ACT SASA KUWAKUTANISHA VIGOGO WA UPINZANI MACHI 29
PROFESA Ibrahim Lipumba-Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi
(CUF), ni miongoni mwa wasomi wa ndani na nje ya nchi walioalikwa kutoa mada
katika uzinduzi wa Chama cha ACT-Tanzania tarehe 29 Machi mwa huu. Anaandika
Mwandishi Wetu … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa
ya Afisa habari wa ACT, Abdallah Khamis uzinduzi huo utaanza saa tisa alasiri,
ambapo Prof. Lipumba, atazungumza kwa niaba ya vyama vya upinzani nchini kuhusu
‘kwanini Tanzania bado ni nchi masikini na nini cha kufanya kuondoa umasikini’.
Khamis anasema, “pia viongozi wote wa vyama vya siasa nchini,
mabalozi wa nchi mbalimbali na wakuu wa asasi zisizo za kiserikali wamealikwa”.
Viongozi wengine walioalikwa ni Samia Nkrumah, Kiongozi wa
Chama cha CPP cha Ghana na mtoto wa Rais wa kwanza wa Ghana Osagyefo Kwame
Nkrumah, Ababu Namwamba-Katibu Mkuu wa Chama cha ODM cha Kenya na Mwenyekiti wa
Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali wa Jamhuri ya Kenya.
“Vile vile ACT – Tanzania inatarajiwa kupata wageni kutoka
vyama rafiki vya Ujerumani Die Linke na Umoja wa vyama vya mrengo wa kushoto
Progressive Alliance.
“ACT-Tanzania kitafanya mkutano wake mkuu na uzinduzi wa
chama mnamo tarehe 28 na 29 Machi 2015. Katika mkutano Mkuu chama kitapitisha
katiba mpya ya chama na kufanya uchaguzi,” amesema.
Khamis ameongeza kuwa, viongozi watakaochaguliwa ni Kiongozi
wa chama, Mwenyekiti, Makamu wenyeviti, Katibu Mkuu na Manaibu makatibu wakuu.
Pia chama kitachagua wajumbe wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu.
“Baada ya uzinduzi, ACT- Tanzania itafanya mikutano ya
hadhara nchi nzima kwa kuanzia na mikoa ya Arusha, Shinyanga, Tabora, Kigoma na
Mbeya,” amesema Khamis.
No comments
Post a Comment