SERIKALI ITENGE BAJETI MAALUM KWA AJIRI YA CEmONC-UTEPE MWEUPE
![]() |
| Meneja mipango wa muungano wa utepe Mweupe wa uzazi salama Sizarina Hamisi akiwasilisha mada kwa waandishi wa habari |
Imetosha! Ndivyo unavyoweza kusema ukisikiliza kwa makini
Takwimu za vifo vinavyotokana na uzazi. Kila siku Nchini Tanzania kuna wanawake
24 wanapoteza maisha, Zaidi ya watoto 144 hufariki lakini pia kama hiyo
haitoshi Takwimu zinaonyesha kila mwanamke mmoja anapofariki huacha wenzake 30
wakipata ulemavu wa kudumu kama vile fistula au miguu kupooza.
Takwimu zinaendelea kuonyesha kwa mwaka Tanzania inapoteza
wanawake 8,000, watoto 48,000 na kunatengeneza walemavu wa kudumu wapatao
240,000.
Ukipiga jumla yake hapo utagundua kwa kila mwaka Tanzania
inapoteza nguvu kazi wapatao 296,000, nilikuwa najaribu kujiuliza hapa, ni kwa
nini hasa?.
Hivi hatujachoka kupoteza nguvu kazi hii, wahusika wanaliona
hili? Na Nini kifanyike. Kwa kweli neno kwa
nini hasa limekuwa lefu. Ni mnyororo unaoanzia mbali kushuka hadi ngazi ya
kata.
Mapema hii leo Fullhabari. Blog ilipata bahati ya kuzungumza
na Mratibu wa Kitaifa wa White Ribon Alliance Bi.Rose Mlay kuhusu suala la vifo
vya mama na mtoto wakati wa kujifungua, nikataka hasa kufahamu njia zinazoweza kuondokana
tatizo hilo linalotia aibu Taifa letu.
Akizungumzia Suala hilo,Bi.
Mlay amesema kabla ya kuangalia
suluhisho la tatizo hilo, Jamii pamoja na Serikali yetu inapaswa kukubali kwa
vitendo kuwa vifo vya uzazi havikubaliki, kuanzia hapo tuanze kuzichambua
sababu za vifo hivyo na kwa nini hasa zipo.
Ameongeza kusema Taifa likiamua kulifanya suala hilo kuwa
ajenda, hakuna kitakachoshindikana kwani ni suala ambalo linahitaji msukumo wa kisiasa
kuliondoa.
Amesema, ukiangalia ukubwa wa tatizo ni dhahili kuna haja
viongozi kukaa chini kuangalia ni kwa jinsi gani wanaweza kuleta msukumo wa
kisiasa kama ilivyoweza kufanya katika sekta zingine za Elimu ambako
kumeonekana mafanikio makubwa ya madawati.
Amesema ieleweke kuwa watoto wote wanapaswa kulindwa tokea
wakiwa tumboni, na kwamba kama Taifa likiamua kufanya kampeni ya kutokomeza vifo
vinavyotokana na uzazi inawezekana.
“Tuone aibu kwa taifa kama la Tanzania kuwa nchi ya pili kwa
idadi ya watu wanaokufa kutokana na uzazi
katika ukanda wa Afrika Mashariki” Nchi zingine kitendo cha kufa mama anayejifungua
ni suala la aibu na wahusika lazima wachukuliwe hatua. Alisema Mlay.
![]() |
| Sehemu ya waandishi wa habari wakifuatilia mada. |
Aidha Mlay amesema Mbali na Msukumo wa Kisiasa, lakini jambo
kubwa ni kuongeza na kuilinda bajeti ya huduma kamili za dharura za uzazi
salama (CEmONC)
Akifafanua kuhusu CEmONC, Mlay amesema huo ndio muarobaini wa
vifo vinavyotokana na uzazi, kwa sababu vifo vingi vinahitaji huduma za dharura
ambazo bajeti yake inatakiwa kuandaliwa mapema.
Amesema asilimia 70 ya vifo vya akina mama na watoto wachanga
wakati wa kujifungua vinasababishwa na sababu kuu tano; ambazo ni Kuvuja
damu,Kifafa cha mimba, Maambukizi baada ya kujifungua,kutoka kwa mimba pamoja
na uchungu pingamizi. Hivyo kunahaja ya kuandaa bajeti maalum kukidhi mahitaji
hayo.
Mlay anasema kwa muda mrefu bajeti inayotengwa kwa wizara ya
afya imekuwa na mambo mengi ya kufanya, ili kukabiliana na vifo hivyo hakuna
budi Serikali kupitia Wizara ya fedha na mipango kupanga bajeti maalum kwa
ajili ya CEmoNC.


