MKUU WA WILAYA YA SAME ATEMBELEA MRADI WA MAJI SAME-MWANGA-KOROGWE
Mkuu wa Wilaya ya Same, Mhe. Kasilda Mgeni akiongozana na kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo, leo machi 03, 2025 wametembelea mradi mkubwa wa maji wa Same-Mwanga-Korogwe, Ziara hii imelenga kukagua maendeleo ya mradi huo unaotekelezwa kwa lengo la kuboresha upatikanaji wa maji safi na salama kwa wakazi wa mikoa ya Kilimanjaro na Tanga.
Katika ziara hiyo, Meneja wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Same (SAMWASA), Mhandisi Rashidi Mwinjuma, alieleza kuwa mradi huu umefikia hatua nzuri ya utekelezaji na unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa maji safi kwa wananchi wa Same, Mwanga na Korogwe.
Mradi wa maji wa Same-Mwanga-Korogwe unalenga kuhudumia zaidi ya wakazi milioni moja, ikiwa ni hatua muhimu katika kuimarisha huduma za maji safi na usafi wa mazingira. Kupitia mradi huu, changamoto za upatikanaji wa maji katika maeneo husika zitapungua kwa kiasi kikubwa, hivyo kusaidia kuboresha hali ya maisha ya wananchi, sekta ya kilimo, mifugo, na viwanda vidogo vidogo.Mhe. Kasilda Mgeni amepongeza jitihada za serikali na wadau wote wanaoshiriki katika utekelezaji wa mradi huu. Ameeleza kuwa serikali ya awamu ya sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuwekeza katika miradi mikubwa ya maji kama sehemu ya mkakati wa kuboresha huduma za msingi kwa wananchi.
Mradi huu unatarajiwa kuzinduliwa rasmi na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, tarehe 9 Machi 2025. Uzinduzi huu utakuwa ni hatua muhimu katika juhudi za serikali kuhakikisha upatikanaji wa maji safi na salama kwa Watanzania, hususan katika maeneo ya Same, Mwanga na Korogwe.
Hakuna maoni
Chapisha Maoni