Zinazobamba

WEZI WA ESCROW WAZIDI KUJICHANGANYA MAADILI,BOSI TCAA AJIINGIZA MKENGE,SOMA HAPA KUJUA


Mkurugenzi wa Idara ya Udhibiti masuala ya Kiuchumi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania (TCAA), Dk. James Diu

MKURUGENZI wa Idara ya Udhibiti masuala ya Kiuchumi wa Mamlaka ya Usafiri wa Anga Tanzania(TCAA), Dk. James Diu, amekiri kupokea kiasi cha sh. milioni 80.8 kutoka kwa James Rugemalira, lakini “akajikoroga” kuhusu matumizi halisi ya fedha hizo. Anaandika Mwandishi wetu…(endelea).
Hatua hiyo ni baada ya Dk. Diu ambaye pia aliwahi kuwa Meneja Udhibiti Uchumi katika Mamlaka ya Udhibiti wa Nishati na Maji (EWURA), kudai kuwa alitumia fedha hizo kwa ajili ya matibabu ya mkewe aliyefariki dunia Agosti mwaka jana, kwa ugonjwa wa saratani.
        Maelezo yake yanatofautiana na yale aliyoyatoa mbele ya Kamati ya Uchunguzi ya Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma na tamko lake la mali na madeni la Desemba 30, mwaka jana, linalobainisha kuwa alitumia fedha hizokulipia deni lake la nyumba alilokuwa akidaiwa.
Kutokana na mkorogano huo mbele ya Baraza la Maadili ya Viongozi wa Umma, Wakili wa Sekrtarieti hiyo, Getrude                    Cyriacus, akihitimisha hoja hiyo, aliomba Dk. Diu ajibu mashtaka na kutoa maelezo zaidi kwa kuwa                 amejichanganya kuhusu matumizi ya fedha hizo.
          Awali, Wakili wa Sekretarieti hiyo, Wemaeli Mtei, amedai kuwa Dk. Diu aliomba na kupokea sh. milioni 80.8 kutoka kampuni ya VIP Engeneering and Marketing Limited kinyume cha Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.
             Amesema pamoja na fedha hizo, pia Dk. Diu amejipatia maslahi ya kiuchumi kwa kupokea kiasi cha dola za Marekani 25,000 kutoka kampuni ya Mabibo Beers, Wine and Spirit mali ya Rugemalira, kinyume cha Sheria hiyo ya maadili.
               Katika hati hiyo ya mashtaka, pia Dk. Diu anadaiwa kupokea dola za Marekani 10,100 kutoka Kampuni ya Prime Fuel Tanzania limited ambazo zote hakuzitamka kama Sheria hiyo ya maadili inavyotaka.
Kwamba, mlalamikiwa ambaye amewahi kufanyakazi EWURA inayoshughulika na masuala ya nishati, alijipatia kiasi hicho cha fedha kutoka kampuni ya VIP yenye hisa asilimia 30 katika kampuni ya IPTL yenye mkataba wa umeme na Tanesco, jambo linalosababisha mgongano wa kimaslahi.
             Shahidi wa Sekteratieti hiyo, Zahara Guga, amesema kitendo cha mlalakiwa kuwa na historia ya kufanya kazi EWURA na kupokea fedha kutoka kampuni ya VIP ambayo inasimamiwa na mamlaka hiyo ni kinyume na Sheria ya maadili na pia ni mgongano wa kimaslahi.
Ameongeza kuwa katika uchunguzi walibaini kuwa Dk. Diu alifungua akaunti Februari 4, mwaka jana katika Benki ya Mkombozi tawi la Kariakoo na kuingiziwa sh. milioni 80.8 Februari 5, mwaka huo na kampuni ya VIP.
           Katika utetezi wake, Dk Diu, alikanusha kuomba fedha hizo kwa Rugemalira na kukiri kuwa alipokea kiasi hicho ambacho alipatiwa kama ahadi ya kumsaidia katika matibabu ya mkewe ikiwa ni pamoja na kumsafirisha kwenda India kwa matibabu zaidi.
“Rugemalira  ni rafiki yangu wa karibu pamoja na familia yangu, lakini pia nimesoma naye shahada yangu ya kwanza Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, mwaka 1982 hadi 1985, alinipatia fedha hizo kama ahadi sijamuomba, kudai wala kupokea maslahi ya kiuchumi kutoka kwake,” alijitetea.
         Alisema kutokana na hali mbaya aliyokuwa nayo mkewe, Rugemalira alikwenda kumjulia hali alipolazwa hospitali ya TMJ na baadaye Sanitarius iliyopo Mikocheni, ndipo aliahidi kutoa fedha hiyo kama mchango na msaada wa matibabu na baadaye mazishi baada ya mkewe kufariki.
          Ameendelea kujitetea kuwa hata katika fomu yake ya tamko la mali na madeni kwa sekretarieti hiyo, aliyoiwasilisha Februari 30, mwaka jana, alizitamka fedha hizo kuwa amezipokea kutoka kwa Rugemalira. “Awali sikuona umuhimu wa kuiwasilisha kwa ofisa masuhuli wangu kwa sababu haikuwa zawadi na sikuona umuhimu wa kufanya hivyo,”alidai.
Aidha alisisitiza kuwa kupokea kwake fedha hizo hakuna mgongano wowote wa kimaslahi kwa kuwa hana uhusiano wowote wa kibiashara na Rugmalira na hata kazi yake katika mamlaka ya TCAA haina uhusiano na kampuni za Rugemalira kibishara.
            Utetezi wake, ulionekana kulikanganya baraza hilo, ambapo wakili wa Sekrtarieti hiyo, Getrude Cyriacus, alibainisha kuwa Dk. Diu alijitetea kuwa fedha hizo alizitumia kulipia deni la nyumba alilokuwa akidaiwa.
“Hata katika tamko la mali na madeni aliloliwasilisha mwaka 2012, aliandika maelezo kuwa anadaiwa sh. milioni 80 za nyumba ambayo haijakamilika aliyonunua huko Mbezi kwa Godson Shangwe, na tamko lake la mwaka jana alibainiha kuwa ametumia fedha hizo alizopewa na Rugemalira kumalizia deni hilo,” alisema Cyriacus.
Dk. Diu alipobanwa, alijitetea kuwa ni kweli alitumia sh. milioni 80.8 kulipia deni hilo la nyumba kutoka kwa                         Rugemalira lakini fedha hizo si hizo zinazodaiwa na Sekretarieti bali ni nyingine.

         Mwenyekiti wa baraza hilo, Jaji Hamis Msumi, amesema kuwa wamesikiliza shauri hilo na litatoa uamuzi wake na mapendekezo kwa mamlaka husika.
Chanzo ni mwanahalisi.online

Hakuna maoni