MBUNGE LEMA AMSHANGAA RAIS MAGUFULI,SOMA HAPO KUJUA
Mbunge
 wa Arusha Mjini, Godbless Lema ameibuka na kueleza kushangazwa na kauli
 ya Rais Dk. John Magufuli kwamba wabunge wa CCM waliotaka kwenda 
kumwona gerezani walikuwa wasaliti.
Lema alisema anatarajia Spika wa Bunge, Job Ndugai, atatoa msimamo juu ya kauli ya kiongozi huyo wa nchi.
Kauli
 hiyo ya Lema imekuja siku moja baada ya Rais Dk. John Magufuli, 
kuripotiwa na chombo kimoja cha habari  kwamba alishangazwa na hatua ya 
baadhi ya wabunge wa CCM waliounda kamati ya kutaka kwenda kumtembelea 
Lema gerezani.
Katika
 mkutano wake na wabunge hao juzi uliofanyika Ikulu ndogo ya Chamwino 
mkoani Dodoma, Rais Magufuli alisema amekuwa akielezwa kuwa kamati hiyo 
ilikuwa imepanga safari za kutaka kwenda kumwona Lema alipokuwa gerezani
 jambo ambalo alilifananisha ni sawa na usaliti kwa chama chake.
Katika
 taarifa aliyoitoa jana kwa vyombo vya habari, Lema alisema kitendo cha 
wabunge hao kutaka kumtembelea si usaliti bali ni upendo ambao ni muhimu
 kwa binadamu yeyote pale anapokuwa na matatizo.
Lema alikaa gerezani kwa muda wa miezi minne kwa kukosa dhamana kutokana na mashtaka yaliyokuwa yakimkabili.
“Mheshimiwa
 Rais Magufuli nakusalimu. Nimetoka gerezani hivi karibuni ambako 
nilikuwa huko kwa zaidi ya miezi minne kwa kunyimwa masharti ya dhamana 
kwa dhamana iliyokuwa wazi.
“Nimeona
 kwenye vyombo vya habari leo kwamba wale wabunge waliokuwa wanataka 
kunisalimia nilipokuwa magereza ni wasaliti wa chama cha CCM.
“Mheshimiwa
 Rais wengi walinisalimia wakiwemo wachungaji, masheikh, wabunge na 
viongozi mbalimbali, sidhani kama hatua hii ilikuwa ni usaliti isipokuwa
 upendo ambao ni muhimu kwa binadamu yeyote pale anapokuwa na matatizo.
“Mheshimiwa 
 Rais nimeogopa sana kwa kauli hii, je Taifa linakwenda wapi? Hivi kweli
 sisi wabunge ni maadui? Kama viongozi tutafikiri utengano ni moja ya 
njia ya kuimarisha vyama vyetu, bila shaka tutakuwa tunalitendea Taifa 
ubaya,” alisema Lema.
Mbunge huyo alisema dhambi hiyo ikikomaa ni wazi kwamba lugha za kidini, ukanda na ukabila hazitaacha kukomaa.
Alisema
 ni muhimu sasa wakajenga utamaduni wa kuhimiza mshikamano wa kitaifa 
bila kujali itikadi kama kweli wanapenda masikini na wanyonge.
“Nawaomba
 wabunge wenzangu walionijali wakati niko gerezani wasijisikie vibaya 
kwani walifanya jambo jema na muhimu kwa wakati muhimu sana katika 
maisha yangu ninatarajia kuwa Spika wa Bunge atatoa neon juu ya kauli 
hii ya Rais.
“Mheshimiwa
 Rais wakati wa msiba wa Christina Lissu dada yake na Tundu Lissu, 
nilikuona katika msiba ule wewe na mama yetu mke wako, je wewe ulikuwa 
unasaliti chama chako?
“Meshimiwa
 Rais neno la Mungu linasema wapendeni maadui zenu, waombeni wanaowadhi,
 wabarikini wanaowaonea kwani kufanya hivi ni kuishi kwa thawabu za 
Mwenyezi Mungu,”alisema Lema.
Mbunge
 huyo alisema pamoja na hali hiyo ya kuzuiwa lakini aliwashukuru wabunge
 wa CCM kwa kwenda kumjulia hali, akiwa nyumbani kwake baada ya kutoka 
gerezani.
“Sina
 la kusema katika hili kama Rais alikuwa anajua hawakuja kuniona 
gerezani lakini niwashukuru wabunge wa CCM wote waliokuja kunijulia hali
 nyumbani. Sisi kama nchi tunatakiwa kuwa na umoja badala ya kuanza 
kubaguana kwa itikadi zetu za vyama.
“Mdogo
 wangu wa kike amepata mchumba lakini familia ya huyo mchumba wake 
inatokana na CCM je tuvunje vikao vya harusi kwa sababu ya tofauti ya 
vyama?
“Jibu
 ni hapana sisi ni Watanzania ni lazima tuishi kwa kupenda na kwa umoja 
kama ambavyo utamaduni wetu unatutaka na si vinginevyo,” alisema.
Lema
 alikamatwa Novemba 2, mwaka jana mjini Dodoma nje ya viwanja vya Bunge 
na kufikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha, Novemba 4 mwaka 
jana akikabiliwa na kesi mbili namba 440 na 441 za uchochezi dhidi ya 
Rais Dk. John Magufuli.
Katika
 kesi ya kwanza ya jinai namba 440, anadaiwa kati ya Oktoba 22 mwaka 
jana maeneo ya Kambi ya Fisi, Kata ya Ngarenaro, katika mkutano wa 
hadhara alitoa maneno yenye kuleta tabaka miongoni mwa jamii kwa kutoa 
matamshi yenye chuki, kuibua nia ovu kwa jamii.
Katika
 kesi ya pili namba 441, alidaiwa kwamba, Oktoba 23, mwaka jana katika 
mkutano wa hadhara uliofanyika Viwanja vya Shule ya Sekondari Baraa, 
Lema  alitoa maneno kuwa:
“Kiburi
 cha Rais kisipojirekebisha, Rais akiendelea kujiona yeye ni Mungu, 
nimeota  Mwaka 2020 haitafika Mungu atakuwa ameshamchukua maisha yake,”.
Februari
 27,  mwaka huu, Mahakama ya Rufaa Tanzania ilifuta rufaa mbili za 
Jamhuri dhidi ya Lema baada ya mawakili wa Serikali kuieleza mahakama  
hiyo kuwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP), hana nia ya kuendelea na rufaa, 
hivyo kuiomba mahakama kuzifuta rufaa hizo zilizokuwa zinahusu dhamana 
ya mbunge huyo.

Post Comment