HABARI MBAYA KUTOKA CHADEMA,KADA WAKE MUHIMU AUAWA KINYAMA,SOMA HAPO KUJUA
Kada wa Chadema katika Jimbo la Hai mkoani
Kilimanjaro, Anitha Swai ameuawa katika tukio lililogubikwa na wingu zito.
Taarifa za awali zilizopatikana usiku wa
kuamkia leo zimedai kuwa Anitha ambaye aligombea ubunge wa viti maalum
mwaka 2015, alitekwa nyara wilayani Rombo na kuuawa maeneo ya TPC nje kidogo ya
mji wa Moshi.
Vyanzo mbalimbali vya habari vimedokeza kuwa mara ya
mwisho mwanasiasa huyo alionekana akiwa na watu wawili wilayani Rombo siku ya
Jumatatu, Februari 27 na kuaga wanaelekea Arusha.
Hata hivyo, tangu siku hiyo Anitha hakuonekana hadi
maiti yake ilipogunduliwa jana (Alhamisi) jioni maeneo ya TPC huku gari lake
likiwa limetelekezwa maeneo ya Bomambuzi mjini Moshi.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Wilbroad
Mutafungwa amethibitisha kuokotwa kwa mwili huo, lakini amekataa kuthibitisha
kama ni wa kada huyo wa Chadema.
"Ni kweli kuna tukio hilo, lakini
ninachoweza kusema bado hajatambuliwa na mwili wake umepelekwa KCMC ili ndugu
waweze kuutambua," amesema.
Hata hivyo, Diwani wa Viti Maalumu wa Kata ya
Mawenzi mjini Moshi, Hawa Mushi amethibitisha kuwa aliyeuawa ni kada wa chama
chao, lakini chanzo na nani waliohusika hakijajulikana.
Hawa amesema taarifa zilizothibitishwa ni kuwa mwili
wake ulipatikana maeneo ya TPC huku simu iliyopatikana katika gari yake ndiyo
iliyosaidia kumtambua.