MWAKYEMBE AONYWA TENA,NI KUHUSU KUINGILIA CHAMA TLS,SOMA HAPO KUJUA
Chama cha Wanasheria Afrika Mashariki (EALS)
kimemwandikia barua Waziri wa Katiba na Sheria, Dkt. Harrison Mwakyembe
kikimtaka aache kuingilia uchaguzi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS).
Barua hiyo imekuja baada ya Dkt. Mwakyembe kudaiwa
hivi karibuni kutishia kuifuta TLS kwa madai kwamba imeanza kuingiliwa kisiasa.
Barua hiyo iliyoandikwa na kusainiwa na Rais wa
EALS, Richard Mugisha, inasema TLS si chama cha kisiasa na kimeanzishwa kwa
kufuata sheria zote.
“Mheshimiwa Waziri, tumesikitishwa na taarifa ambazo
zimeenea kwenye vyombo vyote vya habari na gazeti la East African la Februari
18 ambalo limekunukuu ukisema kwamba Chama cha Wanasheria wa Tanganyika (TLS)
kina muingiliano wa kisiasa,” inasema sehemu ya barua hiyo.
Katika barua hiyo, Mugisha anasema wanasheria
wanatakiwa wapewe uhuru, wasiingiliwe na serikali kama ilivyo kwa nchi nyingine
kwani kuingilia ni sawa na kuvunja sheria za nchi.
Rais wa sasa wa TLS, John Seka amesema kuwa chama
chake kimefurahishwa na barua hiyo kwa Waziri na kwamba nao pia wanafanya
taratibu kumuona ili kujadili mustakabali wa chama hicho.
Alisema kuwa TLS inaendelea na mchakato wa uchaguzi
kama ulivyopangwa na kuwataka wagombea wote kujiandaa kwa uchaguzi huo ambao
alisema ni halali.
Uchaguzi wa chama hicho unatarajiwa kufanyika machi
18 mwaka huu, huku wagombea kutoka vyama vya upinzani wakiwa wamejitokeza
kuwania nafasi ya uongozi wa juu.