Zinazobamba

DC KILWA AIPONGEZA TANESCO KWA KUJIPANGA KUFIKISHA UMEME KATIKA BANDARI YA UVUVI - KILWA.


📌Asema ni Mradi wa kimkakati wenye fursa za kiuchumi kwa maslahi mapana ya nchi

📌Amtaka Mkandarasi kukamilisha mifumo ya upokeaji umeme kutoka TANESCO

Mkuu wa Wilaya ya Kilwa, Mhe. Mohamed Nyundo, ameipongeza TANESCO kwa jitihada na utayari wake wa kuhakikisha umeme unafika katika mradi wa ujenzi wa Bandari ya Uvuvi, inayotarajiwa kuwa na mchango mkubwa katika fursa za kiuchumi.

Mhe. Nyundo ameyasema hayo Mei 6, 2026, baada ya ziara ya Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, katika mradi huo wa ujenzi wa Bandari ya Uvuvi Kilwa, kwa lengo la kuangalia kama miundombinu ya upokeaji wa umeme imekamilika.Amesema, licha ya TANESCO kuwa na utayari wa kupeleka umeme katika bandari hiyo, bado mkandarasi hajakamilisha mifumo ya kupokea umeme kutoka TANESCO.

“Nikupongeze sana MD kwa kufika na timu yako ya wataalamu. Mmejionea mahitaji ambayo TANESCO mnapaswa kutoa, na tumeona mkandarasi bado hajakamilisha baadhi ya mifumo katika eneo lake ili kupokea huduma ya umeme kutoka kwenu,” alisema Mhe. Nyundo.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TANESCO, Bw. Lazaro Twange, amesema TANESCO ina umeme wa kutosha, na tayari kumejengwa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilvoti 33 kutoka Somanga ili kupeleka umeme katika bandari hiyo ya uvuvi.Aidha, ameeleza jitihada zinazoendelea kufanyika za upanuzi wa kituo cha kupokea na kupoza umeme cha Singino, Kilwa, kwa kuongeza transfoma yenye uwezo wa MVA 5 ili kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme katika maeneo hayo.

“Kimsingi, TANESCO tuna umeme wa kutosha kwa ajili ya bandari. Tunafahamu kwamba bandari hii ikiwa inafanya kazi itahitaji takribani megawati 2.5 za umeme. Tutawapa umeme moja kwa moja kutoka katika kituo chetu cha kufua umeme cha Somanga,” alifafanua Bw. Twange.

Ziara ya Mkurugenzi Twange imelenga kukagua miradi ya umeme inayoendelea katika mikoa ya Pwani, Lindi na Mtwara



No comments