Je unajua nini kuhusu bidhaa zenye nembo ya halal?
Na
Selemani Magali, Dar es Salam
Je unajua
nini kuhusu bidhaa zenye nembo ya halal? Mkuu wa Kitengo cha Halal cha Baraza
Kuu la Waislamu Tanzania, (Chief Halal), Mohammed Juma ambaye pia ni Imam Mkuu
wa Msikiti wa Idrisa anakusaidia kuelewa suala hili muhimu kupitia mahojiano
aliyofanyiwa na mwandishi wetu, Selemani Magali.
Swali: Nini faida ya huduma ya halal
katika jamii na taifa kwa ujumla wake?
Halal Chief: Halal ina faida nyingi. Faida ya
kwanza ni kuhakikisha watu wanatumia bidhaa zilizo halal, kwa mujibu wa sheria
ya Kiislamu. Lakini, kwa upande mwingine halal inasaidia kuhamasisha biashara
ya kimataifa. Nchi kama Austalia na Brazil
ambayo ni ya Kikristo, wamelipa kipaumbele suala la halal na matokeo yake
wanauza nyama nyingi katika nchi za Mashariki ya Kati, hususan Saudi Arabia,
Abudhabi, Oman na India.
Ukilingansha
umbali wa kuelekea Mashariki ya Kati kutokea Australia/Brazil na kutokea Afrika Mashariki, unaona wazi kuwa
Afrika ya Mashariki ipo karibu zaidi na Mashariki ya Kati. Sasa, kwa nini
wenzetu wamelishika soko la nyama? Ni kwa sababu ya nyama zao zimethibitishwa
na nembo ya halal kimataifa.
Hata
kiubora, nyama kutoka ukanda wa Afrika Mashariki ni bora zaidi (more natural)
kwa sababu wanyama wetu wanakula nyasi tu. Pia wanyama wa ukanda huu
hawakabiliwi na maradhi mengi, na hivyo basi sisi tungepaswa tupate soko kubwa
huko.
Swali: Ipoje hali ya ‘halal’ hapa
nchini?
Halal Chief: Hali ni mbaya sana sababu watu
wengi hawana ufahamu wa jambo hili na hivyo wengi wanakula na kunywa bila
kuangalia uhalali wa wanachokula. Licha ya kwamba, watengenezaji bidhaa
huandika taarifa kuhusu bidhaa husika, hakuna anayejali na kujitahidi kusoma
ili kujua bidhaa husika imetengenezwa na nini.
Katika
kutatua tatizo hilo, mwaka 2016 ilianzishwa taasisi ya Tanzania Halal
Certification (THC) ili kufanya kazi ya kuthibitisha bidhaa wakishirikiana na
Baraza Kuu la Waislamu Tanzania (BAKWATA).
Taasisi hiyo iliyodumu kwa mwaka mmoja, ikafa. Baadae ilikuja taasisi
nyingine iitwayo Tanzania Halal Certification (Tan HAC) ambayo nayo ilikufa.
Ndipo mwaka 2019, taasisi nyingine ya Mico international Halal Bureau (MIHB)
ilizaliwa kuhuisha huduma ya halal hapa Tanzania.
Swali: Kwa nini baadhi ya taaisi
zilizoundwa hazikufikia malengo yaliyokusudiwa?
Chief Halal: Bahati nzuri nilikuwepo katika
taasisi zote hizo kama kiongozi. Changamoto zilizokuwepo ni pamoja na viongozi
kuingiliana majukumu ambapo unakuta chief halal kwa kutumia misingi ya dini
anasema hili, lakini wenye taasisi wanasema vile. Hivyo, kulikosekana maamuzi
yenye tija na afya kwa jamii na kwa sababu hiyo, mimi na wenzangu tuliondoka na tukahamia huku ambako
wanaheshimu misingi ya dini.
Changamoto
nyingine ilikuwa ni maslahi. Huduma ya halal ina pande mbili, kiimani na
biashara. Hatukupata ushirikiano mzuri kutoka kwa masheikh, hasa wa ngazi za
wilaya na kata ambao walihoji watafaidika vipi na mpango huo? Ikumbukwe,
machinjio yote yapo chini ya Bakwata na hivyo masheikh wa maeneo husika hupata
kiasi cha mapato. Ujio wa halal haukubainisha maslahi hayo ya masheikh. Hili
linaungana na changamoto ya ukosefu wa rasilimali fedha.
Swali: Vipi kuhusu changamoto
kimataifa?
Kimataifa,
changamoto ilikuwa ni ukosefu wa utambulisho wa Shirika la Kidunia
linaloshughulikia mambo ya halal (JAKIMS). Mpaka sasa taifa halijapata kibali
cha kutambuliwa na JAKIMS kwa hiyo hata tukiweka alama zetu za halal
hazitambuliki nje ya mipaka ya Tanznaia.
Tukiweza
kuwashawishi wenzetu wa JAKIMS kuitambua Tanzania, tutapata fursa ya kupeleka
bidhaa zetu, hususan nyama, nje ya nchi. Kikwazo kikubwa cha kupata kibali
hicho, tangu enzi za THC imekuwa ni ukosefu wa wataalamu waliopitia mafunzo ya
JAKIMS. Taasisi hiyo inataka wataalamu watakaofanya kazi ya halal wawe
wamefundishwa na watu wao.
Wenzetu
Kenya walitumia muda mrefu sana kujenga halal lakini walipiga hatua kubwa baada ya kujiunga na
shirikisho la JAKIMS. Sisi pia tumeanza
michakato ya kujiunga na taasisi ya JAKIMS. Zoezi hili limefikia hatua nzuri na
haitachukua muda mrefu watatupatia cheti. Ikumbukwe, JAKIMS ni shirika kubwa
lenye nchi wanachama zaidi ya 46, zikiwemo za Kikristo na Kiislamu na pia kuna
mashirika zaidi ya 60 yaliyosajiliwa – hivyo wana mtandao mkubwa.
Hapa juzi,
serikali ilitoa miezi mitatu kwa wadau wa nyama kufuatilia kwa nini tunashindwa
kuuza nyama nje, ilhali tuna nyama nyingi na tuna watu wa TBS na TFDA ambao
wanathibitisha ubora. Mtaalamu kutoka soko la nyama Dodoma alisema, tatizo
kubwa ni kutotambuliwa na JAKIMS, kwa hiyo tukipeleka nyama hazichukuliwi.
JAKIMS wao wanasoko kubwa la nyama.
Waislamu
na wasio Waislamu, ikiwemo wazungu, wanaliamini shirikisho hilo kwa sababu wana
weledi zaidi zaidi ukilinganisha na mashirika mengine kiasi kwamba, hata kama
mashirikisho mengine yamekagua, bado wao wanaweza kugundua tatizo. Kwa hiyo,
kitu kikipitishwa na JAKIMS kinaaminika. Katika JAKIMS, wanaotoa cheti ya halal
ni watu wengine, wanaokagua ni wengine, na kuna bodi inayofanya maamuzi na
hivyo basi suala la rushwa halina nafasi
kabisa.
Swali: Inaonekana una matumaini sana
na Mico. Mmejipangaje?
Halal
inapaswa kuangaliwa kwa undani upana, kuanzia uzalishaji, usafirishaji na
uuzaji. Wengi wanadhani suala hilo lipo kwenye kuchinja tu kumbe sio kweli bali
linaanzia mbali. Unaweza kuona watu
wamechinja kama inavyotakiwa lakini nyama hiyo ikabaki kuwa ni haramu kwa
sababu huenda chakula alicholishwa mnyama kilikuwa ni haramu.
Wakaguzi
wetu wa Mico Interanational Halal Bureau watafanya kazi kwa kuangalia mnyororo
mzima wa halal: kuanzia chakula anachokula mnyama, hadi nyama inapouzwa kwa
mlaji. Tukigundua kuna changamoto, hatuwezi kukupa nembo yetu ya halal.
Jambo hili
ni zito na linalohitaji uungwaji mkono wa wadau mbalimbali. Kufikia malengo
hayo, tumejipanga kuhakikisha tunapata uungwaji mkono wa wadau na taasisi zingine. Kuna mipango
inafanyiwa kazi, si muda mrefu watu watapata taarifa kuwa tupo na tumekuja
kivingine.
Taasisi
yetu pia inaamini katika nguvu ya elimu. Watu wakielewa dhana hii ya halal,
kila kitu kinawezekana. Kwa hiyo, ni
muhimu ni kutoa elimu ya halal ili watu waelewe kuwa halal si kwenye kuchinja
peke yake bali mnyororo mzima.
Tumejipanga
baada ya kutoa mafunzo hayo tuwape vyeti maalum wachinjaji hao ili kuwatambua
(recognition). Pia, tutatambua machinjio na magari yao kwa kuyapa nembo maalum
kuonyesha kuwa wanajua wanachokifanya. Pia, tunajipanga elimu kwa wauzaji,
ambao ni wadau muhimu katika hili. Wakielewa, watakuwa msaada mkubwa wa
kuwalisha jamii nyama ambayo haina shub’ha.
Jambo
jingine ni kujenga hamasa miongoni mwa jamii sambamba na kushirikiana na wadau
wote walio katika mnyororo wa halal. Tunaamini ukiwakamata wadau muhimu katika
mnyororo wa usambazaji, mlaji atakula kilicho cha halal. Pia, ningeandaa
takwimu za wadau waliopo katika sekta. Yote haya yatawezekana kama jamii
itaelewa kuhusu kazi hii nzito.
Swali: Nchi nyingine duniani ambako
wamefanikiwa, walifanyaje?
Chief Halal: Wenzetu huko duniani wamekuwa na
uelewa mkubwa juu ya halal. Hawatumii vitu ambavyo havina nembo ya halal.
Malaysia, kwa mfano, kuna idara maalumu ya serikali ndio inafanya kazi hii ya
halal ikiingizia serikali mapato makubwa. Wafanyakazi wa idara hiyo wanalipwa vizuri
…unaweza kufananisha na mishahara ya Benki Kuu ya Tanzania (BOT). Halal ni
jambo kubwa sana katika nchi za wenzetu.
Hapa
Tanzania, tunapaswa kuangalia mifumo yetu ili kuifanya sekta hii ikue kwa
haraka kwa kila mmoja kutimiza wajibu wake.
Swali: Changamoto gani mnakumbana
nazo katika utekelezaji wa majukumu yenu?
Chief Halal: Moja ya changamoto ni rushwa. Kwa
mfano, kampuni moja ya chakula iliyopo Ubungo (jina tunalihifadhi) waliomba
kupatiwa hati ya halal, lakini nilipoenda kukagua walikataa kunifungulia
makontena mawili. Nilipouliza kwa nini, walisema zimefungwa na TFDA, lakini
TFDA nao walikana. Walisema ingekuwa wao, kungekuwa na nembo (seal) za TFDA.
Niliandika
taarifa yangu na suala hilo lilipofikishwa katika shura ya viongozi nao
walilikataa. Hata hivyo, suala hilo lilipitishwa na wenye taasisi bila ya
wengine kujua; nami ndipo nikaamua kuondoka. Siwezi kubeba dhima ya kulisha
watu haramu kwa maamuzi yaliyofanywa na mtu ambaye hajui athari ya jambo
lenyewe.
Pia,
tuligundua kampuni moja ya kutengeneza soseji (jina tunalihifadhi) kwa
kuchanganya na nyama ya nguruwe. Tuliandika taarifa yetu lakini hakukuwa na
hatua zilizochukuliwa. Katibu Mkuu wa BAKWATA wa miaka hiyo aliahidi kuzungumza
suala hilo kwenye Baraza la Idd lakini hakufanya hivyo, na sababu
haikufahamika.
Soseji
hizi zinatumika sehemu mbalimbali. Tulipowauliza wauzaji wakasema kwamba, watu
wenyewe ndio wanataka bidhaa hiyo. Zipo soseji za aina mbili: za ng’ombe na za
nguruwe, lakini jambo la ajabu ni kwamba, hata Waislamu wanaagiza zile
zilizochanganywa na nguruwe.
Vilevile,
tulishuhudia ugomvi mkubwa katika baadhi ya mikoa hadi kufikia watu kupigana
kwa sababu ya kutembelewa na watu wa halal. Ukinzani huo ulionekana katika
machinjio makubwa matano hapa nchini (The big five slaughter house in
Tanzania): Dodoma, Rukwa, Mwanza, Singida na Tanga.
Swali: mmeanza safari ya kutoa
huduma hii ya halal hapa Tanzania, mpango wenu ukoje kuhakikisha mnafanikiwa?
Halal
chief: Kwanza, sisi wenyewe tumehakikisha tunatambua umuhimu wa halal. Baada ya
hapo, tumeanza kuongeza ufahamu wa wadau juu ya umuhimu wa jambo hili, kwa
kushirikiana na mamlaka na taasisi nyingine. Kisha mengine yataendelea.
Soko la
halal ni pana na sisi tunataka tuwe kichocheo cha kutengeneza fursa za kuingiza
fedha kwa wengine na kutengeneza ajira. Tunaamini halal ikisimama, hata nchi
itafaidika.
Hakuna maoni
Chapisha Maoni