Zinazobamba

Serikali imekipatia Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) zaidi ya Sh. bilioni 6.7, SUMATRA YAKIPIGIA MFANO


Image result for MGANILWA NIT
Serikali imekipatia Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) zaidi ya Sh. bilioni 6.7 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya ufundishaji wa chuo hicho, ikiwemo kujenga madarasa na nyumba za walimu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mkuu wa chuo hicho, Profesa Zacharia Mganilwa alisema fedha hizo ambazo zimetengwa katika bajeti ya mwaka huu wa fedha zitasaidia kufanya NIT itoe wataalam wenye weledi wa kushindana katika soko la kimataifa la ajira.
Prof. Mganilwa alisema chuo kimejipanga pia kuendelea kutoa wataalam waliobobea katika fani mbalimbali ambazo zitaendana na mahitaji ya sasa ya taifa na kushiriki katika shughuli za ujenzi wa taifa, ikiwemo ujenzi wa bomba la mafuta kati ya Uganda na Tanzania, upanuzi wa bandari na shughuli nyingine za kijamii na kiuchumi.
“Chuo kinatoa mafunzo katika mfumo unaotambulika na Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi (NACTE) na mfumo unaozingatia elimu kwa vitendo ambao unampa uwezo mkubwa mwanafunzi kushindana katika soko la ajira,” alisema Prof. Mganilwa.
Alisema Chuo hicho kinadahili wanafunzi waliofaulu kidato cha nne kwa masomo ya cheti na diploma na wanafunzi waliomaliza kidato cha sita kwa masomo ya shahada.
Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mamlaka ya Usafiri wa Majini na Nchikavu (Sumatra), Giliard Ngewe alisema NIT ni muhimili wa uchumi na kwamba bila usafirishaji huo uchumi hauwezi kukua.
Ngewe alisema wakati wa awamu ya kwanza ya Serikali kulikuwa na mashirika ya usafirishaji ya mikoa ambayo yalichangia kwa kiasi kikubwa katika kujenga uchumi wa taifa, ambayo "yaliongozwa na wataalamu kutoka chuo hiki".
Akizungumza katika hafla hiyo, rais wa serikali ya wanafunzi wa NIT, Stambuli Mwombeki alipongeza juhudi zinazofanywa na Rais John Magufuli ya uboreshaji wa miundombinu ya usafirishaji na kwamba vijana wanaohitimu katika chuo hicho wataweza kupata ajira katika sekta hizo.
Alisema miongoni mwa mafunzo yanayotolewa chuoni hapo ni uhandisi wa vyombo vya usafiri wa anga, utalaamu wa usafirishaji wa njia ya reli ambayo inaboreshwa na kuwa ya kiwango cha kisasa pamoja na urubani na huduma za denge.
Chanzo: Nipashe