Zinazobamba

MAREKANI YAMWOGOPESHA MAGUFULI,AAMUA KUMUITA MAALIM SEIF IKULU,SOMA HAPO KUJUA


MAALIM Seif Shariff Hamad ambaye anapigania haki yake ya kutangazwa mshindi wa uchaguzi mkuu wa Zanzibar baada ya uchaguzi huo kufutwa kihujuma, amekutana na Rais John Magufuli leo Ikulu jijini Dar es Salaam. Anaandika Jabir Idrissa … (endelea).
Ni mkutano wa faragha uliomhusisha pia Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ambaye Dk. Magufuli aliahidi kushirikiana naye pamoja na Dk. Ali Mohamed Shein kutatua mgogoro wa kisiasa Zanzibar.
Maalim Seif amekuwa akishiriki vikao vya faragha na viongozi wastaafu wa Zanzibar, pamoja na Dk. Shein ambaye ameendelea kubaki madarakani licha ya madai kuwa urais wake ulikoma kisheria tangu Novemba 2.
Vikao ambavyo Maalim Seif amekuwa akishiriki pamoja na Dk. Shein, ndani ya Ikulu ya Zanzibar, vimehusisha pia marais wastaafu Ali Hassan Mwinyi, Dk. Salmin Amour Juma na Amani Abeid Karume, ambaye alishirikiana naye kujenga siasa za maridhiano kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Hakuna taarifa iliyotolewa na upande wowote baada ya kikao cha Maalim Seif na Rais Magufuli, lakini mazingira yanaonesha kuwa ni hatua za dhati za kiongozi huyo mpya za kusimamia utatuzi wa mgogoro wa Zanzibar.
Rais Magufuli aliahidi wakati wa kuzindua Bunge la 11 mjini Dodoma kuwa kuna tatizo linapaswa kushughulikiwa Zanzibar na mbali na makamu wake wa rais, Samia, atashirikiana na Dk. Shein.
Mkutano wake na Maalim Seif unafanyika katika wakati ambao wananchi wamekuwa wakisubiri kwa shauku kubwa kujua hatima ya mgogoro uliotokana na hatua ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha kuufuta uchaguzi wa Zanzibar uliofanyika Oktobva 25.
Taarifa yake hiyo imepingwa kwa nyanja mbalimbali, ikianzia na wanasheria wa ndani ya Tanzania, serikali za kimataifa na wananchi, wakisema hakuna mamlaka yoyote ya kisheria yanayompa haki ya kufanya hivyo.
Chama cha Wanasheria wa Zanzibar (ZLS) kimesema Jecha hana mamlaka hayo kwa sheria yoyote wala katiba ya Zanzibar, na anapaswa kufuta tamko lake ili Tume ikamilishe kazi ya kuhakiki kura zilizobakia na kutangaza matokeo yake pamoja na mshindi wa nafasi ya urais.
Alipotoa tangazo la kufuta uchaguzi Oktoba 28, Jecha alikuwa ameshatangaza matokeo ya urais ya majimbo 33, ambayo wawakilishi wake walishapatiwa vyeti vya ushindi pamoja na majimbo mengine yote yaliyobaki. Zanzibar ina majimbo 54 ya uchaguzi.
Maalim Seif na chama chake Chama cha Wananchi (CUF) wanasema Jecha alishinikizwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuufuta uchaguzi baada ya kuthibitisha kuwa kilishapoteza madaraka kwa kushindwa uchaguzi.
CCM imekuwa ikishikilia kuwa Tume itangaze tarehe ya kufanyika uchaguzi mpya, shinikizo ambalo watendaji wa Tume wanasema hawawezi kulifanyia kazi kwa kuwa hawajapatiwa fedha za maandalizi ya uchaguzi huo.
habari hii kwahisani ya Mwanahalisi oline


Hakuna maoni