WAZIRI MKUU ATAKA WAZAZI WA MWANAFUNZI ATAKAYEPEWA MIMBA AFUNGWE JELA MIAKA 30,SOMA HAPO KUJUA
Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, amesema serikali
itatoa adhabu kali ya kifungo cha miaka 30 jela kwa wazazi wote wawili wa mtoto
wa kike atakayekatishwa masomo na kulazimishwa kuolewa ama akipata ujauzito.
Aidha amesema Serikali itamfunga jela miaka 30
kijana anayetaka kumuoa msichana anayesoma pamoja na wazazi wake.
Amesema Serikali ya awamu ya tano imedhamiria
kumlinda mtoto wa kike katika kuhakikisha kuwa anapata haki yake ya msingi ya
kusoma kufikia elimu ya chuo kikuu kwa kujenga mabweni na kuwachukulia hatua
kali za kisheria watu watakaowapa mimba na kuwaozesha katika umri mdogo na
kukatisha masomo yao.
Majaliwa aliyasema hayo jana wilayani Hanang, mkoani
Manyara katika ziara yake ya kikazi ya siku sita kwa mkoa huo.
Alisisitiza kuwa kupitia sera ya kuboresha elimu
nchini serikali imeondoa michango ya fedha za kulipia bili za maji, umeme,
gharama za mlinzi na mitihani ili kumpunguzia gharama mzazi na mlezi na
kuwaacha wazazi kushughulikia maeneo mengine muhimu kwa mtoto wao.
Alisema tayari kwa mwaka huu wa fedha, walimu 4,396
wa masomo ya sayansi wameajiriwa ambapo alisisitiza kuwa wazazi na walezi
wanalo jukumu kubwa la kusimamia maendeleo ya shule ya watoto wao kwa lengo la
kupandisha ufaulu wa elimu kwa wilaya,mkoa na taifa.
“Mtoto akiwa mtoro baba na mama wa mtoto huyo
atashitakiwa,mtoto wa kike asiguswe,vijana waendesha bodaboda acheni kuwalaghai
watoto hao kwa zawadi na usafiri, tutawasaka wote,” alisisitiza.
Akizungumza na watumishi wa umma katika halmashauri
ya wilaya hiyo, aliwataka watumishi hao kujivunia serikali yao kwa kuienzi
katika kufanya kazi kwa nidhamu katika kuwatumikia wananchi bila kujali uwezo
wao, kabila wala rangi zao kwa kuwa wamepewa dhamana ya kusikiliza kero zao.
Majaliwa alifafanua kuwa wafanyakazi wana wajibu wa
kuwatumikia watanzania kwa kuwa wao ni waajiriwa wa serikali hivyo ni muhimu
wakatoka maofisini na kwenda vijijini kusikiliza kero na kuzitatua badala ya
wananchi kungojea viongozi wa kitaifa kuja kusikiliza kero na malalamiko yao
wakati wao ni watendaji wakuu katika maeneo yao.
“Utumishi wenu hauhitaji upendeleo ama ahadi za njoo
kesho, utumishi wa awamu ya tano ni wa uwajibikaji zaidi na uwajibikaji ni
pamoja na kuwa mwaminifu katika kulinda na kusimamia kikamilifu fedha za
serikali zinazotengwa katika halmashauri husika kwa ajili ya maendeleo,”
alisema.
Akizungumzia soko la kimataifa la Endagaw,
aliwapongeza wananchi wa wilaya hiyo kwa kukubaliwa kujengewa soko kubwa la
kimataifa ambako wakulima watapeleka mazao yao na kuyauza lakini pia wataweza
kuingiza mapato kwa kukodisha makampuni makubwa yanayohitaji kukodi kuhifadhi
mazao kama NRFA.
Aliwataka wakulima wa mazao mbalimbali wilayani
Kateshi kulitumia soko la mazao la kimataifa la Endagaw lililojengwa na ofisi
yake kuuza mazao yao kwa bei nzuri badala ya kuuza mazao majumbani ambako
wamekuwa wakiuza kwa bei ya chini isiyowasaidia kukuza kipato chao.
Alieleza kuwa serikali itaendelea kjuimarisha
miundombinu ya soko hilo kwa kujenga eneo la wazi la nje kudhibiti magari
makubwa yanayoshusha na kupakia mizigo yasikwame kutokana na matope na kuwa na
mizani ya kupimia mazao na magari.
Kuhusu kero ya maji katika mji wa Katesh, alisema
marekebisho yanafanyika kurekebisha mashine ya kuvuta maji na kuhakikisha sera
ya maji inatekelezwa kwa vitendo katika kumpatia maji kila mwananchi umbali
usiozidi mita 400.
Awali katika taarifa yake Mkuu wa Wilaya ya Hanang,
Sara Msafiri alimweleza Waziri Mkuu kuwa changamoto kubwa inayoikabili wilaya
hiyo ni migogoro ya ardhi, kuanzisha gereza la wilaya kupunguza usumbufu wa
kuwapeleka wahalifu Babati, jambo ambalo alisema atalipeleka wizara ya mambo ya
ndani lipate kushughulikiwa.
Msafiri aliomba pia kujengewa mahakama ya wilaya
ambapo alisema ni mchakato uliopo wa mahakama kuu kujenga mahakama katika ngazi
za wilaya hivyo jambo hilo nalo litashughulikiwa.
Mbunge wa Viti Maalum Mkoa, Ester Mahawe alibainisha
tatizo la kuwa na shule ya kidato cha tano na sita moja kwa wilaya nzima ambapo
alimwomba Waziri Mkuu kutoa kipaumbele katika bajeti zake za elimu ili shule
zaidi zijengwe mkoani humo.
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Manyara, Rose Kamili
(Chadema) aliiomba serikali kufuatilia na kuyatolea maamuzi mashamba makubwa
ambayo yamekuwa hayaendelezwi na wawekezaji kutoka Ngano Ltd wanayoyamiliki
zaidi ya ekari elfu 45 ambapo wamekuwa wakilima ekari elfu 16 pekee na kuacha
migogoro ya ardhi baina yao na wananchi na kukosesha mapato ya halmashauri.
Ziara hiyo ilipata baraka za mvua kubwa baada ya
ukame wa muda mrefu ilishangiliwa na umati wa watu waliokuwa wakiimba kwa
furaha kuashiria Waziri Mkuu kuja na baraka hiyo kuneemesha mazao yao.
Leo Waziri Mkuu anatarajiwa kuhitimisha ziara yake
wilayani Babati ambapo pamoja na mambo mengine atafanya majumuisho ya ziara
hiyo na kutoa maelekezo ya serikali kwa wananchi na viongozi ngazi ya mkoa.