Zinazobamba

KIKWETE AJITETEA KWA RAIS MAGUFULI,AIRUKA KAULI YAKE ALIYOISEMA UDSM,SOMA HAPO KUJUA



Rais Jakaya KIkwete (kulia) akifurahi na Rais mteule, John Magufuli muda mchache baada ya kutangazwa kushinda uchaguzi

JAKAYA Mrisho Kikwete, Rais mstaafu wa awamu ya nne amesema kuwa asingependa kuhusishwa na ukosoji wa utendaji wa serikali ya awamu ya tano iliyo chini ya Rais John Pombe Magufuli, anaandika Charles William.

Kikwete ameyasema hayo kupitia ukurasa wake wa mtandao wa Twitter ikiwa ni siku nne tangu anukuliwe na vyombo mbalimbali vya habari akisema maendeleo hayana maana ya kuharibu mazuri uliyoyakuta jambo lililohusishwa na kumkosoa Rais Magufuli. 

“Nimestaafu naomba niachwe nipumzike. Nisingependa kuhusishwa na siasa za mtandaoni dhidi ya Serikali. Namuunga mkono Rais na serikali yake,” ameandika leo Kikwete.

 

Katika kutilia msisitizo Kikwete amesemema, “Nasikitishwa sana na matumizi mabaya ya picha zangu mtandaoni hususan watu kunilisha maneno kwa kutaka kutimiza malengo yao ya kisiasa.”

JK alisema nini UDSM mpaka kuzua mjadala mitandaoni na katika vyombo vya habari kiujumla?

Rais mstaafu Kikwete ambaye pia ndiye mkuu wa chuo hicho alikuwa akihutubia ndani ya ukumbi wa Nkurumah katika maadhimisho ya miaka 55 ya kuanzishwa kwa UDSM alieleza yafuatayo katika sehemu ya hotuba yake;

“Lazima ukishakuwa mpya watu waone kama kuna mambo mapya, lakini mapya ya maendeleo (akasita na kucheka..), siyo mapya ya kubomoa kule tulipotoka.”

Kauli hii ilitafsiriwa kama ni kuikosoa serikali ya Rais Magufuli kwa namna ambavyo imekuwa ikichukua hatua mbalimbali za kufumua mfumo wa utendaji uliokuwepo katika awamu iliyopita hata kama baadhi ya mambo hayo ni mazuri.

Baadhi ya mambo yanayotajwa kuwa yalikuwa mazuri lakini Serikali ya Rais Magufuli imeamua kuyabadili ni kurushwa kwa matangazo ya Bunge ya moja kwa moja (live), kutoa uhuru kwa vyombo vya habari na kuruhusu mikutano ya hadhara, kutofukuza wafanyakazi bila kuwapa haki ya kujitetea pamoja na kutoa mikopo ya vyuo vikuu kwa wanafunzi wengi zaidi.