Zinazobamba

EXCLUSIVE---NANI ANAFAA KUMRITHI HECHE BAVICHA?SOMA HAPA KUJUA ZAIDI


Freeman Mbowe
Pichani ni Mwenyekiti wa Chadema Freeman Mbowe picha na Maktaba


Na Edson Kamukara
      NIKIWA kijana ninayeamini katika siasa za mabadiliko, najiona nina wajibu na kila sababu ya kutoa maoni na ushauri wangu kwa viongozi wa Baraza la Vijana Taifa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (BAVICHA), unaomaliza muda wake ili wahakikishe wanapata warithi makini.
               Swali hili na nani anafaa kumrithi Mwenyekiti wa BAVICHA, John Heche, kwa leo nitalijibu kwa kutaja sifa za mtu anayehitajika kuliongoza baraza hilo nyeti ambalo naweza kulifananisha kama nguzo mhimu ndani ya CHADEMA.
              Ila katika makala yangu ijayo, nitawataja moja kwa moja wagombea hao kwa majina ili kutoa mwangaza kwa wajumbe, wapime kama wanazo sifa za kuitoa BAVICHA hapa ilipo na kuisogeza katika hatua nyingine ya kuwawezesha vijana kuikomboa nchi yao mikononi mwa mafisadi.

           Ninapomtaja Heche, sina shaka kwamba ni kiongozi ambaye amejijengea umaarufu wa kutosha kwa kipindi alichoiongoza BAVICHA kama mwenyekiti aliyerithi mikoba ya mtangulizi wake John Mnyika.
             Nimemfahamu Heche kwa miaka kadhaa tukiwa pamoja katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine, Mwanza (SAUT). Huyu tumekutana na kufahamiana katika siasa kupitia tawi letu la chuo, nikiwa mwenyekiti mwanzilishi wa tawi hilo.
          Heche alijiunga SAUT mwaka mmoja nyuma yangu, ingawa ilituchukua muda mfupi mimi na viongozi wenzagu kufahamiana naye kutokana na ujasiri wake wa kuwa mstari wa mbele katika kusimamia masuala ya CHADEMA.
          Wakati tunafikia kipindi cha ukomo wa uongozi wetu, Heche alikuwa ni mtu ambaye kila mmoja wetu alitamani arithi nafasi mojawapo kati ya mwenyekiti au katibu wa chama.
          Tamanio letu lilitimia tena katika mazingira ya kushangaza kidogo kwa sababu Heche alishinda uchaguzi na kuwabwaga wagombea wengine katika nafasi ya ukatibu bila kuwepo kujinadi kwa wapiga kura.
             Hii ndiyo ilikuwa sababu yangu ya kwanza kuamini uwezo wake na kukubalika kwake kwa wenzake, japo hakuma maarufu sana bali wajumbe walithamini uwezo na ujasiri wake aliouonyesha wakati tukiwekewa mizengwe na viongozi wa CCM tawi hadi mkoa kuhakikisha tawi letu halifunguliwi.
             Hata aliponishirikisha kusudio lake na kutaka kuwania uenyekiti wa BAVICHA Taifa, nilimpa matumaini kwa vile niliamini ndiye mtu sahihi aliyepaswa kurithi mikoba ya Mnyika aliyekuwa ameitumikia BAVICHA kwa mafanikio makubwa.
             Nasema tena kwamba Heche aliiongoza BAVICHA akiwa si maarufu lakini anaondoka akiwa amepata umaarufu mkubwa kwa sababu alitumikia wadhifa huo akiwa na nia, malengo na madhumuni ya kuieneza CHADEMA kupitia baraza hilo.
               Heche hakugombea uenyekiti kutafuta sifa ya kukuza umaarufu wa jina lake, hakutumia rushwa ili achaguliwe, hakuwa na kundi nyuma yake lililomtanguliza ili alinde maslahi yake na kubwa zaidi alikipenda CHADEMA kwa moyo wa dhati akiamini katika mabadiliko ya kuona siku moja kikiwa chama tawala.
           Si kusudio langu kumsifia Heche katika makala haya, isipokuwa nilikuwa najenga msingi wa hoja yangu ili nipate kueleweka ninapouliza ni nani anafaa kumrithi mwenyekiti huyu BAVICHA.
               Ni kweli wamejitokeza vijana wengi kuchukua fomu za kugombea nafasi mbalimbali za BAVICHA kila mmoja kulingana na matamanio yake. Niseme nawapongeza wote ambao wameisha chukua fomu hizo na kuzirudisha bila kujali kama wanatosha au hawatoshi kivigezo.
                  Kujitokeza kuchukua fomu ni ushujaa, achilia mbali kwamba ni haki ya kikatiba. Sasa kazi ya kumpata mgombea makini wa kuivusha CHADEMA hapa ilipo na kwenda mbali zaidi, itategemea mchujo wataoufanya wakina Heche na wenzeke kisha majina hayo kuamuliwa kwa wajumbe wa BAVICHA.
             Iwapo mchujo wa wakaina Heche utaegemea kwenye ushwahiba, rushwa, ubinafsi, kulindana, umaarufu, eneo analotoka mgombea, dini, kabila na upuuzi mwingine, ni dhahiri watakuwa wameiuza na kuizika rasmi BAVICHA.
              Katika kuteua wagombea, husuasani nafasi ya mwenyekiti na makamu wake, Heche na wenzake lazima wajikumbushe usaliti wa akina Juliana Shonza, Habib Mchange, Mwampamba na wengineo, ambao waliingia kwenye mchakato wakati huo kwa kulinda matakwa ya wafadhili wao kisiasa na sio kukijenga CHADEMA.
                 Lazima watambue kuwa hata kwenye kundi kubwa hili la vijana waliojitokeza kuomba kuwarithi, wengi wana malengo yao binafsi wala hawako kwa ajili ya kukipigania CHADEMA kisonge mbele kushika dola 2015.
              Wajue kuwa humo wamo wanaotafuta umaarufu wa kutangaza majina yao, wako wanaotumiwa na makundi ya kusaka madaraka lakini mbaya zaidi wako waliopandikizwa kwa fedha chafu za wapinzani wao kisiasa ili waingie kuwavujishia siri za CHADEMA.
               Kwa hiyo, iwapo Heche na wasaidizi wake watadanganyika na umaarufu wa mgombea, kuzunguka kwake mikoani kwenye ziara za chama, kutoa matamko mengi alipokuwa chuoni, bila kuzingatia utiifu wake, mapenzi mema kwa chama na uwezo wake binafsi katika kukieneza CHADEMA, BAVICHA itakufa na wao waaibika.
              Sio kazi ya Heche wala katibu mkuu wake, Deogratius Munishi au kiongozi yoyote wa BAVICHA taifa, kujigeuza mshauri nasaa wa kuwapigia ramri baadhi ya wagombea na kuwaelekeza wawanie nafasi fulani. Kiongozi anaye wania nafasi ya kulazimishwa, kamwe hawezi kuitumikia kwa dhati.
              Huyu atababishwa, atarubuniwa, atanunulika na huyo hawezi kuisongesha BAVICHA katika kuiongoza CHADEMA kutwaa madaraka 2015.
            Makala ijayo, nitawataja wagombea ambao kwa upeo wangu nadhani wanaweza kuivusha BAVICHA endapo watapata ridhaaa ya kuchaguliwa.
            Kila la kheri Heche na wenzako katika kupata warithi wenu.

No comments