Zinazobamba

Taarifa ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muugano akizungumzia kuhusu changamoto za muungano na majibu yake


Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muugano Bi. Bi Samia Suluhu Hassan akifafanua jambo kwa waandishi wa habari mapema hiyo jana
Waandishi wa habari wakiwajibika,

Tangu kuasisiwa kwa Muungano wetu mwaka 1964, kumekuwepo na changamoto mbalimbali katika utekelezaji wa Mambo ya Muungano. Changamoto hizo zimekuwa zikishughulikiwa na Tume na Kamati mbalimbali zilizokuwa zinaundwa katika vipindi tofauti vya Uongozi wa nchi yetu. Miongoni mwa Tume na Kamati hizo ni Tume ya Jaji Nyalali (1991), Kamati ya Amina Salum Ali (1992), Kamati ya Shellukindo (1994), Kamati ya Jaji Mark Bomani (1995), Kamati ya Shamhuna (1997), Kamati ya Jaji Kisanga (1998), Kamati ya Ramia (2000) na Kamati Shellukindo (2004) iliyopelekea kuundwa kwa Kamati ya Pamoja ya SMT na SMZ (2006). Mambo yaliyoibuliwa na Kamati ya Shellukindo (2004) ni:- Aidha, hadi mchakato wa kuandika Katiba mpya unaanza, changamoto kubwa zilizokuwa zinaendelea kutafutiwa ufumbuzi ni kama ifuatavyo: 

1.      Utafutaji na uchimbaji mafuta na gesi asilia;
2.      Ushirikiano wa Zanzibar na taasisi za nje;
3.      Ajira kwa watumishi wa Zanzibar katika Taasisi za Muungano;
4.      Sheria ya Haki za Binaadamu kufanyakazi Tanzania Bara na Zanzibar;
5.      Uvuvi katika Ukanda wa Uchumi wa Bahari Kuu;
6.      Utekelezaji wa Merchant Shipping Act na Zanzibar kujiunga naInternational Marine Organization;
7.      Ushiriki wa Zanzibar katika Jumuiya ya Afrika Mashariki;
8.      Mgawano wa Mapato yatokanayo na Misaada kutoka Nje;
9.      Misamaha ya Mikopo ya fedha kutoka IMF;
10. Hisa za SMZ zilizotoka iliyokuwa Bodi ya Sarafu ya Afrika Mashariki, na Mgawano wa Mapato yatokanayo na Faida ya Benki Kuu;
11. Malalamiko ya Wafanyabiashara wa Zanzibar kutozwa Kodi mara mbili;
12. Uwezo wa SMZ kukopa ndani na nje ya nchi; na
13. Usajili wa Vyombo vya Moto.
Mambo yote Kumi na Tatu (13) yalipatiwa ufumbuzi isipokuwa baadhi ya masuala ya Uhusiano wa Kifedha na Usajili wa Vyombo vya Moto ambayo yanasubiri maamuzi katika ngazi mbali mbali za Serikali.  Machakato wa kutunga Katiba Mpya ya Nchi yetu nayo ilikuwa fursa adhimu iliyotuwezesha kuweka ndani ya Katiba ya Nchi, yale tuliyokubaliana na kutolewa maamuzi na Kamati ya Pamoja ya SMT na SMZ.  Kwa maana hiyo, Katiba Inayopendekezwa imejielekeza kwenye mambo yafuatayo:-

a)         Kuanzishwa kwa Tume ya Mambo ya Muungano
Ibara ya 127 ya Katiba Inayopendekezwa inaanzisha Tume ya Usimamizi na Uratibu wa Mambo ya Muungano. Tume hii, pamoja na mambo mengine, itakuwa na jukumu maalum la kuwezesha uratibu na ushirikiano wa sera, sheria, mipango na mikakati baina ya SMT na SMZ. Uratibu huu utasaidia sana kubainisha changamoto zozote zitakazojitokeza katika kutekeleza shughuli za Muungano. Itakumbukwa kwamba hivi sasa ipo Kamati inaoyongozwa na Makamu wa Rais ya kushughulikia changamoto na masuala mengine ya Muungano. Kamati hii haikuanzishwa kikatiba, hivyo, ipo mifano ambayo utekelezaji wa maamuzi ya Kamati ulitegemea sana uhusiano mzuri kati ya watendaji na taasisi husika za pande zote mbili. Uhusiano mzuri na utashi wa kisiasa ni mambo muhimu.  Hata hivyo, Katiba Inayopendekezwa imeona hii haitoshi.  Hivyo, mojawapo ya malengo ya kuanzishwa kwa Tume hii ni kujenga misingi imara ya kikatiba ya utekelezaji wa shughuli za Muungano, na kuyapa nguvu ya kisheria maamuzi mbalimbali yatakayotolewa na Tume hii.

b)      Nafasi na Hadhi ya Rais wa Zanzibar
Kwa mujibu wa Hati ya Makubaliano ya Muungano, Rais wa Zanzibar alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano ya Tanzania. Hata hivyo, kufuatia mabadiliko mbalimbali yaliyotokea katika nchi yetu, hususan kurejeshwa kwa mfumo wa vyama vingi vya siasa mwaka 1992, nafasi ya Rais wa Zanzibar kama Makamu wa Rais iliondolewa.  Baada ya mabadiliko mbalimbali ya kisiasa na kikatiba (hususan kwa upande wa Zanzibar, na uzoefu uliopatikana wa namna bora zaidi ya kuimarisha Muungano wetu), Katiba inayopendekezwa inarejesha nafasi ya Rais wa Zanzibar kama Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano kupitia Ibara ya 99(b).

c)          Ushirikiano na Uhusiano wa Zanzibar na Taasisi za Kimataifa
Jambo hili ni miongoni mwa mambo ambayo yalionekana kuwa moja ya changamoto zilizoukabili ustawi wa Muungano na maendeleo ya pande zote mbili za Muungano wetu. Katiba inayopendekezwa inatambua umuhimu huu na haja ya kuimarisha mamlaka ya Zanzibar kwa mambo yasiyo ya Muungano yanayohusu Zanzibar. Katiba inayopendekezwa inajibu hoja hii kupitia Ibara ya 76.  Kwa mujibu wa ibara hii, Zanzibar itakuwa na uwezo na uhuru wa kuanzisha uhusiano au ushirikiano naJumuiya au Taasisi yoyote ya kikanda au kimataifa kwa mambo yanayoihusu. 

d)        Uwezo wa Zanzibar kukopa ndani na nje ya nchi
Katiba ya  Jamhuri ya Muungano ya mwaka1977, inaweka mamlaka ya kukopa nje ya nchi katika Serikali ya Jamhuri ya Muungano. Katika muktadha wa kuimarisha uwezo na uhuru wa Zanzibar kwa shughuli za maendeleo yake, Katiba Inayopendekezwa katika Ibara ya 261 inatoa mamlaka kwa SMZ kukopa fedha ndani na nje ya Jamhuri ya Muungano bila ya kulazimika kupitia Serikali ya Muungano. Kwa minajili hii, endapo mkopo husika utahitaji dhamana, basi SMT itatoa dhamana kwa mkopo unaoombwa. Ni wazi utaratibu huu utarahisisha sana upatikanaji wa mikopo kwa maendeleo na ustawi wa Zanzibar.


e)            Orodha ya Mambo ya Muungano
Muungano wetu ulianza kwa kuainisha mambo 11 ambayo ndiyo yaliyokuwa msingi wa ushirikiano kati ya iliyokuwa Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya Watu wa Zanzibar. Hadi leo ushirikiano umekua na kufikia mambo 22. Katika kipindi cha miaka takriban hamsini ya Muungano wetu mahitaji na mazingira yamebadilika. Pande zote mbili za Muungano zimejiimarisha kwa namna mbalimbali katika maendeleo yao. Kwa kuzingatia ukweli huu, Katiba Inayopendekezwa inaainisha masuala 16 badala ya 22 ya sasa [Ibara ya 74(3)]. Miongoni mwa mambo yaliyopunguzwa ni suala la utafutaji na uchimbaji wa mafuta na gesi asilia ambalo kipekee lilionekana kuwa changamoto kubwa katika ustawi na maendeleo ya taifa letu.

f)          Ajira katika Taasisi za  Muungano
Mojawapo ya changamoto zilizojitokeza katika uhai wa Muungano wetu ni suala la ajira ya wananchi wa pande zote mbili katika taasisi za Muungano. Pamoja na Tume ya Utumishi wa Umma kuwa na jukumu la ujumla katika eneo hili, Katiba Inayopendekezwa katika Ibara ya 128(1)(f) na 128(3) inatamka wazi kwamba Tume ya Usimamizi na Uratibu wa Mambo ya Muungano itakuwa vile vile na jukumu la kusimamia uwakilishi wa pande zote mbili za Muungano ndani ya ajira ya utumishi wa Jamhuri ya Muungano. Ibara ya 150(4) imekuwa wazi zaidi katika nafasi za Spika na Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Aidha, Tume itaweka utaratibu utakaowezesha uteuzi wa viongozi na watumishi katika taasisi au wizara za Muungano kufanyika kwa kuzingatia uwakilishi wa pande zote mbili za Muungano. Hii ni hatua muhimu ya kuleta uwiano murua,  kupata mchango  chanya wa wananchi wote katika ajira na kuuimarisha  Muungano wetu, na kama ilivyosisitizwa katika Ibara ya 209(2) ya katiba inayopendekezwa.

Mafanikio mengine yaliyopatikana ndani ya miaka 51 ya Muungano ni kuwepo kwa Taasisi za Utendaji Serikalini kwa Pande zote za Muungano. Taasisi zenye Ofisi zake Bara na Zanzibar ni; Taasisi za Ulinzi na Usalama wa Taifa (Jeshi, Polisi na Usalama wa Taifa), Benki Kuu ya Tanzania, Idara ya Uhamiaji, Ofisi ya Usajili wa Vyama vya Siasa Tanzania, Ofisi ya Vitambulisho vya Taifa, Mamlaka ya Hali ya Hewa, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Tume ya Sayansi na Teknologia (COSTECH), Tume ya Nguvu za Atomic (TAEC), na Kitengo cha Biashara za nje (TANTrade),

Pamoja na kuwepo kwa Taasisi hizo pia kumekuwa na Miradi ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi ambayo nayo imekuwa na Sura ya Muungano. Miradi hiyo ni; TASAF, MACEMP, Millennium Challenge Account, Miradi ya Kilimo na Ufugaji (ASSDP na ASDPL),  Miradi ya Mikopo kwa Wajasiriamali wadogo wadogo (SELF), na Masuala ya Vyuo na Mikopo ya Elimu  ya Juu.

Changamoto zinazoambatana na Mafanikio haya ni; Ugumu wa Urasimu katika kupata ufumbuzi wa mambo yanayotawaliwa na sheria tofauti baina ya Tanzania Bara na Zanzibar, pamoja  na Uhaba wa Rasilimali katika kuendeleza vikao vya majadiliano ya kutafuta ufumbuzi wa changamoto za Muungano.

No comments