Mazungumzo ya amani kati ya serikali ya DR Congo na kundi la waasi wa M23 huenda yakarejewa
![]() |
| Raisi wa Uganda Yoweri Museven alipokuwa katika mazungumzo na raisi wa DR Congo Jeseph Kabila |
Na Martha Saranga Amini
Mazungumzo ya amani kati ya serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo
na kundi la waasi la M 23 lililoshindwa na jeshi la serikali huenda
yakarejelewa tena jijini Kampala.
Hatua hiyo inajiri baada ya rais Joseph Kabila kukutana na rais Yoweri
Museveni alipositisha kwa muda ziara yake mashariki mwa nchi DRC na
kuelekea mjini Kampala Uganda kwa mazungumzo na raisi wa taifa hilo
Yoweri Kaguta Museveni kuhusu hatma ya mazungumzo ya Kampala baada ya
kusambaratishwa kwa kundi la waasi wa M23.
Mwezi mmoja uliopita vikosi vya serikali ya DRC kwa kusaidiwa na vile
vikosi maalum vya Umoja wa Mataifa vilivyoko mashariki mwa nchi hiyo
walifanikiwa kuwafurusha waasi wa kundi la M23 waliokuwa wakikalia
maeneo mengi ya mashariki ya nchi hiyo.
Kabla ya kuondoka mjini Goma raisi Kabila aliwaomba raia wa eneo hilo
kuwa na subira na serikali yake inajipanga upya kuanza utekelezaji wa
miradi ya maendeleo baada ya kulishinda kundi la M23.
Katika hatua nyingine ndege zisizokuwa na rubani zinaanza kutumika leo
jumanne huko Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokraia ya Congo ili kusaidia
kuimarisha usalama katika mpaka Kwa mara ya kwanza ndege hizo zisizokuwa
na rubani kutoka Italia ndizo zinaanza kufanya uchunguzi na kuimarisha
hali ya utulivu katika eneo la Mashariki mwa DRC.
Hatua ya Umoja wa Mataifa imelenga kufuatilia harakati za makundi ya
uasii katika maeneo ya Kivu, wakati huu kukiwa na taarifa kuhusu raia
kukimbia makazi wakielekea katika mpaka wa DRC na Rwanda.

No comments
Post a Comment