Zinazobamba

KIKONGWE ALIVYOUAWA NA KUCHUNWA NGOZI MOROGORO



 Familia iliyohusika kumsaka kikongwe Helena Petri siku aliyopotea.Picha na Juma Mtanda 

Morogoro. Tukio la kifo cha kikongwe, Hellan Petri Mahunzila (75) ambaye alipotea katika mazingira ya kutatanisha kwa siku 12 kisha siku ya 13 mwili wake kuonekana kando ya shamba lake huku  mwili wake ukiwa imechunwa ngozi mwili mzima, imezua hofu kubwa.
Wakazi Kitongoji cha Gongo, Kijiji cha Mgata, Kata ya Bwakilajuu mkoani Morogoro, ambako tukio hilo limetokea, sasa wanaishi kwa hofu.
Baadhi yao  wanalazimika kujisaidia haja ndogo na kubwa katika makopo hasa nyakati za usiku, ndani ya nyumba zao. Tukio hilo limebadili kabisa mfumo wa maisha na kutembea, wengi wanalazimika kuingia ndani ya nyumba kuanzia saa 12 asubuhi hadi saa 12:30 jioni wakihofia kutekwa.
Tukio lenyewe
Ni  saa 7 usiku, siku ya Jumatano kuamkia Alhamisi ya Oktoba 2 mwaka huu, Eliza Steven (19) anaamka na kumnyonyesha kichanga chake,  James Peter (miezi mitatu), baada ya kilio cha mtoto huyo mchanga kuhitaji kunyonya.
Baada ya James kunyonya na kushiba, alinyamaza kulia, hiyo ilikuwa ni kama kumpa fursa mama yake kutoka ndani ili aende nje kwa ajili ya kujisaidia haja ndogo.
Anafungua mlango wa chumba chake na kutoka nje kujisaidia huku akipiga jicho na kuangalia mlango wa chumba anacholala bibi yake,  anaona mlango upo wazi. Jambo hilo, hakulitilia shaka sana kwani alikuwa na imani angeweza kukutana naye nje ama chooni,  haikuwa hivyo.
Alilazimika baadaye kuingia  chumba anacholala bibi huyo, aliangalia kitandani ili kuweza kujibu maswali yake yaliyojaa kichwani likiwamo la kwa nini bibi yake ameshindwa kufunga mlango kama alitoka nje? Anaanza kusema Eliza. Eliza aliendelea kueleza kuwa baada ya kuchunguza katika chumba kile kinachotumiwa na bibi yake, Hellen ambaye alikuwa na kawaida ya kufunga mlango pindi aiingiapo kulala, hakumwona na kuchukua jukumu la kumwamsha mama yake mzazi, Yustina Kasian (40) ili aweze kusaidiana naye kumtafuta.
Yustina Kasian ambaye ni mtoto wa pili kwa kuzaliwa kwa bibi, Hellen Petri Mahunzila anasema baada ya kuelezwa maneno yale na mtoto wake, Eliza Steven ambaye ni bibi yake alienda katika kile chumba anacholala mama yake na kuangalia huku na huku, bila mafanikio.
 
“Nilienda chooni na kuangalia ndani ya choo lakini sikumwona, nilirudi ndani na kumwamsha mume wangu, Steven Francis (50) ili naye atusaidie kumfuata kwani tayari hofu ilianza kutanda moyoni mwetu na kujiuliza maswali ambayo hatukuweza kupata majibu usiku ule,” anasema Yustina.
Mimi baada ya kuelezwa jambo hilo na mke wangu nilitoka nje na tochi hadi chooni na kumulika ndani na kuzunguka kile choo, sikuweza kumwona. Nilienda pia kumtafuta  kwenye banda la kupikia na eneo zima la migomba lakini mama mkwe wangu hakuweza kuonekana akiwa hai ama amekufa,” anasema Steven Francis.
Francis anasema baada ya kushindwa walikwenda kwa majirani kuomba msaada wa kumtafuta; walikwenda kwa jirani Selis Silili na Calist Stephano.

Jirani zake hao walitoa wazo la kwenda kutoa taarifa la tukio hilo kwa Mwenyekiti wa Kitongoji cha Gongo, Kijiji cha Mgata, Kata ya Bwakilajuu, Festo Mfaume usiku ule wa saa 7:45.
Mwenyekiti huyo aliwaeleza kuwa kutokana na giza nene na mvua wangemtafuta asubuhi yake siku ya Alhamisi.
Mwenyekiti huyo wa Kitongoji cha Gongo, Festo Mfaume katika mahojiano na mwandishi wa makala haya anasema,
“Kitongoji changu kina zaidi  ya wananchi 325 na tukio hili limekuwa la kwanza kutokea. Nilichofanya ni kuwatawanya watu katika makundi kuanza kumtafuta bibi yetu Hellen sehemu za misitu, vichanga, shambani kwake, mapango na kutoa taarifa vitongoji vya jirani ili nao watusaidie kumtafuta, lakini tulifanya kazi hiyo kwa siku sita bila mafanikio na kukata tamaa”.
Katika ardhi ya kitongoji hicho hakuna sehemu ambayo wananchi wameshindwa kufika lakini cha ajabu baada ya wao kukata tamaa kwa kumtafuta kwa siku sita, mwili wake ulionwa na mjukuu wake, Eliza Steven Oktoba 15 kando ya shamba lake ukiwa umechunwa ngozi na kutelekezwa, anasema mwenyekiti huyo wa kitongoji.
Siku ya Oktoba 15 saa 7 mchana mwaka huu, Eliza Steven aliondoka nyumbani kwenda shambani kuchuma mbaazi katika shamba la bibi yake, mita chache aliona nyasi zimelala na mburuzo wa kitu jambo hilo lilimshtua.
“Kabla ya njia ya kuingilia shambani niliona nyasi zimelala, ni kama kuna kitu kilikuwa kimeburuzwa, nilistuka kidogo kwa sababu eneo hilo la mburuzo kuna nyasi  na miba, nami nikaona ngoja nipite katika njia hiyo ya mburuzo nione mwisho wake,” alisema Eliza.
Eliza anasema umbali wa hatua 18 za miguu akaona khanga na hatua mbili mbele yake akaona tena kitenge,  aliponyanyua macho mbele yake aliona mwili wa mtu.
“Nilitambua zile nguo kuwa ni za bibi yangu Hellen aliyepotea siku 13 zilizopita na nilipousogelea zaidi ule mwili nilitambua kwa kuona nguo nyingine ambazo alivalishwa likiwamo gauni, bangili, hereni na shanga shingoni lakini mwili wake nilishangaa kuuona umekuwa mweupe hauna ngozi”.
Baada ya kuona vile alipatapwa na mshtuko mkubwa huku moyo ukimdunda kwa hofu kwa kuona tukio hilo ambalo kwake ni la ajabu na kuamua kurudi kinyumenyume huku akimwita mama yake ambaye naye alienda shambani huko akimpelekea mtoto wake ambaye alikuwa analia ili aweze kumnyonyesha kwani siyo mbali na shamba.
Mwenyekiti wa Kitongoji cha Gongo, Festo Mfaume anaeleza kuwa baada ya kuonekana kwa mwili huo alifuatwa nyumbani kwake na kijana aliyefahamika kwa jina la Anthony Kalisti na kumweleza kuwa bibi aliyepotea ameonakana kando ya shamba lake lakini tayari amekufa.
Diwani wa Kata ya Bwakilajuu, Emili Kidevu anasema “Baada ya mimi kujulishwa juu ya tukio lile na kuona mwili namna ulivyochunwa ngozi mwili mzima, nilienda Ofisi ya Mtendaji na Mwenyekiti wa Kijiji cha Mgata kutoa taarifa. Akatoa agizo la kuulinda mwili ule hadi atakapofanya utaratibu wa kuwaleta askari polisi na daktari ili wachunguze tukio hilo”.

Marehemu Hellen Petri Mahunzila (75) ameacha watoto watatu wakiwamo wawili wa kiume , Kassim Athmani Lingila (58), Banzi Mazangwa (55) na mwanamke pekee, Yustina Kasian (40) na aliachana na mume wake miaka 10 iliyopita huku historia yake ikielezwa kuwa maisha yake yote alijishughulisha na suala la kilimo.
Diwani wa Kata ya Bwakilajuu, Emili Kidevu anasema kuwa tangu kutokea tukio hilo hakuna uchunguzi wowote umefanyika kutoka ndani ya jeshi la polisi zaidi ya kufika siku ya tukio.
Shaka nyingine inayumkumba diwani huyu na jamii ya Kitongoji cha Gongo, Kijiji cha Mgata na vijiji jirani ni namna tukio hilo lilivyotekelezwa kiutalaamu bila kukosea.  Kwanza anaweza kusema kuwa marehemu alitekwa, kisha akahifadhiwa ndani ya nyumba kwa siku 10 kabla ya kifo chake.
Naye Kamanda wa jeshi la Polisi mkoa wa Morogoro, Faustine Shilogile akitolea ufafanuzi na kuthibitisha kutokea kwa tukio la marehemu, Hellen Petro (75) kufariki dunia baada ya kupotea kwa siku 11 kisha mwili wake kukutwa umechunwa ngozi siku ya 12 amelihusisha tukio hilo na masuala ya ushirikina.
Shilogile anasema kuwa jeshi la polisi lipo katika uchunguzi wa kuwabaini wauaji na watakapobainika sheria itafuata mkondo wa sheria ikiwemo kufikishwa mahakamani.
“Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi, tuna imani wahusika watakamatwa,” anasema.
MWANANCHI

Hakuna maoni