Zinazobamba

WANAFUNZI WA CHUO CHA IFM WAMUANGUKIA LOWASSA,WASEMA YAO SOMA HAPA KUJUA



 

Wanafunzi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM) jijini Dar es Salaam wametangaza azma yao ya kumuunga mkono Waziri Mkuu mstaafu, Edward Lowassa (pichani), iwapo ataamua kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

Wamesema wataanza kutekeleza azma yao hiyo kwa vitendo kwa kumsindikiza atakapokwenda kuchukua fomu za kukiomba ridhaa chama chake ya kuwania nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu.

Kauli hiyo ilitolewa na Mbunge wa Bunge la Serikali ya Wanafunzi wa Chuo hicho, Hafsa Masumai, kwa niaba ya wenzake, alipozungumza na waandishi wa habari, jijini Dar es Salaam juzi.

Mkutano huo na wanahabari, ambao ulifanyika ndani ya eneo la IFM, ulihudhuriwa pia na baadhi ya viongozi wa serikali ya wanafunzi na wanafunzi wa chuo hicho. 

Alisema wanamuunga mkono Lowassa kwa kuwa ni miongoni mwa viongozi watetezi wa masuala ya elimu.

“Wanafunzi wamekuwa wanakabiliwa na changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa sugu hata kutatuliwa na serikali, ikiwamo mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu,” alisema Masumai.

Aliongeza: “Tutamuunga mkono Lowassa, kwani ni kiongozi, ambaye anaonekana kujali elimu na tunaamini anaweza kutatua matatizo haya, ambayo yamekuwa yanatukabili kwa muda mrefu.”

Alisema Lowassa mbali na kuwa kiongozi aliyetetea elimu pia amekuwa akisaidia vijana katika nyanja mbalimbali, ikiwamo kuwasaidia kwenye vikundi vyao na kujikwamua dhidi ya makali ya maisha.

Masumai alisema kuachwa vijana hao vijiweni, kunaweza kukawafanya wajiingize kwenye makundi ya ujambazi, uvutaji unga na sehemu za hatari kwa maisha yao.

“Lowassa ni kiongozi wa pekee, ambaye anaweza kutusaidia vijana na kututetea kielimu. Na sisi kama vijana, tutamuunga mkono na tutahakikisha tunamsindikiza kuchukua fomu ya urais,” alisema Masumai.

Alisema endapo Lowassa atafanikiwa kupata nafasi hiyo, wanaamini kuwa vijana watapata haki zao za msingi pamoja na kuboreshewa elimu katika ngazi zote.

Kwa mujibu wa Masumai, vijana wamekuwa wakisahaulika kwenye nafasi mbalimbali na kwamba, hilo lisipoangaliwa na kutiliwa mkazo na serikali watakuja kupata makundi ya uhalifu.

Alisema makundi hayo yamekuwa yakifumbiwa macho bila kuangalia njia ya kuwawezesha kwa ngazi mbalimbali.

“Sisi kama vijana tumeona umuhimu wa Lowassa katika kipindi cha uongozi wake alipokuwa waziri mkuu. Hivyo, tuna imani hata akipata nafasi ya urais, tuna hakika kuwa vijana tutapata haki zetu,” alisema Masumai.

Hata hivyo, wanafunzi hao hawakufafanua kama katiba ya serikali yao ina kipengele kinachoruhusu viongozi kutangaza misimamo ya kuamua nani wa kumuunga mkono katika chaguzi za kisiasa.

Lowassa ni miongoni mwa makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambaye anatajwa kujitosa katika kinyang’anyiro cha kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.

Hata hivyo, hadi sasa Lowassa mwenyewe kwa kinywa chake hajatangaza kama atawania urais katika uchaguzi huo.

Badala yake, mara zote, ambazo amekuwa akiulizwa kuhusiana na hilo, amekuwa akijibu kwa kifupi kuwa: “Huwezi kuvuka daraja kabla hujalifikia.” 

Hadi sasa makada wa CCM waliotangaza nia na wanaotajwa kuwania urais kupitia chama hicho ni pamoja na Naibu Waziri wa Sayansi, Teknolojia na Mawasiliano, January Makamba; Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba; Mbunge wa Nzega, Dk. Hamis Kigwangallah; Waziri Mkuu wa sasa, Mizengo Pinda na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu.

Wanaotajwa kuwania nafasi hiyo ya juu kuliko zote nchini ni Mbunge wa Songea Mjini, Dk. Emmanuel Nchimbi na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.

Wengine ni Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe; Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta na mawaziri wakuu wastaafu, Lowassa na Frederick Sumaye.

Wanatajwa pia Spika wa Bunge, Anne Makinda; Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Prof. Mark Mwandosya na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wasira.

 Kati ya makada hao, sita waliwahi kuitwa na Kamati Ndogo ya Nidhamu iliyokuwa ikiongozwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Philip Mangula na kuwahoji kwa tuhuma za kuanza kampeni za uchaguzi mkuu ujao kabla ya wakati.

 Baada ya mahojiano hayo, Februari, mwaka jana, Kamati Kuu (CC) ya CCM ilitangaza uamuzi mzito dhidi ya makada wake hao baada ya kutiwa hatiani, kwa kuwafungia kugombea nafasi za uongozi ndani ya chama hicho kwa miezi 12, huku pia wakiwa chini ya uangalizi. Siku za kifungo hicho zilikamilika jana.

 Makada hao ni pamoja na Sumaye, Lowassa, Membe, Wasira, Ngeleja na Makamba, ambao wanakisubiri chama kutangaza hatma yao wakati wowote kuanzia sasa baada ya kipindi cha uangalizi kupita.

Hakuna maoni