Zinazobamba

WANAHARAKATI WAANZA MCHOKONOA MAGUFULI,SASA LHRC WAINGILIA KATI,SOMA HAPO KUJUA



 Helen Kijo Bisimba, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC

STAILI ya Rais John Magufuli kutimua watumishi wa umma kwa ‘munkari’ inawavuruga watu wengi ambapo Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimeonya, anaandika Regina Mkonde.

Kabla ya LHRC kuonya, Edward Lowassa, aliyekuwa mgombea uraas kupitia Chadema na kuungwa mkono na Ukawa pia Sheikh Ponda Issa Ponda, Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam nchini walionya staili hiyo na kushauri taratibu za kisheria za utumishi wa umma zifuatwe.

Helen Kijo Bisimba, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC ameikumbusha serikali kufuata sheria za utumishi wa umma katika kuwawajibisha watumishi wanaotuhumiwa kufanya makosa.
Bisimba ametoa kauli hiyo leo wakati wa uzinduzi wa ripoti ya haki za binadamu ya mwaka 2015 uliofanyika jijini Dar es Salaam, MwanaHALISI Online lilishuhudia.

“Inafahamika kwamba, Rais John Pombe Magufuli ameikuta nchi sehemu mbaya na anahitaji kuirekebisha.

“Ila ni vema akafuata taratibu za kisheria wakati anapotaka kumtumbua mfanyakazi aliyeajiriwa na serikali ambayo ndiyo anayoiongoza,” amesema Bisimba.
Anaeleza kuwa, Rais hakuchukua uamuzi wa busara kwa kumsimamisha kazi Wilson Kabwe, aliyekuwa Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam mbele ya hadhara na kwamba, alitakiwa kufanya uamuzi huo kwa kufuata sheria.
“Makonda (Paul Makonda) hakuwa na sababu za kumsema Kabwe mbele ya hadhara, alitakiwa afuate utaratibu, si maanishi kuwa namtetea Kabwe, bali kutokana na agizo la rais alilotoa la kusimamishwa na kufanyiwa uchunguzi, je atakapobainika kuwa ni msafi ataweza kumsafisha?” anahoji.
Bisimba amewataka Watanzania waache unafiki kwamba, wapo baadhi ya wanasheria wanaojua taratibu za kumsimaisha kazi mtumishi wa umma lakini walishindwa kumshauri badala yake waliacha aendelee na uamuzi wake.
“Mfano jana alikuwa anauliza wananchi, nimtumbue nisimtumbue, mbele ya hadhara, huyo aliyekuwa anamfanyia hivyo ni mtumishi aliyeajiriwa na serikali, isitoshe Kabwe ninavyomjua ni mgonjwa, je angepata matatizo ingekuaje?” anauliza.
Bisimba pia ametolea mfano wa hatua iliyochukuliwa wakati wa kufukuzwa kazi Anne Kilango Malecela, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga kwamba, aliju akwamba amefukuzwa kazi baada ya kupigiwa simu akiwa ofisini.
“Kilango alitumbuliwa wakati alipokuwa ofisini, alipigiwa simu ili kujibu baadhi ya maswali juu ya kufukuzwa kwake, cha kustajaabisha hakuwa na taarifa kama alifukuzwa kazi na rais,” amesema.
Amesema kuwa, mfumo wa utumishi mbaya ulianzishwa na serikali baada ya kuuondoa mfumo wa ujamaa na kuuweka mfumo wa ubepari.
Kwa upande wa sheria anasema, zipo nzuri ila nyingi kati ya hizo zinahitaji maboresho na kwamba, inahitajika Katiba Mpya ili ifanyike marekebisho ya sheria zilizoachwa na mkoloni.
Aidha, ripoti iliyotolewa leo inaonesha kuwa, uchaguzi uliofanyika tarehe 25 Oktoba 2015 ulikuwa huru japo kulikuwa na wasiwasi wa kutokuwa na haki kutokana na madai ya kuibiwa kura.
Ripoti hiyo inabainisha kuwa, kwa mujibu wa uangalizi uliofanywa na LHRC umebaini kuwa, elimu ya uraia haikutolewa vizuri, watu wenye ulemavu walipata shida kufika maeneo ya kampeni na kutumika kwa vifaa vya serikali wakati wa kampeni hasa magari pamoja na uchelewashaji wa kutangaza matokeo katika vituo mbalimbali.

Hakuna maoni