Zinazobamba

ZIARA YA RAIS MAGUFULI KENYA YABADILI HALI YA HEWA,SOMA HAPO KUJUA



Rais Kenyatta, Rais Magufuli na mkuu wa majeshi wa Kenya Jenerali Samson Mwathethe
RAIS John Magufuli leo amekutana na Uhuru Kenyatta, Rais wa Kenya kwenye ziara yake ya kikazi na kubadili upepo wa kisiasa uliokuwa unamwandama, anaandika Wolfram Mwalongo.

Akizungumza kwenye viwanja vya Ikulu, Kenya Rais Magufuli amesema, anao uhusiano mzuri na Rais Kenyatta na kwamba, waliokuwa wanadhani kuwa uhusiano huo una utata ‘hawakufikiri sawasawa.’

“…Najisikia nipo nyumbani na bahati nzuri Kenyatta namfahamu vizuri alipokuwa waziri wa tawala za mikoa…, huwa tunapigiana simu na Uhuru Kenyata watu, wengi hawajui- mjue leo huwa tunapigiana simu,” amesema Rais Magufuli.

Rais Magufuli amekuwa akihusishwa na siasa za upinzani nchini Kenya kutokana na uswahiba wake wa karibu na Raila Odinga, aliyekuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo na aliyeingia kwenye mpambano na Uhuru kwenye kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2012.
Kutokana na ukaribu wake, Rais Magufuli akiwa waziri wakati wa utawala wa Jakaya Kikwete, Rais Mstaafu aliwahi kwenda Kenya na kuungana na Odinga kwenye kampeni zake jambo lililodhihiri ukaribu wake.
Lakini pia, Aprili 2016 Odinga alimtembelea Rais Magufuli Wilaya ya  Chato, Tanzania wakati Magufuli akiwa mapumziko.

Raila Odinga, aliyekuwa Waziri Mkuu nchini Kenya akishuka kwenye Helkopta alipokwenda kumtembelea Rais John Magufuli Chato, Tanzania.
Odinga alikwenda kusali na Rais Magufuli katika kanisa la Bikira Maria Parokia ya Chato mkoani Geita kwenye ibada ya jumapili ya pili ya Pasaka ambapo alipata nafasi ya kuwasalimia waumini wa kanisa hilo.
“Nataka kuwathibitishia, ndugu yangu Uhuru Kenyatta na Wakenya wote, ninyi ni ndugu zetu, mfano Kenya kuna Wamasai pia Tanzania kuna wamasai, hata wanapotaka nyasi sidhani kama huwa wanaangalia hata mipaka. Tanzania wapo Wajaluo, hapa wapo Wajaluo …..,” amesema.
Amesema kuwa, Kenya ndio mshirika wa kwanza wa Tanzania katika uwekezaji na biashara barani Afrika na kwamba, hakuna taifa jingine ambalo limewekeza nchini mwake kama Kenya.
Amesema kuwa, kulingana na rekodi za uwekezaji nchini Tanzania kuna takriban kampuni 529 nchini humo kutoka Kenya ambazo zinaingiza takriban dola bilioni 1.7 kila mwaka huku takriban Watanzania 57,260 wakiwa wameajiriwa.
Amewataka mawaziri wa mambo ya nje wa pande zote mbili kukutana kabla ya mwaka kuisha ili kuona namana ya kuboresha ushirikiano kwa maslahi ya pande zote mbili.
RaisUhuru amesema kwamba, amefurahishwa na ziara ya Rais Magufuli nchini humo na kuwa, kufanya hivyo kunadhihirisha umoja wao.
Amesema, ili mataifa hayo yapate mendeleo ni lazima yafanye kazi kwa pamoja na kwamba, wamejadili namna ya kuimarisha uchumi, ulinzi, mawasiliano na miundombinu ya Barabara ya Tanga (Tanzania) mpaka Malindi nchini Kenya.
“Ili kupanua uchumi ni lazima Kenya na Tanzania tutembee pamoja na mawazili wetu wa nje watakubaliana ili kukamilisha hilo
“Tumeongea pia kuhusu usalama wa nchi zetu pia tumekubaliana mambo ya mawasialiano, tupo na mpangao wa barabara kutoka Tanga mpaka Malindi,” amesema Kenyatta.
Hii ni ziara ya tatu ya Rais Magufuli tangu kuapishwa kwake Novemba mwaka jana ambapo alianza kutembelea nchini Rwanda alipoenda kuzindua Daraja la Rusumo, ziara ya pili alikwenda Uganda kwenye sherehe za kuapishwa Rais Yoweri Maseveni.