Zinazobamba

SIKIKA YAILIPUA SERIKALI YA KIKWETE,NI KUHUSU UPUNGUFU WA DAWA,SOMA HAPO KUJUA


Wagonjwa wakisubiri tiba hospitali ya Taifa Muhimbili
Wagonjwa wakisubiri tiba hospitali ya Taifa Muhimbili
SERIKALI imetakiwa kuongeza fedha za kutosha kwa ajili ya vifaa tiba kwa mwaka wa fedha 2015/2016 ili kuhakikisha upatikanaji wa dawa nchini unaongezeka kufikia asilimia 80 kama inavyotarajiwa na Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN). Anaandika Pendo Omary … (endelea).
           Mbali na kuongeza fedha hizo pia serikali kupitia Wizara za Fedha na Afya, inapaswa kuhakikisha fedha zilizotegwa kwa ajili ya dawa muhimu na vifaa tiba zinatolewa kwa wakati ili kupunguza uhaba wa dawa nchini.
       Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Asasi Isiyo ya Kiserikali ya SIKIKA – inayohusika na utetezi wa masuala ya afya nchini.
       Akizungumza na waandishi wa habari Irenei Kiria, Mkurugenzi wa Sikika amesema, “ Wizara ya Afya itoe mwongozo na mikakati inayoeleweka na kuwezekana katika kutumia mapato ya afya ya Halmashauri kwa ajili ya ununuzi wa dawa muhimu na vifaa tiba. Pia miongozo hii iweke wazi mifumo ya uwazi na uwajibikaji”.
        “Kwa takribani miaka minne iliyopita, bajeti ya dawa muhimu za vifaa tiba imekuwa ikishuka na kusababisha ongezeko kubwa la uhaba wa dawa muhimu huku waathirika wakuu wakiwa ni wananchi wa hali ya chini,” amesema Kiria.
        Kiria amesema mahitaji ya dawa muhimu na vifaa tiba yameongezeka kutoka Sh. 188 bilioni  mwaka 2011/2012 hadi Sh. 577 bilioni mwaka 2014/2015 na makadirio ya Sh. 36.2 bilioni kwa mwaka wa fedha 2015/2016.
          Aidha kwa miaka ya fedha 2011/2012 na 2012/2013 kulikuwa na ongezeko kubwa kidogo la bajeti ya dawa muhimu na vifaa tiba ambazo ni Sh. 123.4 bilioni na Sh. 80.5 bilioni ingawa hakukuwa na matokeo chanya ya upatikanaji wa dawa.
           “Makadilio ya bajeti ya mwaka 2015/2016 yameshuka kwa zaidi ya asilimia 48 kutoka katika bajeti ya mwaka uliopita. Cha kujiuliza je hii bajeti inaendana na malengo ya BRN ya kuhakikisha upatikanaji wa dawa muhimu kwa zaidi ya asilimia 80 ifikapo mwaka 2016?,” amehoji Kiria.
        Kuhusu kuchelewa kutolewa fedha, Kiria amesema, hali hiyo inaathiri mfumo mzima wa ununuzi na usambazaji wa dawa.  Kwa mfano, kipindi cha miaka minne iliyopita ukiondoa mwaka wa fedha 2012/2013 ambapo fedha yote iliyoidhinishwa ilitolewa, ni asilimia 78 tu ya wastani wa fedha zinazoidhinishwa ndizo zimekuwa zikitolewa.

          “Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inapanga kutumia mapato mbadala kutoka fedha za uchangiaji (bima ya afya) ili kusaidia bajeti ya dawa muhimu na vifaa tiba. Ni asilimia 20 ya watanzania wamejiunga na mifuko hii. Hivyo mapato yake hayawezi kuziba pengo la bajeti ya dawa katika mwaka wa fedha unaokuja.” Kiria ameongeza.
chanzo ni Mwanahalisi oline

Hakuna maoni