Zinazobamba

UHURU KENYATA ANAPOLILIA LUGHA YA KISWAHILI, ASEMA ANGEPENDA KITUMIKE KUWAUNGANISHA WANA AFRIKA MASHARIKI.

Rais Uhuru Kenyatta ametoa wito Kiswahili kitumiwe kuleta umoja baina ya wananchi wa mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Uhuru Kenyatta
Rais Uhuru Kenyatta akihutubu awali. Picha/PPS
RAIS Uhuru Kenyatta ametoa wito Kiswahili kitumiwe kuleta umoja baina ya wananchi wa mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Akihotubia wabunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) waliokuwa katika Bunge la Kitaifa Nairobi Jumanne, rais alisema utumizi wa Kiswahili baina ya wananchi wa EAC ni njia mwafaka ya kudumisha utambulisho wa pamoja ulio wa kipekee.
“Mungu ametupatia sauti inayoweza kuleta umoja baina ya wananchi wote Afrika Mashariki, na tunafaa tuitumie ipasavyo kupitia vyombo tofauti vya habari ili kutimiza utangamano,” alisema.
Hata hivyo, kinaya iliyodhihirika ni kuwa alitoa hotuba yake yote kwa Kiingereza.
Rais Kenyatta alitoa hakikisho kuwa juhudi za kutimiza umoja kati ya mataifa ya EAC ziko sambamba, ingawa hakuna usawa kati ya mataifa katika utekelezaji wa mikakati ya kukamilisha juhudi hizo.(BMCL)
Alitoa wito kwa wabunge hao wajitahidi kupitisha sheria zitakazodumisha umoja wa EAC, hasa zinazohusu uendelezaji wa biashara kati ya mataifa husika.
Spika wa bunge la EALA Margaret Zziwa alimmiminia sifa Rais Kenyatta kwa kusema amedhihirisha kujitolea kwa Serikali anayoongoza katika kutimiza maazimio ya EAC.


Kulingana na Bi Zziwa, hatua ya Serikali kukabiliana na changamoto zilizokuwa zikiwakumba wafanyabiashara wanaopitisha mizigo katika maeneo ya mipaka na katika bandari ya Mombasa ni ishara ya kujitolea kwa Serikali kutimiza malengo ya EAC.
“Hatua hii imeboresha biashara na hakika, wafanyabiashara katika mataifa ya EAC tayari wanafaidika kwenye biashara zao,” alisema.
Mwenyekiti wa wabunge wa EALA kutoka Tanzania Adam Kimbisa, alimshauri Rais Kenyatta awe “mtumwa” kwa wananchi.
“Maisha yako sasa yamebadilika kutoka uhuru na kuwa utumwa. Ukiwa mtumwa kwa wananchi, hiyo ni taadhima na baraka kwako, na Mungu atakubariki sana,” alisema Bw Kimbisa.
Vijana
Alitumia muda aliopewa kumsifu Rais Kenyatta kwa kujitolea kwake kuleta umoja baina ya mataifa ya bara la Afrika.
Alizua kicheko bungeni alipomwambia Rais Kenyatta ashauri viongozi wenzake wa mataifa ya Afrika kuhusu jinsi ya kutawala kama vijana.
“Nadhani itakuwa msaada sana ukionana na marais wenzako na kuwaambia “waoneni hawa vijana”, nao waweze kuchangamka,” alisema.
Rais pia alisifiwa kwa mipango ya kipekee iliyoanzishwa na Serikali, kama vile mradi wa kupeana vipakatalishi kwa watoto wa shule za msingi.
“Kuna mataifa mengi Afrika ambayo yameshindwa kununulia wanafunzi kitabu na kalamu, ilhali wewe unafuata mkondo wa dijitali kwa elimu,” alisema Bw Kimbisa.
Alikariri msimamo wa EALA kuunga mkono Muungano wa Afrika (AU) kuhusiana na kesi zinazomkabili rais na naibu wake William Ruto katika Mahakama ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC).

No comments