Zinazobamba

KUKAMATWA KWA MANJI KWAANZA KUIUMIZA KLABU YA YANGA,SASA HALI YAWA MBAYA KIFEDHA,SOMA HAPO KUJUA

YANGA imekiri kuwa na wakati mgumu kiuchumi, lakini imeapa kupambana kutetea taji lake la Ligi Kuu bara na kufanya vizuri kwenye michuano ya kimataifa ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Mabingwa hao watetezi wa Ligi Kuu wapo nafasi ya pili kwenye msimamo wakiwa na pointi 49 nyuma ya Simba yenye pointi 54 kileleni.
Yanga ina faida ya mchezo mmoja kibindoni.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Yanga, Charles Mkwasa alisema wana hali ngumu kiuchumi kutokana na Mwenyekiti na mfadhili Yusuf Manji kupata matatizo, lakini atashirikiana na viongozi wenzake kuhakikisha mambo yanakwenda sawa.
Manji anatuhumiwa kutumia dawa za kulevya na kuajiri wafanyakazi wa kigeni bila kufuata taratibu, suala linalodaiwa kukwamisha masuala yake mengi yakiwemo kuigharamia Yanga kama ilivyo siku za nyuma.
“Hatupo vizuri kifedha ni kweli hiyo ni kutokana na matatizo ya mfadhili wetu hivyo uongozi ndio tunasimamia mambo yote kwa sasa kuhakikisha hatukwami mahali, ikiwemo ushiriki wetu wa ligi pamoja na michuano ya kimataifa,” alisema.
Yanga inatarajiwa kucheza na Zanaco ya Zambia katika mechi ya Ligi ya Mabingwa katikati ya mwezi ujao. Mkwasa aliyewahi kucheza na kufundisha timu hiyo pia aliajiriwa kwenye nafasi hiyo katikati ya mwezi huu akichukua mikoba ya Dk Jonas Tiboroha aliyesitishiwa mkataba wake.
Yanga kesho inatarajiwa kushuka kwenye uwanja wa Taifa kuikaribisha Ruvu Shooting katika mechi yake ya Ligi Kuu ambapo inahitaji ushindi ili kurudisha imani ya mashabiki wake walioonekana kufadhaika baada ya kupoteza mechi ya mtani wake mwishoni mwa wiki iliyopita. Akizungumzia mechi hiyo Mkwasa alisema kila kitu kiko sawa na wanaingia uwanjani kusaka ushindi kama wanavyofanya kwenye mechi zote.
“Timu imeshasahau yaliyopita na imeshajipanga kwa mchezo wetu ujao ambao tunatarajia tutashinda ili tuendelee vizuri na kampeni za kutetea ubingwa,” alisema Mkwasa.
Aidha katika hatua nyingine, Shirikisho la soka Tanzania (TFF) limerejesha mechi za Ligi Kuu kwenye uwanja wa Jamhuri Morogoro na Jumapili hii Mtibwa Sugar itaikaribisha Yanga. Awali TFF ilifungia uwanja huo kutumika kwenye mechi za ligi baada ya kuonekana kuchakaa sehemu ya kuchezea ikiwa haina nyasi.