Zinazobamba

KUMFANANISHA IMAAM HUSSEIN NA NABII ISA" YAANI YESU" NI UPOTOSHAJI ULIOVUKA MIPAKA...


Na Mwandishi wetu,


Katika kuendeleza upotovu wao, Mashia wamemfananisha mjukuu wa Hussein na Nabii Isa, na kwamba eti Nabii Isa aliuawa akipigania haki, mambo ambayo si ya kweli na yanapingana Qur’an na Sunna za Mtume.
Kauli hizo za upotofu za Mashia zilisikika Jumapili iliyopita katika kituo cha Mashia cha Ghadir kilichopo Kigogo jijini Dares Salaam, ambako kulifanyika semina yenye anuani  ‘Jitihada za Imam Hussein na Masihi Yesu katika kusimamisha haki na amani ya dunia”. Katika hotuba yake, Sheikh wa dini hiyo ya Mashia, Hemed Jalala alidai kuwa amani, mapenzi, huruma, utulivu na maelewano baina ya wanajamii vitatokana na kuyasoma maisha ya Nabii Issa (amani ya Allah iwe juu yake) sanjari na kufanyia kazi harakati za utumishi wa Walii wa Mwenyezi Mungu (Imam Hussein) kama mrithi wa kiti cha Utume wa Muhammad (rehema na amani ya Allah iwe juu yake).
 Alisema malengo ya Nabii Issa yalikuwa ni kuleta mabadiliko kwenye jamii yake kama ilivyokuwa kwa Imamu Hussein (Allah amridhie) ambaye katika kipindi chote cha maisha yake alihakikisha haki na amani vinatawala katika mji wa Karbala (Iraq).
Katika hali ya kushangaza kiongozi huyo wa jamii ya Mashia alidai Waislamu, Mayahudi na Wakristo ni ndugu, na ndiyo maana ndani ya Qur’an kuna sura mbalimbali zinazoonesha mahusiano ya karibu kati ya watu wa dini hizo. Alizitaja sura hizo kuwa ni Maryam –yaani- sura ya Mariam Mtakatifu ambayo Wakristo huitambua kama sura ya Bikira Maria, pamoja na Surati Ruum yaani sura ya Roma. Kwa ajili hiyo, akawataka wasomi na jamii ya Watanzania kuwa macho na maadui wasioutambua Uislamu ambao moja ya harakati zao ni kutaka kuiaminisha jamii kuwa, Waislamu na Wakristo ni watu waliotofautiana sana.
Sheikh Jalala aliwaambia wajumbe wa semina hiyo kuwa, dini za Uislamu, Ukristo na Uyahudi kwa pamoja zimekuja na misingi mitatu ambayo ni kumuabudu Mungu mmoja, kumuamini mjumbe aliyetumwa na Mungu, na kuamini siku ya mwisho.
 Kuhusiana na itikadi ya Wakristo katika kuamini utatu, Mtakatifu Sheikh Jalala alisema, hilo ni suala la tofauti za kifalsafa na mitazamo katika madhehebu, lakini ukweli ni kuwa kinachotoka katika vinywa vyao ni neno la Mungu mmoja. “Waislamu na Wakristo ni ndugu, na Nabii Issa  (amani ya Allah ziwe juu yake), Hussein bin Ali (amani ya Allah iwe juu yake), pamoja na Mtume (Rehema na amani ya Allah zimfikie) wote ukijaribu kuwasoma utagundua kuwa walichokilingania ni kitu kimoja, lakini pia hata lugha yao ni moja” alibainisha.
 Katika hali ya kushangaza, pamoja na maneno yake hayo, bado alinukuu aya za Mwenyezi Mungu zinazosema: “Huyo ndiye Isa mwana wa Maryamu, hiyo ndiyo kauli ya haki ambayo wanaifanyia shaka. Haiwi kwa Mwenyezi Mungu kuwa na mwana, Subhanahu, Yeye ametakasika! Anapolihukumia jambo basi huliambia tu: kuwa! Likawa” (Qur’an, 19:34-35). Ukitafakari juu ya maneno ya Jalala, utaona ni juhudi za Mashia kutaka kujikurubisha kwa wasio Waislamu kitaqiya hata kwa kuziuza aya za Allah Ta’ala kwa thamani ndogo ya kidunia.
Allah Ta’ala anasema kuwaambia wana wa Israeli: “Na wala msiivike haki batili na mkaificha haki na huku mnajua” (Qur’an 2: 42 ). Jalala amefanya talbisi nyingi katika hotuba yake hiyo. Kwanza amemlinganisha Hussein bin Ali (Allah amridhie) na Manabii wawili wa Allah katika wale Mitume wakuu watano waitwao ‘Ulu al‘azmi” yaani Nabii Nuhu, Nabii Ibrahim,  Nabii Musa, Nabii Isa na Nabii Muhammad (amani za Allah ziwe juu yao). Hilo ni kosa kiitikadi kwa sababu mjukuu wa Mtume Hussein bin Ali (Allah amridhie) alikuwa mwanadamu wa kawaida tu na wala si Mtume wala Nabii.
 Pamoja na juhudi yake kupinga na kuondoa dhulma iliyozuka zama za fitna, Hussein bin Ali katu hawezi kulinganishwa na Manabii hao wawili wa Allah. Halafu Jalala akasema: “…Nabii Isa na Hussein wote wawili waliuawa wakipigania haki na kupinga dhulma”. Kudai kwamba Nabii Isa aliuawa hiyo ni imani ya Wakristo na Wayahudi.
Ama Waislamu wa Ahlus Sunnah imani yetu kuhusu Isa ni hii. “Na walisema hakika sisi tumemuuwa Isa mwana wa Maryam mtume wa Allah, na wala hawakumuua na wala hawakumsulubu lakini walishabihishiwa (hivyo), na hakika wale waliotofautiana kuhusu yeye (Isa) wako katika shaka juu yake, hawana elimu juu ya hilo isipokuwa kufuata dhana, na wala hawakumuuwa kwa yakini” (Qur’an, 4:137).
Sasa Jalala anaposema Nabii Isa (amani ya Allah iwe juu yake) na Imam Hussein waliuawa wakipigania haki, kama lipo katika itikadi za Shia au alikuwa anafanya taqiya ni vema akabainisha na kama alikuwa anawafurahisha Wakristo basi ajuwe amemuudhi Allah Taa’la. Lakini hatushangai sana kwani hiyo ndiyo itikadi ya Mashia juu ya maimamu wao kwamba nao wanapokea wahyi kama manabii na hata kudai maimamu wao ni bora kuliko hata manabii! Astaghfirullah.
Wakati Jalala akitangaza kwamba Mashia ni kitu na ndugu moja na Mayahudi na Wakristo, Mashia hao hao wanajiona ni tofauti na Masunni lakini kwa Mayahudi na Wakristo wao ni kitu kimoja. Sisi tumeambiwa: “Hakika Waumini ni ndugu, basi patanisheni baina ya ndugu zenu, na mcheni Mwenyezi Mungu ili mrehemewe”(Qur’an, 49:10) Aliyesema Wakristo ni tofauti na Waislamu ni Allah Jalala anadai kwamba wanaoamini kuwa Wakristo na Waislamu ni watu wanaotofautiana sana ni maadui na wasioutambua Uislamu.
Huku ni kupotosha ukweli kutoka kwa Allah. Kuhusiana na itikadi ya Wakristo katika kuamini utatu Mtakatifu Sheikh Jalala alisema, hilo ni suala la tofauti za kifalsafa na mitazamo katika madhehebu, lakini ukweli ni kuwa kinachotoka katika vinywa vyao ni neno la Mungu mmoja Allah anasema: “Hakika wamekufuru wale wasemao hakika Mungu ni Isa mwana wa Maryamu …” (Qur’an, 5:72). Kisha Allah akasema: “Hakika wamekufuru wale wasemao hakika Allah ni wa tatu katika utatu…” (5:73) Sasa vipi huyu Shia kudai kwamba tofauti kati ya Uislamu na Ukrsito ni tofauti za kifalsafa na mitazamo ya kimadhehebu tu? Aya hizi na nyingine nyingi hazioni?
Ina maana Ukristo, Uyahudi na Uislamu ni madhehebu tu za dini moja? Kauli kama hizi ni kupingana wazi wazi na Allah Ta’ala kwa malengo ya kuwafurahisha Wakristo waliohudhuria semina hiyo ambapo kwa mujibu wa mmoja wa Maprofesa aliyekuweko siku hiyo, alidai sasa ameuelewa Uislamu. Waislamu tujihadhari na upotoshaji wa aina hii kwani hawa hawana tofauti na yule ‘Bwana’ aliyedai siku za hivi karibuni akiwa kanisani kwamba huu ni wakati wa Injili na mkombozi wa ulimwengu ni Yesu.