Zinazobamba

WANANCHI WAOMBWA KUJITOKEZA KESI YA KUPINGA TAMISEMI KUSIMAMIA UCHAGUZI.

Na Mwandishi Wetu

Raia Watatu wa Tanzania  ambao  ni Dkt Ananilea Nkya,Bob Wangwe pamoja na Bubelwa Kaiza, wamefungua kesi Mahakama Kuu Masijala ya Kanda ya Dar es Salaam  dhidi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kupinga Wizara ya Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kusimamia uchaguzi wa mwaka huu wa Serikali za Vijiji, Kamati za Mitaa na  wa Vitongoji .

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Agost 27,2024 na Dkt Ananilea Nkya mbele ya Mkutano na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam , Maombi hayo  yatasikilizwa Jumatano ya Agost, 28 Agosti 2024 wiki hii,nakwamba Maombi hayo yalitajwa kwa mara ya kwanza Agost 22,2024.

Dkt Nkya ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba Tanzania (JUKATA) amewaomba Wananchi kujitokeza kwa wingi Kwa ajili ya kusikiliza kesi hiyo ambayo itasikilizwa majira ya saa nane Mchana Mahakama Kuu Masijala ya Kanada ya Dar es salaam.

"Maombi hayo (Misc Cause no 19721 ya 2024 mbele ya Jaji Dyansobera)  yalipotajwa Mahakamani kwa mara ya kwanza, Jaji Dyansobera aliwapa wanasheria wa Serikali  siku saba, kati ya Agosti 22 na 28 2024, kuleta hoja za Serikali mahakamani ili mahakama izisikilize, kupima na  kutoa maamuzi kuhusu maombi ya raia kuzuia TAMISEMI kujihusisha na uchaguzi wa Serikali za Vijiji, Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji." Amesema Dkt Nkya

Nakuongeza kuwa "Sisi raia tuliopeleka maombi ya kufungua shauri la Kikatiba Mahakama Kuu tunaamini kuna umuhimu mkubwa  kwa wananchi kufika kwa wingi Mahakama Kuu Dar es Salaam siku ya Jumatano, Agosti 28, 2024 maombi ya shauri hilo yatakaposikilizwa, Raia watapata fursa  ya kusikiliza hoja za serikali moja kwa moja kutoka kwa wanasheria wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na hoja za raia kupitia kwa Mawakili wetu kupinga TAMISEMI kusimamia uchaguzi wa Serikali za Vijiji, Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji mwaka huu, 2024.
              
Kwa upande Wake Bob Wangwe amesema kuwa wamefungua shauri hilo kwa kuwa wanatambua kwamba raia ndio  mamlaka ya nchi kama inavyothibitishwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 8(1)(a) 

"Ibara hii ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inasema kuwa “Wananchi ndiyo msingi wa Mamlaka yote na Serikali itapata Madaraka na Mamlaka yake yote kutoka kwa wananchi kwa mujibu wa Katiba hii”amesema  Wangwe

Nakuongeza kuwa " sisi raia  kwa mamlaka tuliyonayo kwa mujibu na Katiba tunapinga ,tunaona ni kinyume cha Katiba na sheria za nchi iwapo TAMISEMI itasimamia uchaguzi wa Serikali za Vijiji, Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji.

 Aidha Wangwe ameendelea kusema kuwa, kifungu cha 10(1)(c) cha Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi Namba 2 ya 2014 kinatoa wajibu na mamlaka ya kusimamia uchaguzi wa Serikali za Vijiji, Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji kwa Tume, siyo TAMISEMI. 

Bob Wangwe ambaye pia ni Mkurugenzi Mkuu wa JUKATA amesema uchaguzi ukisimamiwa na mamlaka isiyohusika kuna hatari ya uchaguzi huo kutokuwa na unyoofu, huru na haki  na athari zake ni pamoja na kusababisha vijiji, mitaa na vitongoji kuongozwa na watu wasiowaadilifu na wasiowajibika kwa raia, hata kufuja michango na kodi za wananchi.

"Msingi wa Kisheria wa Kesi hii
Maombi ya kesi yanahoji kwamba Wizara ya Ofisi ya Rais TAMISEMI kusimamia uchaguzi kunaleta hatari kubwa kwa haki na uwazi wa mchakato wa uchaguzi. Matukio ya awali ya dosari na upendeleo unaoonekana ndani ya Wizara yamezua maswali juu ya uwezo wake wa kusimamia uchaguzi huu bila upendeleo. Amesema

Nae Bubelwa Kaiza amesema kuwa hatua hiyo ya kisheria inalenga kulinda haki ya kikatiba ya raia wa Tanzania kushiriki katika mchakato wa kidemokrasia ambao ni nyoofu, huru na wa haki.

Amesema kwamba baada ya kutungwa kwa sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi 2024 na kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania 1977 ibara ya 74(6)(e) majukumu ya kusimamia uchaguzi wa Serikali za Vijiji, Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji yako chini ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi.

"TAMISEMI kutaka kusimia uchaguzi huu ni batili na kinyume cha sheria. Kwa mujibu wa kifungu cha 1 0(1)(c) cha Sheria ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, ni Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi pekee yenye jukumu la kusimamia uchaguzi wa Serikali za Vijiji, Kamati za Mitaa na Wenyeviti wa Vitongoji.

Madhara ya Kukosekana kwa Viongozi halali kwenye Mitaa, Vijiji, na Vitongoji 
Tunahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kufuatilia na kusikiliza maombi ya kesi hii mahakamani kwa sababu uchaguzi wa viongozi wa vitongoji, vijiji na mitaa 2024 usipoendeshwa kwa mujibu wa Katiba, sheria na uadilifu raia wataendelea kukabiliwa na changamoto za maendeleo pasipo msukumo wa uongozi kuwajibika kuzishughulikia.

Hakuna maoni