Zinazobamba

WATAALAM WA TANROADS WASISITIZWA KUZINGATIA MATUMIZI YA TAARIFA ZA HALI YA HEWA KATIKA KUPANGA NA KUTEKELEZA SHUGHULI ZA UJENZI


Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) imesisitiza umuhimu wa kuzingatia  matumizi ya taarifa za hali ya hewa katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa miundombinu ikiwemo barabara na madaraja . 

Akizungumza na viongozi na watumishi mbalimbali wa  Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS)- DODOMA, katika kikao kilichofanyika leo kati ya TMA na Menejimenti na Wataalamu wa TANROAD -Dodoma, Mkurugenzi Mkuu wa TMA na Makamu Mwenyekiti wa Jopo la Kimataifa ya Sayansi ya Mabadiliko ya Hali ya Hewa na Tabianchi, Dkt.Ladislaus Chang’a, alisema “Dunia inakabiliwa na changamoto ya kasi kubwa ya ongezeko la joto, idadi na ukubwa wa matukio ya hali mbaya ya hewa ikiwemo mvua kubwa, mafuriko, upepo mkali na ukame.

Matukio haya ya hali mbaya ya hewa yanaendelea kuhatarisha maisha ya watu na mali zao, ikiwemo uharibifu wa miundombinu mbalimbali ikiwemo ya barabara na madaraja". 

Aidha, aliongeza kwa kusema kuwa mwaka huu 2026, dunia inakabiliwa na changamoto ya El Nino, ambayo inatarajiwa kuendelea kuimarika kuelekea mwishoni mwa mwaka. Mamlaka ya Hali ya Hewa inaendelea kufuatilia kwa karibu na itatoa taarifa ya kina kuhusu mwelekeo na athari za El-Nino 2026 tarehe 18/08/2026 wakati wa kutoa utabiri wa mvua za VULI. 

Dkt. Chang’a alisisitiza umuhimu wa kuzingatia sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania Na. 2 ya Mwaka 2019 katika matumizi ya taarifa na huduma za hali ya hewa katika sekta zote za kiuchumi na kijamii ili kuokoa maisha ya watu na mali zao, na pia kuongeza ufanisi na tija katika shughuli zote za kimaendeleo.

Hatua na mikutano hii ni mwendelezo wa mkakati wa kuhamasisha matumizi ya taarifa na  huduma za hali ya hewa katika mipango na maendeleo ya Taifa, hususan kipindi hiki ambapo Dunia kwa ujumla inakabiliwa na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa.

No comments