Zinazobamba

TUNAMUOMBA RAIS ATUMIE MAMLAKA YAKE KUTANGAZA BALAA LA NJAA TANZANIA: ACT-WAZALENDO







 Chama Cha ACT –Wazalendo kimesema tatizo la njaa bado lipo Nchini na kwamba kama Taifa hatua za makusudi zinapaswa kuchukuliwa ikiwemo kutangaza balaa hilo ili kuwaokoa wananchi wa hali ya chini.
Hayo yamebainishwa na katibu wa kamati ya maendeleo ya jamii kutoka chama cha ACT-Wazalendo Bi. Janeth Rithe wakati akizungumza na Waandishi wa habari  ofisini kwake.
Amesema kwa mujibu wa utafiti walioufanya kupitia mikoa minane, wamebaini kuwa chakula muhimu kama unga wa mahindi na Maharagwe zimeanza kuadimika na kusababisha bidhaa hiyo kuongezeka bei kwa kasi ukilinganisha na miezi mitatu ya Nyuma.
“Takwimu zetu zinaonyesha kuwa bei ya unga, maharage na vyakula vingine muhimu kwa wananchi walio wengi vimepanda kutoka shilingi 900/= kwa kilo katika miezi mitatu iliyopita hadi kufikia shilingi 2000/= kwa hivi sasa” Alisema
Amesema kupanda kwa bei ya vyakula hivyo muhimu kwa kasi kubwa namna hiyo ni kiashiria tosha kuwa upatikanaji wa vyakula hivyo umeshuka sokoni na hivyo kufanya mahitaji kuwa makubwa kuliko usambazaji wake.(supply and demand concept)
 Amesema utafiti huo unaonyesha kuwa Mkoa wa Arusha bei ya unga wa mahindi kwa sasa ni Shilingi 1700, wakati bei ya Maharagwe ni Shilingi 2200, Jiji la Dar es Salaam Bei ya unga wa mahindi ni Shilingi 2000, huku bei ya Maharage Shilingi 3000, Mkoa wa Dodoma bei ya mahindi 1600 na maharage  Shilingi 2200 na Mkoa wa Morogoro bei ya unga wa mahindi 18,000 na maharage 18,000.
“Kutokana na hali ya chakula nchini, na hali ya maisha kwa wananchi kwa ujumla, Chama cha ACT Wazalendo kinatoa wito kwa serikali ya CCM kuchukua hatua za haraka kurekebisha mambo, ikiwemo kuchochea Tija kwenye Kilimo.” Alisema
Ameongeza kusema uamuzi wa Serikali ya CCM kupunguza bajeti ya ruzuku ya mbolea kutoka shilingi bilioni 78 mwaka 2015/16 mpaka bilioni 10 mwaka 2016/17 haukuwa uamuzi sahihi na umechangia katika kuwapunguzia wananchi uwezo wa kuzalisha.

Serikali  inapaswa kuchochea kilimo kwa kuongeza bajeti eneo hilo ili kukuza uzalishaji ambao umeanza kushuka kutoka 2.5% kwaka 2016 hadi kufikia 0.6% kwa sasa.
Tunataka Serikali itenge pesa kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji ili kupunguza utegemezi wa kilimo cha mvua ambazo zinazidi kutokutabirika. Serikali ijenge maghala ya kutosha na Bunge liongeze bajeti ya hifadhi ya Chakula ya Taifa. Alisema
Kutokana na hali ya ukame katika mikoa mingi nchini, na hali ya chakula kuendelea kudorora, tunamshauri Rais atumie mamlaka yake kikatiba kutangaza rasmi janga la ukame nchini na hali mbaya ya chakula.