu tofauti akipatiwa jumla ya mita za ujazo 600.
             Mjumbe wa CCM (Mkutano Mkuu) Mkoa wa Iringa, Godfrey Mosha amemegewa vitalu viwili  kupitia kampuni zake za Mufindi Wood Plantation & Industries  na Mufindi Environmental Trust (MUET) jumla ya  mita za ujazo 400.
             Orodha hiyo pia inaoonyesha kuwa mke wa Mosha ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) Wilaya ya Mufindi  Marselina M. Mkini amepewa mita za ujazo 200 na Mariam Angetile Hidda  ambaye anatajwa  kuwa ni Mke wa Mkurugenzi Jiji la Mwanza  Khalifa Hidda.
             Majina mengine ambayo yanatiliwa shaka kuwa hayakustahili kupewa vibali ni pamoja na Inocent Menrard Kigola anayedaiwa kuwa mtoto wa Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini (mwanafunzi) , Halima Mahmoud Mgagula anayedaiwa kuwa mtoto wa Mgimwa na Evarist Mangala ambaye aliwahi kuwa Kamanda wa Polisi Mkoa wa Iringa.
                   Kuna pia watu wanaodaiwa kuwa karibu na wakuu wa wilaya kadhaa za Mkoa wa Iringa, Wenyeviti wa Halmashauri, Madiwani, Maafisa wa Polisi ngazi ya Mkoa na watumishi wa juu wa idara nyingine nyeti za serikali.
          “Hawa ni viongozi wa CCM na serikali na wengi wao hawana hata leseni ya biashara ya mbao wala hawana sifa ya kupewa vitalu vya miti, hivyo kilichofanywa na kamati ya ugawaji ni ukiukwaji mkubwa sheria na taratibu,” alieleza mtoa taarifa wetu.
           Taarifa zinabainisha kuwa mmoja wa wafanyabiashara maarufu wilayani Mufindi, Hezron Ng’umbi, ambaye anadaiwa kuwa na uhusiano wa karibu na Naibu Waziri Mgimwa amemegewa vitalu zaidi ya vitano kupitia kampuni zake na ndugu zake wa karibu.
          Kampuni zinadaiwa kuhusishwa na mfanyabiashara huyo ni pamoja na C.F Investiment Co.Ltd., Mtili G. Enterprises, Mtili Sawmill & Timber, Ng’umbi Services &Timber, Sitex  Enterprises,  CFN Enterprises na West Solution Ltd.
       Katika orodha hiyo pia inawahusisha ndugu wa karibu wa mfanyabiashara huyo ambaye ni pamoja na Chesco Fransis Ng’umbi, Christian Fransis Ng’umbi, Agness Elias Mwagala, Rehema Yeriko Mwagala na Stewart F. Ng’umbi.
          “Majina hayo yote ni yanahusishwa na huyo mfanyabiashara Hezron Ng’umbi ambaye kwa njia ambazo tunadhani si halali amepewa vitalu vya kuvuna miti zaidi ya vitalu saba kinyume cha utaratibu kuwa kila mwombaji atapatiwa kitalu kimoja,” kilieleza chanzo chetu.
           Aidha uchambuzi wa majina hayo unaonyesha kuna majina 31 yanayodaiwa kuwa ni ya watu wenye maslahi ya moja kwa moja na Naibu Waziri Mgimwa na inadaiwa kuwa wamepewa vibali kwa ushawishi wake.
Jinsi biashara inavyofanyika
               Uchunguzi wa Raia Mwema umebaini kuwa baada ya wahusika kupewa vibali hivyo, huviuza kwa wafanyabiashara wakubwa wa mbao kwa bei kati ya shilingi milioni 7-13 kulingana na mapatano na hivyo kupata faida bila kuwekeza chochote.
           Wandishi wa habari wa gazeti hili walifanya mazungumzo na baadhi ya wafanyabiashara wa mbao mjini Mufindi ambao walikuwa katika harakati za kutafuta wadau wenye vibali ili wavinunue kwa ajili ya viwanda vyao.
              “Kama una kibali hakuna shida. Tuna fedha za kutosha na nitakulipa kupitia benki au hata fedha taslimu, ukitaka hakuna tatizo,” alisema mfanyabiashara mmoja huku akiwa amezungukwa na madalali wanaomtafutia vibali vya kununua.
                            Uchunguzi zaidi unaonyesha ya kuwa wengi wa watu waliopata vibali wametumia ushawishi wa nafasi zao za uongozi pamoja na baadhi wakitumia  njia za rushwa.
               Akizungumza na Raia Mwema mmoja wa wadau wa biashara ya mbao George Kavenuke ambaye pia ni mjumbe wa Mkutano Mkuu CCM, Mkoa wa Iringa, alieleza kuwa kilichofanyika na Kamati ya Ugawaji na Wizara ni ukiukwaji mkubwa wa haki za wananchi wa Mufindi.
          “Ugawaji huu ni batili. Vibali vimetolewa bila kuzingatia vigezo. Kuna wajasiriamali wenye mashine za kupasua mbao ambao wamewekeza fedha zao hawajapewa vipaumbele katika ugawaji jambo ambalo si haki kabisa,” alisema Kavenuka.
        “Kwa msingi huo tunamtaka Waziri mhusika (Maliasili na Utalii) Lazaro Nyalandu kufuta haraka vibali vyote ili utaratibu ufanyike upya na waliohusika na uzembe huu wachukuliwe hatua,” alisema Kavenuka.
            Mfanyabiashara mwingine William Mgowole alieleza kuwa hatua ya kunyimwa vibali pamoja na kwamba wana sifa na wameifanya kazi hiyo kwa zaidi ya miaka 35 ni kuwanyima haki wananchi wa Wilaya Mufindi.
         “Binafsi nimeifanya kazi hii kwa zaidi ya miaka 30 nimewekeza nguvu, fedha na rasilimali zangu nyingi, ghafla leo naambiwa kwamba sina sifa ya kupewa kitalu cha kuvuna miti, lakini wakati huo kuna watu wamepwa vibali  zaidi ya kimoja  bila kuwa na sifa na badala yake wanafanya ulanguzi  jambo hili halikubaliki,” alisema Mgowole.
           Aliongeza kuwa hatua hiyo inaathari kubwa kwa maisha na uchumi wa wananchi wengi wa wilaya hiyo ambao  wanategemea biashara hiyo kama njia ya kujikumu kimaisha na itawandoa katika ajira watu zaidi ya 2000 ambao walikuwa wameajiriwa katika viwanda vya kati.
Majibu ya wanaotuhumiwa
          Akizunguzia madai hayo Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mahmoud Mgimwa aliliambia Raia Mwema kuwa taarifa hizo ni uzushi mtupu na hahusiki kwa namna yoyote katika ugawaji wa vitalu vya miti ya kupasua mbao.
           “Mimi kama Naibu  Waziri wa Maliasili na Utalii sihusiki kwa njia yoyote na ugawaji wa vitalu, kuna  Wakala wa Misitu  (TFS) pamoja na menejimenti  ya mashamba ya Sao Hill. Majukumu ya ugawaji yameachwa mikononi mwao,” alisema.
         “Madai yanayoenezwa yamelenga kunichafua kisiasa hasa ukizingatia kuwa mwakani tunafanya uchaguzi. Kuna watu wameanza kupitapita kuwalaghai wananchi na moja ya turufu zao ni kunichafua kupitia  habari za ugawaji wa vitalu vya miti,”alisema Mgimwa.
           Kwa upande wake Meneja wa Shamba hilo Saleh Beleko alikiri kuwapo malalamiko katika ugawaji lakini akatuma lawama  kwa TFS ambao ndio waliohusika kutoa orodha ya mwisho ya waliofanikiwa kupata vibali.
            “Sisi kama menejimenti ya shamba kazi yetu ni kupokea maombi ya watu wote na tukishapokea tunapeleka Dar es Salaam  kwa TFS ambao hutuletea orodha ya walioidhinishwa  na kazi yetu ni kuitangaza,” alisema Beleko.
           Juhudi za kumpata Mtendaji Mkuu wa TFS, Juma Mgowo, hazikuweza kufanikiwa kama ambavyo waandishi walivyoshindwa kuwapata, hadi tukienda mitamboni, Spika Makinda, Chana, Sanga na wengine wanaotajwa kwenye nyaraka za mgao huo wa vitalu vya mbao.
             Kwa upande wake mfanyabiasha Hezron Ng’umbi ambaye anatuhumiwa kutumia  ukwasi wake kujilimbikizia vitalu alikanusha madai hayo na kuongeza kuwa hata yeye ni mhanga wa ugawaji uliofanyika.
             “Makampuni na majina yanayohusishwa na mimi siyafahamu, nimepewa mita za ujazo 450 kwa  jina langu la Chesco Fransis. Kiasi hiki ni kidogo sana.  Nitavuna kwa wiki mbili baada ya hapo inabidi nifunge kiwanda kwa sababu nitakuwa sina malighafi,” alisema.
           Aliongeza kuwa kiwanda chake kimeajiri zaidi ya watu 60, ambao hata ajira yao itakoma baada ya kumaliza kupasua mbao katika eneo alililopewa  na kusisitiza kuwa  ugawaji wa msitu huo kwa mwaka huu umekiuka taratibu.

Chanzo ni Gazeti la Raia Mwema

No comments