Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu ,Kazi,Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu Profesa Joyce Ndalichako
NA Mussa Augustine.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu
,Kazi,Vijana,Ajira na Wenye Ulemavu Profesa Joyce Ndalichako amewataka Mawakala
Binafsi wa Ajira ndani na nje wanapowatafutia Watanzania ajira nje
ya nchi wazingatie utu na kwamba wasipofanya hivyo watachukuliwa hatua za
kisheria ikiwemo kuwafutia leseni zao.
Agizo hilo amelitoa Oktoba 23,2023 Jijini Dar es salaam wakati
alipokutana na Wakala binafsi wa huduma za ajira ajili ya Kujadili namna ya kuongeza ufanisi na kutatua
changamoto zinazowakabili mawakala hao.
Profesa Ndalichako amesema kuwa mawakala hao
wazingatie matakwa ya kisheria katika kuendesha shughuli zao,hivyo wanapaswa
kuhakikisha watanzania wanaoenda kufanya kazi nje ya nchi wanapata haki zao kwa
mujibu wa sheria.
Aidha pia amewataka mawakala hao kutovuka
mipaka yao ya kazi ikiwemo kushikilia mishahara ya wafanyakazi waliowatafutia
ajira,huku wakiwachukulia nusu ya mishahara,ambapo amesema wakibainika
watachukuliwa hatua za kisheria.
Amesema kuwa Serikali ilisitisha huduma za
ajira nje ya nchi mwaka 2018 baada ya serikali kuona mawakala hao walikuwa
wanaangalia kipato kuliko utu wa mtanzania.
“Mawakala mnapowapeleka Watanzania nje ya
nchi utu wa mtanzania uthaminiwe, Serikali haipo tayari kuona wananyimwa
stahiki zao,hawana mikataba na wakitaka kuondoka hawana uhuru wa kurudi
nyumbani,serikali itachukua hatua kwa wakala yeyote atakaebainika”amesisitiza
Profesa Ndalichako
Nakuongeza kuwa "Nawasihi mawakala wote
kuzingatia matakwa ya kisheria katika kuendesha shughuli
zenu na wale wachache wanaokiuka misingi ya kisheria watachukuliwa hatua
za kisheria ikiwemo kufuta leseni,
Ameongeza kuwa wapo mawakala wachache
wanaofanya shughuli hapa nchini ambao hawazingatii sheria ikiwemo kujihusisha
na mahusiano ya kiajira na wafanyakazi wanaotakiwa kuwaunganisha na waajiri
wanashindwa kuwapatia wafanyakazi wao mikataba ya ajira na kutowachangia
katika Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.
Profesa Ndalichako alisema vitendo
hivyo ni ukiukwaji wa sheria za kazi pamoja na ukiukwaji wa haki za
binadamu.
Amesema Serikali imeruhusu mawakala binafsi
kuunganisha watanzania na fursa za ajira nje ya nchi kufanyika ambapo kwa mwaka
wa fedha 2022/23 takribani mawakala 83 walisajiliwa kati ya hao 56
wamehuisha leseni zao kwa mwaka 2023/24.
Naye Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Cyprian
Luhemeja amewataka mawakala hao kushirikiana na serikali kumaliza
changamoto ya ajira nchi.
"Naamini leo tutajadiliana jinsi ya
kuongeza ubunifu na ufanisi katika kuboresha na kumaliza changamoto ya
ajira nchini kwasababu Tanzania tumechelewa sana kupeleka watanzania nje ya
nchi hivyo serikali inawaunga lakini kwa kufuata utaratibu mzuri wa kuwapeleka
watanzania nje na utaratibu uwe wa leseni," alisema Luhemeja.
Mwakilishi wa mawakala binafsi wa Ajira ndani
na nje ya nchi ,Bona Manyema alisema anaishukuru Serikali kwa kuwawekea
mazingira wezeshi na wameahidi kufuata tararibu hivyo atakayeenda tofauti
na hayo atachukuliwa hatua za sheria.
Hakuna maoni
Chapisha Maoni