YA KIKWETE YAMKUMBA MAGUFULI,SOMA HAPO KUJUA
HOJA nzito, uchunguzi na ufuatiliaji wa vyama vya
upinzani uliokuwa unatesa utawala wa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete, sasa
zinaelekezwa kwa Rais John Magufuli, anaandika Faki Sosi.
Rais Magufuli anakumbana na
mtikisiko kutoka vyama vya upinzani ambapo sasa anakosolewa kutokana na
kushindwa kutenganisha majukumu ya mihimili miwili –Bunge na Serikali-hivyo
kusababisha sintofahamu.
Hatua
anazochukua ikiwa ni pamoja na kuhamisha matumizi ya fedha jambo ambalo
linatajwa kuingilia muhimili mwingine wa Taifa kinyume na taratibu za nchi.
Mjini
Dodoma kabla ya kususa Hotuba ya Kasim Majaliwa, Waziri Mkuu; Freeman Mbowe,
Kiongozi wa Upinzani Bungeni amesema utawala wa sasa unavunja Katiba ya Jamhuri.
Mbowe
ambaye pia ni Msemaji Mkuu wa Kambi rasmi ya Upinzani Bungeni katika Ofisi ya
Waziri Mkuu amesema, “kitendo cha serikali kuamua kufanya re-allocation ya
bajeti bila kupata idhini ya Bunge ni dharau kwa bunge lakini mbaya zaidi ni
uvunjaji wa Katiba na Sheria.”
Amefafanua
kwamba, ni Bunge la Bajeti kwa mujibu wa ibara ya 63(3)(b) ya Katiba ya Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania ndio lililo na mamlaka ya kujadili utekelezaji wa kila
wizara wakati wa Mkutano wa Bunge wa kila mwaka wa Bajeti ikiwa ni kujadili na
kuidhinisha Bajeti ya Serikali.
“Ikiwa
fedha zilizoidhinishwa na Bunge hazikutosha kutekeleza majukumu ya serikali,
kifungu cha 41(1) cha Sheria ya Bajeti ya Mwaka 2015 kinaelekeza kwamba:
“Serikali
itawasilisha Bungeni kwa idhini, bajeti ya nyongeza ya fedha zilizotumika
ambazo zimezidi kiwango kilichoidhinishwa na Bunge au kwa madhumuni ya
kugharamia mahitaji ambayo hayakupangwa.”
Amefafanua
kwamba, utaratibu huo unatiliwa nguvu na Sheria ya Fedha za Umma ya mwaka 2001
ambapo kifungu cha 18 (3) na (4) kinaitaka serikali kupeleka bungeni bajeti ya
nyongeza kwa ajili ya kupata idhini ya Bunge ikiwa fedha zilizoidhinishwa awali
hazikutosha.
Lakini
utaratibu huo umekuwa ukivunjwa na Serikali ya Rais Magufuli kutokana na
kufanya matumizi ya fedha ambazo hazikuidhinishwa na Bunge na kwamba, jambo
hilo linaua dhana ya madaraka ya Bunge ya kuisimamia na kuishauri serikali.
Ametoa
mfano kwamba, bajeti ya maendeleo iliyokuwa imeidhinishwa na Bunge kwa Wizara
ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kwa mwaka wa fedha 2015/16 ilikuwa ni Sh.
883.8 bilioni ambapo kati ya fedha hizo, fedha za ndani zilikuwa ni Sh. 191.6
bilioni.
“Jambo
la kushangaza ni kwamba, hadi kufikia mwezi Machi 2016 wizara ilikuwa
imeshapokea kutoka hazina shilingi bilioni 607.4 ikiwa ni fedha za ndani.
“Ukitazama
takwimu hizo, utaona kuwa kuna ongezeko la fedha zilizotolewa na hazina hadi
kufikia mwezi Machi 2016 ukilinganisha na fedha zilizoidhinishwa na Bunge,”
amesema Mbowe.
Amesema
tangu kuidhinishwa kwa bajeti ya Wizara ya Ujenzi, hakuna bajeti ya nyongeza
iliyopelekwa bungeni na serikali ili kupata idhini kutokana na matakwa ya
Sheria ya Bajeti ya 2015 au sheria ya Fedha ya 2015.
Hivi
karibuni Rais Magufuli amekuwa akibadili matumizi ya fedha zilizopangwa na
bunge kwa ajili ya shughuli fulani na kuzipeleka kwenye kazi nyingine kinyume
na utaratibu wa nchi.
Miongoni
mwayo ni fedha za Sherehe za Muungano ambazo sasa zimeelekezwa kwenye upanuzi
wa Barabara ya Makongoro – Uwanja wa Ndege wa Mwanza kuanzia eneo la Ghana.
Fedha
za Sherehe ya Uhuru ziliamriwa kuelekezwa kwenye upanuzi wa Barabara ya kutoka
Mwenge kwenda Moroco jijini Dar es Salaam ambapo upanuzi huo unaendelea.
Hakuna maoni
Chapisha Maoni