Zinazobamba

KUELEKEA UCHAGUZI MDOGO WA MARUDIO..NEC YAANZA KUWAWEKEA VIZINGITI WAPIGA KURA HAWA,SOMA HAPO KUJUA



Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi (NEC), Ramadhani Kailima. 
WAKATI ikiwa imebakia mwezi mmoja tu kuelekea kwenye uchaguzi mdogo wa marudio  wa udiwani kufanyika kutokana na kata mbali mbali kuwa wazi,TUME ya Taifa ya Uchaguzi(NEC), imesema hati ya kiapo cha mahakama ya kudhibitisha majina ya mtu(Affidavit), haitatumika katika kupiga kura kwenye uchaguzi mdogo wa kata 43.
Hati za kupigia kura zitakazotumika katika uchaguzi huo ni leseni ya udereva, Kitambulisho cha Utaifa  na hati ya kusafiria.

Hayo yamebainishwa Dar es Salaam leo na Mkurugenzi wa NEC, Ramadhani Kailima akizungumza na Fullhabari.blog na kwamba matumizi ya hati hizoyatapunguza biashara ya watu kununua au wizi wa vitambulisho vya kupigia kura na kuongeza uwanda mpana wa mtu kupiga kura. 

"Hati ya kiapo cha mahakama cha kuthibitisha majina yako na taarifa zako haitaruhusiwa kupigia kura katika uchaguzi huu mdogo, kuna hati tatu tu ambazo zitaruhusiwa kutumika,"amesema.

Kailima amesema hati mahakamani haitatambuliwa na kutoruhusiwa kwa namna mbili ikiwemo kutokuwa na mtiririko wa majina ya mpiga kura na kwamba yanatakiwa mtiririko huo ufanane kwa maneno na herufi.

"Huna kitambulisho cha NIDA, leseni ya udereva, hati ya kusafiria umekwenda mahakamani umeapa haitakubalika, Tume kwa mamlaka iliyonayo imesema kwa mujibu wa Sheria mwenye vitambulisho vitatu na hivi vitatumika kwenye uchaguzi mdogo wa Kata 43,"amesema.

Amesema ukifika uchaguzi Mkuu, Tume itatoa maelekezo mengine na kwamba hayo ni maelekezo ya uchaguzi mdogo wa Kata hizo kutokana na matakwa ya sheria na kutokuboreshwa kwa daftari la kudumu la wapiga kura.

"Hii ndiyo tunaanza kupiga kura kwa hati hizo tatu, kutokana na kutokuboresha daftari,ili isipoteze haki ya mtu kupiga kura na tumeona uwanda wa NIDA ulipofika watu wanaweza kuwa na vitambulisho, pia leseni za udereva watu wengi wanazo ikiwemo maeneo ya vijijini madereva wa pikipiki wanazo"amesema.

Amesema fomu za uchaguzi huo imeanza kutolewa leo hadi Oct 26,mwaka huu ambazo zinapatikana kwa Mkurugenzi wa Halmashauri au Msimamizi wa Uchaguzi ngazi ya Kata.

"Mwisho Oct 26 mwaka huu saa kumi jioni, baada ya hapo fomu za wateule zitawekwa sehemu za wazi ili kutoa fursa ya kuwekewa pingamizi ambapo wanaoruhusiwa kufanya hivyo ni Mgombea mwenza wa Udiwani kwenye Kata husika.

"Si kutoka Kata nyingine, Msimamizi wa Uchaguzi ngazi ya Jimbo na Msajili wa Vyama vya siasa kutokana na sheria za gharama za uchaguzi na kama msimamizi wa uchaguzi akimwekea pingamizi mgombea itabidi aweke rufaa ikishindikana inaamia NEC  iwapo kama pande mojawapo ikishindwa kukubaliana na maamuzi ya kamatiya rufaa ya pingamizi itakuwa kesi baada ya uteuzi.

Katika uchaguzi huo wapiga kura zaidi ya 300,000 wanatarajia kupiga kura katika vituo zaidi ya 800 na Kata 43.